Wajumbe wa kituo cha Taarifa na Maarifa (Mtandao wa Nyuki) kutoka kata ya Mwadui-Lohumbo wakiimba ngonjera yenye ujumbe wa changamoto mbalimbali zinazowakabili kwenye kata yao.


 
Ofisa kutoka TGNP Makao Makuu, Nyanjura Kalundo akitoa maelezo kwenye kikao maalumu cha uwasilishaji wa taarifa na kuelezea changamoto zinazowakabili wakazi wa kata ya Mwadui - Lohumbo.


Wajumbe wakifuatilia kwa makini kikao kinavyoendelea.

WANAFUNZI wa kike katika shule za msingi na sekondari wilayani Kishapu hupoteza siku 40 za masomo kwa kila mwaka kutokana na shule nyingi wilayani humo kutokuwa na vyumba maalumu vya kujihifadhi pale wanapokuwa katika siku zao.



Hali hiyo imebainishwa na wajumbe wa kituo  cha Taarifa na Maarifa kutoka kata ya Mwadui-Lohumbo wilayani Kishapu mkoani Shinyanga kwenye kikao maalumu kilichoandaliwa na Mtandao wa Jinsia nchini - TGNP  makao makuu Dar es Salaam kwa ajili ya kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili wakazi wa kata Mwadui-Lohumbo.

Wakisoma risala yao mbele ya mgeni rasmi, Kaimu mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, George Kessy wanakituo hao walisema watoto wa kike hushindwa kuhudhuria masomo wanapokuwa kwenye siku zao kwa hofu ya kuaibika kutokana na ukosefu wa chumba kitakachowawezesha kujirekebisha na kujiweka katika hali ya usafi.

Walisema hali hiyo huchangia washindwe kufuatilia vyema masomo yao na kusababisha kupata matokeo yasiyo mazuri katika mitihani yao ya mihula na hata ile ya majaribio ambapo waliomba halmashauri ya wilaya iangalie uwezekano wa kujenga vyumba maalumu mashuleni vitakavyotumiwa na watoto wa kike wanapokuwa katika siku zao.

Akijibu changamoto hiyo, Ofisaelimu msingi wilayani Kishapu, Richard Mutatina alikiri kuwepo na changamoto hiyo ambapo alisema tayari halmashauri yake imeanza kuchukua hatua za kujenga vyumba maalumu mashuleni kwa kushirikisha nguvu za wananchi ili kuweza kuwasaidia watoto wa kike.

“Ni kweli watoto wengi wa kike hushindwa kuhudhuria masomo pale wanapoingia katika siku zao, hali hii inachangiwa na kukosa eneo maalumu la wao kujihifadhi wanapokuwa shuleni, na mara nyingi huona aibu, takwimu zinaonesha kwa mwaka hupoteza siku 40 za masomo kutokana na kuwa katika siku zao,”

“Hata hivyo tayari halmashauri yetu imeanza kulifanyia kazi tatizo hili na kuangaliwa uwezekano wa kujenga chumba kimoja katika kila shule kwa ajili ya kuwasaidia watoto hawa, tunatarajia kushirikisha pia nguvu za wananchi ili kufanikisha ujenzi huu,” alieleza Mutatina.

Akijibu hoja ya uhaba wa vyumba vya madarasa na ukosefu wa shule za msingi katika vijiji vya Nyenze na Mwanholo, Mutatina alikiri kuwepo na upungufu mkubwa katika vyumba vya madarasa na madawati hali iliyochangiwa na wazazi wengi kuitikia wito wa kupeleka watoto wao shuleni.

“Suala la upungufu wa vyumba vya madarasa na madawati kwa sasa halipo katika kata ya Mwadui-Lohumbo pekee, ni wilaya nzima na huenda pia ni katika maeneo mengi nchini, hii inatokana na mpango ulioanzishwa na serikali wa elimu bure, wazazi wengi wamehamasika kupeleka watoto wao shule,” alieleza Mutatina.

Akifafanua alisema mpaka hivi sasa wilaya ya Kishapu ina upungufu wa vyumba vya madarasa 792 ikiwemo pia ukosefu wa nyumba za walimu, tayari kiasi cha shilingi milioni 279.5 zimetengwa kwa mwaka huu wa fedha kwa ajili ya ujenzi wa vyumba 33.

Pia alisema halmashauri imetenga kiasi cha shilingi 435,375,000 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa nyumba 19 za walimu ambazo zitapunguza kwa kiasi fulani upungufu wa nyumba hizo katika baadhi ya shule za msingi na sekondari.

“Idadi ya wanafunzi walioandikishwa ni wengi sana, tuna wanafunzi wapya 15,000 wa darasa la kwanza, kwa upande wa madarasa ya awali wapo wanafunzi zaidi ya 10,000 hii imechangia kujitokeza upungufu mkubwa wa madawati, tayari tumetenga shilingi 280,000,000 kwa ajili ya kukabiliana na upungufu wa madawati,” alieleza Mutatina.


Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top