Ofisa kutoka dawati la Jinsia wilayani Kishapu mkoa wa Shinyanga, Amina Masunga akiongea na wajumbe kutoka Kituo cha Taarifa na Maarifa (Mtandao wa Nyuki) katika kata ya Mwadui-Lohumbo wilayani Kishapu kwenye kikao kilichoandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)



MTANDAO wa Jinsia nchini (TGNP) umepongezwa kwa kazi nzuri ya ya kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kupiga vita vitendo vya ukatili wa kijinsia na jinsi ya kudai haki zao za msingi wanazostahili kupatiwa ma serikali.


Pongezi hizo zimetolewa na kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu, George Kessy alipokuwa akifungua kikao maalum cha utoaji taarifa na kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili wakazi wa kata ya Mwadui-Lohumbo wilayani Kishapu kilichoandaliwa na Mtandao wa Jinsia nchini (TGNP).

Kessy alisema juhudi zinazofanywa na Mtandao wa Jinsia nchini zimewezesha wananchi wengi waishio vijijini kuelewa haki zao za msingi sambamba na kupiga vita vitendo vya ukatili wa kijinsia ambapo pia wameanza kushiriki katika shughuli za kijamii kwa hiari yao bila ya kushurutishwa.

Baadhi ya wana kituo cha Taarifa na Maarifa pamoja na wataalamu wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu wakifuatilia kikao.

“Nichukue fursa hii kuwapongeza wenzetu wa Mtandao wa Jinsia - TGNP kwa kazi nzuri wanazozifanya kwa jamii ya watu wa Kishapu katika kuwaelimisha juu ya masuala muhimu ikiwemo kutambua haki zao na jinsi ya kuzidai kutoka kwa mamlaka husika,”

“Kazi nzuri mnazozifanya za kuwaelimisha wananchi tayari zimeanza kuonesha matokeo chanya, hasa katika suala la wananchi kushiriki katika mikutano ya hadhara inayojadili masuala mbalimbali ya maendeleo katika maeneo yao, haya ni mafanikio ikilinganishwa na hapo awali, tunakupongezeni sana,” alieleza Kessy.


Wana kituo wakionesha moja ya igizo kuhusu changamoto zilizopo kwenye zahanati zao kwenye kata ya Mwadui-Lohumbo wilayani Kishapu mkoa wa Shinyanga.
Alisema kutokana na wananchi kuibua changamoto zilizoko katika maeneo yao, serikali kwa upande wake hivi sasa imeanza kuchukua hatua za kutatua changamoto hizo katika sekta za afya, maji, madini na kilimo na kwamba hali hiyo huenda ingechukua muda kushughulikiwa iwapo wananchi wasingapaza sauti zao.

Akijibu hoja ya uhaba wa vyumba vya madarasa katika shule za msingi, Kessy alisema tayari serikali imeanza kuchukua hatua za kukamilisha majengo yaliyoanza kujengwa kwa kushirikiana na wananchi na kwamba halmashauri ya Kishapu imetenga kiasi cha shilingi 279,542,514 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba 33.

“Naamini tukishirikiana na wananchi katika suala hili tutaweza kupunguza tatizo, kwa sasa tunawahimiza wao wajenge maboma na halmashauri itafanya kazi ya kumalizia kwa kuyaezeka,  hii ni kwa mujibu wa sera ya nchi inayowataka wananchi kushirikiana na serikali yao katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo,” alieleza Kessy.

Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top