Mmoja wa wahitimu kidato cha nne katika shule ya sekondari Kom akipokea kutoka kwa mgeni rasmi, Mohamed Kahundi cheti cha kuhitimu elimu ya sekondari.
Mgeni rasmi katika mahafali ya nane ya wahitimu wa kidato cha nne KOM sekondari akiwahutubia wahitimu, wazazi na waalikwa mbalimbali katika sherehe za mahafali zilizofanyika katika viwanja vya shule ya KOM, Kushoto kwa mgeni rasmi ni mkurugenzi wa KOM Sekondari, Mr. Jackton Koyi na wa kwanza kulia ni mmoja wa wadau wa shule hiyo, meneja wa Tawi la CRDB Shinyanga, Mr. Said Pamuhi.
WAZAZI mkoani Shinyanga wamekumbushwa wajibu wao wa kuwajengea mazingira mazuri watoto wao ikiwemo kuwafundisha mila na desturi zinazofaa ili kuepuesha ongezeko la mmomonyoko wa maadili miongoni mwa vijana hapa nchini.


Wito huo umetolewa na Ofisa elimu mkoani Shinyanga, Mohamedi Kahundi aliyekuwa mgeni rasmi katika mahafali ya nane ya wahitimu wa kidato cha nne wa shule ya sekondari Kom iliyopo manispaa ya Shinyanga.

Kahundi alisema kumomonyoka kwa maadili miongoni mwa vijana wengi katika siku za hivi karibuni ikiwemo uvaaji wa mavazi yasiyofaa kunachangiwa na tabia ya baadhi ya wazazi kutokuwa na utamaduni wa kukaa na watoto wao kuwafundisha masuala muhimu ya kijamii ikiwemo na tabia nzuri.

Wahitimu wa kidato cha nne wakiingia kwenye uwanja wa sherehe


Mmoja wa wahitimu akipongezwa na mmoja wa wamiliki wa shule muda mfupi baada ya kukamilisha zoezi la ukataji wa keki.



Wahitimu wakiburudisha wazazi na wageni waalikwa.



Zoezi la ulishaji keki mgeni rasmi na mkurugenzi wa Shule.
“Tuna tatizo la kuporomoka kwa maadili miongoni mwa vijana wetu, yapo mambo yanafanywa ambayo yanapingana na mila na desturi zetu hapa nchini, mfano uvaaji wa suruali mitepesho, au vimini vinavyobana kwa watoto wa kike, haya siyo maadili ya kitanzania,”

“Hali hii inachangiwa kwa kiasi kikubwa na sisi wazazi wenyewe, maana tumeacha ile mila muhimu ya kukaa na watoto wetu usiku na kuwapa nasaha juu ya maisha wanayopaswa kuishi, pia kufuatili mienendo ya masomo yao, jukumu hili wengi mmeliacha kwa walimu pekee, nasema tubadilike,” alieleza Kahundi.

Alisema ni muhimu wazazi wakahakikisha wanashirikiana na walimu katika malezi ya watoto wao hasa katika suala la kuwafundisha maadili mema na kutowaruhusu kuvaa nguo zisizofaa au kujiingiza kwenye makundi yatakayochangia wajikute wakifanya vitendo visivyofaa ikiwemo matumizi ya madawa ya kulevya.

Kwa upande mwingine Kahundi aliipongeza Bodi ya shule ya Kom kwa kuisimamia vyema shule hiyo hasa upande wa ufundishaji hali iliyochangia iwe na matokeo mazuri katika mitihani ya kumaliza kidato cha nne na ile ya kidato cha pili na hivyo kusababisha wazazi wengi kupeleka watoto kwenda kusoma kwenye shule hiyo.


Mgeni rasmi, Ofisa elimu mkoani Shinyanga, Bw. Mohamedi Kahundi  (katikati) mwenyekiti wa Bodi ya shule ya Sekondari KOM, Bw. Peter Puguru (wa kwanza kushoto) na Mkurugenzi wa shule, Bw. Jacton Koyi wakiingia rasmi katika eneo la sherehe za mahafali ya nane ya wahitimu wa kidato cha nne.

“Nichukue fursa hii kuipongeza bodi ya shule na mkurugenzi wake, kwa kweli mnajitahidi, ofisini kwangu sina malalamiko yoyote kutoka kwa wazazi wakiulalalamikia uongozi wa uongozi wa shule hii ni tofauti na shule nyingine, lakini pia tabia ya kutowachuja watoto wenye uwezo mdogo, binafsi imenifurahisha,” alieleza Kahundi.

Akifafanua alisema baadhi ya shule binafsi zimekuwa na utaratibu wa kuwachuja watoto wenye uwezo mdogo na kuwafukuza shule bila kujali fedha walizolipa wazazi ambapo kwa shule ya Kom watoto wa aina hiyo hupewa kipaumbele katika kufundishwa ili waweze kuwa na wenzao wenye uwezo mzuri.

Mgeni rasmi alitoa wito kwa wazazi na walezi wenye watoto waishio mkoani Shinyanga wawapeleke watoto kusoma katika shule hiyo badala ya kuhangaika kwenda kutafuta shule nyingine nje ya mkoa wakati tayari mkoa wao una shule inayotoa masomo kwa kiwango cha juu na matunda yake yameonekana kwa wengi.




Mgeni rasmi akipata maelezo kutoka kwa wanafunzi wa fani mbalimbali alipotembelea kujionea maonesho ya kazi mbalimbali wanazofundishwa shuleni kwao.

Mmoja wa wadau wa Kom Sekondari akifurahia jambo pamoja na mmoja wa wajumbe wa Bodi ya shule ya Kom.
Awali katika taarifa yake mkurugenzi wa Sekondari ya Kom Jackton Koyi alisema shule hiyo imekuwa na mafanikio makubwa tangu ilipoanzishwa miaka 11 iliyopita na kwamba siri ya mafanikio hayo ni ushirikiano mkubwa unaooneshwa kati ya wazazi na uongozi wa shule.

Alisema moja ya mafanikio yaliyopatikana mbali ya kuwa na matokeo mazuri ya wahitimu wa kidato cha pili na cha nne katika mitihani ya kitaifa hivi bado kuna changamoto kadhaa zinazowakabili ikiwemo suala la wazazi kuchelewa kulipa ada na kuchelewa kwenda shule.

“Mheshimiwa mgeni rasmi tuna changamoto kadhaa zinazotukabilia pamoja na kwamba yapo mafanikio yaliyopatikana, hii ni ongezeko la gharama za uendeshaji, kukosekana kwa miundombinu kadhaa, nyumba za walimu, jengo la jiografia na barabara za ndani,” alieleza Koyi.

Aidha mkurugenzi huyo amewashukuru wazazi wote na wadau mbalimbali wa shule ya KOM kutokana na ushirikiano wao mkubwa wanaouonyesha katika kuchangia maendeleo ya shule hiyo na kuiwezesha ipige hatua katika suala zima la kitaaluma.

“Kwa ridhaa yako naomba sasa nigeukie kwa wahitimu wetu wa leo, tunao wahitimu 144 kati yao wasichana ni 60 na wavulana 84 wote wameweka juhudi kubwa katika masomo yao na kwa kuwa, “…Mcheza kwao hutunzwa, punde utawatunuku vyeti vyao, vijana hawa wana matumaini na ndoto za hali ya juu,”

“Shule ya KOM imewaandaa kujiwekea malengo ya juu katika maisha yao, muda wote tuliokuwa nao, tumewapa elimu na ujuzi stahili, tumewafunza upendo, wema, huruma, ukarimu, busara, ubunifu, uvumilivu, heshima na ushujaa,” alieleza Koyi.,

Katika hatua nyingine Koyi alisema hivi sasa shule hiyo inafanya maandalizi kwa ajili ya kuanzisha masomo ya kidato cha tano na sita ili kuwapunguzia wazazi tatizo la kuhangaika kutafuta shule nyingine kwa watoto wao wanaokuwa wamefaulu vizuri mitihani yao ya kumaliza kidato cha nne.

Kwa upande wao wazazi, walezi na wageni waalikwa mbalimbali walijitokeza kuchangia harambee kwa ajili ya kusaidia ujenzi samani zitakazowekwa kwenye bweni la wasichana watakaojiunga na masomo ya kidato cha tano mapema mwanzoni mwa mwaka 2017 ambapo kiasi cha shilingi milioni 1.9 zilichangwa.


Mgeni rasmi akiweka mchango wake wa shilingi 300,000 kwa ajili ya kuchangia ununuzi wa samani katika bweni la wasichana watakaojiunga na kidato cha tano mwakani.



Wazazi na walezi wa kike walijitokeza kwa wingi kuchangia harambee ya kukusanya fedha kwa ajili ya ununuzi wa samani katika bweni la wasichana wa kidato cha tano.


Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top