Sehemu ya magunia ya mahindi yaliyohifadhiwa kwenye ghala la NRFA kanda ya Shinyanga ambayo wabunge yanaonesha dalili za kuanza kubanguliwa na wadudu waharibifu.

Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini Mohamed Mgimwa (mwenye T.shirt ya pundamilia) akiwaongoza wabunge wenzake kukagua ghala la wakala NRFA Kanda ya Shinyanga, kushoto ni mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack.

Baadhi ya wabunge ambao ni wajumbe wa Kamati ya kudumu ya bunge ya Maji, Kilimo na Mifugo wakifuatilia kwa umakini mkubwa taarifa inayotolewa kwao na Mtendaji mkuu wa wakala wa Taifa wa Hifadhi ya chakula (NRFA) katika ghala la Kanda ya Shinyanga.
SERIKALI imeshauriwa kuangalia uwezekano wa kuanza kuuza mahindi yaliyohifadhiwa katika maghala ya wakala wa Taifa wa Hifadhi ya chakula nchini (NRFA) ambayo baadhi yake yapo katika hatari ya kuanza kuharibiwa na wadudu waharibifu wa mazao.
 
Ushauri huo umetolewa mjini Shinyanga na wabunge wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji, Kilimo na Mifugo iliyokuwa ikitembelea miradi mbalimbali iliyopo chini ya kamati hiyo inayotekelezwa mkoani Shinyanga.
 
Mbali ya hofu ya kuharibika kwa mahindi hayo ambayo kumbukumbu zinaonesha yalinunuliwa katika msimu wa 2014/2015 pia wabunge walishangazwa na kitendo cha serikali kuendelea kuyahifadhi wakati maeneo mengi nchini wananchi wanahitaji chakula cha kununua kwa bei nafuu kutokana na bei hivi sasa kuwa juu.
 
Wakiwa katika ghala la akiba ya chakula (NRFA) mjini Shinyanga wabunge wa kamati hiyo wakiongozwa na mwenyekiti wao, Mary Nagu walishuhudia sehemu ya magunia ya mahindi yaliyomo ndani ya ghala hilo yakiwa na wadudu na baadhi yake yakitoa ungaunga kuashiria kuanza kushambuliwa na wadudu.
 
Wabunge walionesha mshangao kutoka na hali waliyojionea ambapo walishangazwa na kitendo cha serikali kuendelea kuhifadhi idadi kubwa ya chakula katika maghala yake huku maeneo mengi nchini ikiwemo wilaya 55 zikiwa na uhaba mkubwa wa chakula na wananchi wakiuziwa debe moja la mahindi kati ya shilingi 20,000 hadi 25,000.
 
 
Wabunge wakitoa ushauri wao kwa viongozi wa serikali akiwemo Naibu waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi nchini Ole Nasha kuhusiana na suala la kuuzwa kwa magunia ya mahindi ambayo yanaonesha dalili za kutaka kuharibiwa na wadudu.
 
“Mheshimiwa mwenyekiti hii hali inatushangaza, ni ajabu kuona chakula kipo cha kutosha lakini huko nje wananchi wanahangaika na hivi sasa wanauziwa mahindi kwa bei kubwa, lakini cha ajabu haya yaliyopo hapa tumejionea wenyewe yameanza kubunguliwa na wadudu, ipo hatari yataharibika,”
 
“Katika taarifa ya NRFA wamesema moja ya changamoto waliyonayo ni uhaba wa fedha, hiki ni kichekesho, kwa nini wasiuze mahindi  waliyonayo zaidi ya tani 8,000 wakati hali ya soko ni nzuri, ni bora wayauze ili wapate fedha na wanunue mengine mapya,” alieleza Mohamedi Mgimwa mbunge wa Mufindi Kaskazini.
 
Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Uzini, Salum Rehani alisema iwapo serikali haitochukua hatua ya kuruhusu kuuzwa kwa mahindi hayo ipo hatari yakakosa soko baada ya wananchi kuanza kuvuna mavuno mapya hivi karibuni na kwamba wanachohitaji wananchi ni chakula cha bei nafuu na siyo cha bure.
 
Hata hivyo kwa upande wake Kaimu Ofisa mtendaji mkuu wa NRFA, Deusdedit Mpazi alikanusha madai ya mahindi kuwa katika hatari ya kuharibika kwa vile mara kwa mara hufanyika ukaguzi wa kuangalia iwapo hayajaingiliwa wadudu waharibifu.
 
“Mheshimiwa mwenyekiti si kweli kwamba mahindi haya yapo katika hatari ya kuharibika, hawa wadudu mnaowaona hapa hawana madhara makubwa, ni wadudu visumbufu tu, na hivi karibuni tunatarajia kuanza zoezi la kupulizia dawa, hivyo hayawezi kuharibika kama mnavyohofia,” alieleza Mpazi.
 
Akizungumzia suala la mahindi hayo kutopelekwa kwa wananchi ili yauzwe kwa bei nafuu, Naibu waziri wa Kilimo, mifugo na uvuvi, Ole Nasha alisema hofu ya serikali ni kuona mahindi hayo yatakapopelekwa kwa wananchi kuangukia kwenye mikono ya walanguzi na kuuzwa kwa bei ya juu.
 
“Hatukurupuki kusambaza mahindi haya ovyo, tuko makini ili kuhakikisha pale yatakapopelekwa kwa wananchi yanawafikia walengwa husika, lakini pia tunasubiri kipindi halisi cha mavuno ili tuweze kuona kiasi halisi cha mazao kitakachopatikana, na hivyo chakula hiki kitapelekwa kwenye maeneo yenye upungufu mkubwa,” alieleza waziri.
 
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top