Nape Nnauye akiwahutubia waandishi wa habari akiwa amesimama juu ya gari lake baada ya kikao chake cha ndani kupigwa "STOOOP" na Polisi.




Khamis Mgeja katika moja ya mikutano ya chama chake cha CHADEMA.


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
MWENYEKITI wa Tanzania Mzalendo Foundation, Khamis Mgeja amelaani kitendo cha kutishiwa kwa silaha ya moto aliyekuwa waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na michezo nchini, Nape Nnauye na kwamba kitendo kilichofanyika ni ukiukwaji wa haki za kibinadamu na utawala bora.

Mgeja ambaye kwa hivi sasa ni miongoni mwa makada wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) alitoa kauli ya kulaani kitendo hicho alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mkoani Kigoma ambapo amemuomba waziri mkuu, Kassim Majaliwa asimame hadharani kuwaomba radhi watanzania kwa niaba ya serikali.

Akifafanua Mgeja aliyewahi kuwa kiongozi wa ngazi ya juu ya kimkoa ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) alisema tukio la Nape kutishiwa silaha ni moja ya matukio ya ukandamizaji wa haki za kibinadamu yanayoendelea kushamiri hapa nchini chini ya serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na CCM.

Nape Moses Nnauye

“Kwa kweli mimi binafsi pamoja na taasisi yangu ya Tanzania Mzalendo Foundation tunalaani vikali kitendo kilichotendwa hadharani na mmoja wa walinzi wa raia kutumia kumtisha raia kwa silaha ya moto kwa lengo tu la kumzuia asizungumze na wanahabari, tukio hili limetushitua na kutusikitisha,”

“Matukio haya ni ishara ya wazi ya ukandamizaji wa demokrasia na ni matumizi mabaya ya madaraka ambayo yameanza kushika kasi miongoni mwa viongozi wa serikali, wananchi wengi hivi sasa hawatendewi haki, angalieni yanayotokea kwa wafugaji, hivi karibuni vijana wawili wa wafugaji kule Bagamoyo walipigwa risasi na kufa,” alieleza Mgeja.

Aliendelea kueleza kuwa wananchi wanyonge hivi sasa wanajiuliza iwapo mtu aliyekuwa waziri wa serikali, kada maarufu ndani ya chama tawala na aliyekipigania kiweze kupata ushindi japokuwa kwa goli la mkono leo anafanyiwa hivyo na vyombo vya dola na kudhalilishwa mbele ya kadamnasi kwa wananchi wanyonge hali ingekuwaje.

“Tunashauri sasa waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ambaye ni kiongozi na msimamizi mkuu wa shughuli za serikali za kila siku, asimame hadharani kwa niaba ya serikali yake ya CCM awaombe radhi watanzania kwa matukio haya ya uvunjaji wa haki za kibinadamu na demokrasia ikiwemo ukandamizaji wa haki kibinadamu na utawala bora hapa nchini,” alieleza Mgeja.

Mwenyekiti huyo ameiomba na kuishauri serikali iache kushughulikia watu kwa vitisho bali ielekeze nguvu zake katika kuboresha maisha ya watanzania ili yawe bora na kwamba kwa sasa hali ya maisha kwa watanzania wengi imekuwa ngumu huku mfumko wa bei za bidhaa mbalimbali ukipaa kila siku.

Hata hivyo kwa upande mwingine Mgeja alimpongeza Nape kwa ujasiri aliouonesha japokuwa anapingana naye kiitikadi na kimtizamo kwa muda mrefu na kwamba kitendo alichokifanya kimeonesha uzalendo wake hasa pale alipowahamasisha vijana na watanzania kutokuwa waoga na kuwataka wasimame imara kudai haki zao.

“Haya yanayojitokeza sasa nchini tumekuwa tukiyaona nchi za wenzetu kule Zimbabwe, Congo, Rwanda, Burundi na hata jirani zetu pale Uganda, hivyo tusidanganyane kwamba hii ni Tanzania mpya tunayoitaka watanzania, tuwaombe viongozi wetu wa dini na wastaafu waisaidie nchi kuliko kukaa kimya, maana hili ni janga jipya kwa taifa letu,” alieleza.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top