Kaimu Mkurugenzi wa watoto, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na Watoto,  Margareth Mussai akihutubia zaidi ya watoto 200 katika kongamano maalumu lililofanyika katika Ukumbi wa Vijana Centre, Ngokolo Manispaa ya Shinyanga ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike ambayo kwa mwaka 2016 yamefanyika kitaifa mkoani Shinyanga.
 
Mratibu wa Shirika la Agape Aids Control Programme (AACP) la mkoani Shinyanga, Samwel Magina akitoa taarifa juu ya ukubwa wa tatizo la mimba na ndoa za utotoni mkoani Shinyanga katika Kongamano la maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa kike lililofanyika mjini Shinyanga.
SEREKALI imeombwa kutunga sheria itakayotoa adhabu kali kwa wazazi wenye tabia ya kukatisha masomo na kuwaozesha kwa lazima watoto wao wa kike bila kujali madhara wanayoyapata kutokana na kuolewa wakiwa na umri mdogo.


Ombi hilo limetolewa na watoto walioshiriki katika Kongamano la Siku ya Kimataifa ya mtoto wa kike duniani lililofanyika mjini Shinyanga ikiwa ni maandalizi ya kilele cha maadhimisho hayo yatakayofanyika kitaifa Oktoba 11, mwaka huu mkoani Shinyanga.

Watoto hao walisema wazazi wengi wamekuwa wakikimbilia kuwaozesha watoto wao wa kike bila kujali athari wanazopata ikiwemo mimba katika umri mdogo zinazoweza kusababisha kifo na kwamba tabia hiyo inaelekea kuwa sugu miongoni mwa wakazi wa mkoa wa Shinyanga kutokana na kutokuwepo kwa sheria kali inayozuia watoto wadogo kuozeshwa.

Sehemu ya watoto wa kike walioshiriki kongamano wakimsikiliza mgeni rasmi kutoka wizarani, Bi. Margareth Mussai

Mwakilishi kutoka Shirika la ICS SP, Shadia Naka akitoa neno kwa washiriki wa Kongamano.
Wakitoa ushahidi juu ya madhara wanayopata kutokana na kuolewa wakiwa na umri mdogo baadhi ya watoto walisema wengi wao wamekuwa wakiathirika kiafya na kisaikolojia ikiwemo kukosa elimu baada ya kukatishwa ndoto zao za kusoma kwa kadri ya uwezo walionao kama wenzao wa kiume wanavyopatiwa fursa hiyo.

Miongoni mwa watoto waliokatishwa masomo na kuozeshwa kwa nguvu  ambao hivi sasa wanatunzwa na Shirika la Agape Aids Control Programme (AACP) la mjini Shinyanga walipata nafasi ya kutoa ushuhuda juu ya madhara waliyoyapata baada ya kufungishwa ndoa kwa lazima na wazazi wao bila ya ridhaa yao.

Moja ya madhara waliyotaja ni vipigo kutoka kwa wanaume waliozeshwa ambao hawakuwa na mapenzi nao ya dhati kwa vile hawakuridhia kuolewa ikiwemo suala la kupata matatizo wakati wa kujifungua kutokana maumbile yao hasa ikizingatiwa umri mdogo waliokuwa nao huku wanaume wengine wakizikataa mimba wakidai si za kwao.

Sehemu ya watoto wa kike ambao ni wahanga wa mimba na ndoa za utotoni wanaotunzwa na kupatiwa elimu ya kujiendeleza na Shirika la Agape Shinyanga.

“Mimi niliolewa nikiwa na umri wa miaka 13, pamoja na kuchaguliwa kujiunga na masomo ya sekondari mwaka 2013, lakini wazazi wangu walikataa nisiende shule na badala yake walinitafutia mwanamume ili anioe, huyo alikuwa na miaka 36, nilisikia machungu makubwa hasa nilipoona wenzangu niliofaulu nao wanaendelea na masomo,”

“Wazazi wangu walipokea mahari ya ng’ombe 11 na nikaozeshwa kwa nguvu, hata hivyo kipindi kifupi tangu niolewe, mwanamume yule alikuwa akinipiga kila siku, na hata pale nilipopata ujauzito alikataa na kudai mimba ile si yaka, na kunitaka nirudi kwetu, kweli niliumia na kujuta sana,” alieleza mmoja wa wahanga wa ndoa za utotoni. 

Aliendelea kueleza baada ya muda maisha kati yake na mume wake yalikuwa magumu zaidi, pamoja na usuluhishi wa mara kwa mara uliokuwa ukifanywa na ndugu za upande wa mume, lakini tabia ya mume wake ya kumpiga na kumuumiza vibaya iliendelea na hivyo aliamua kuondoka kwa na kurudi kwa wazazi wake.

Hata hivyo alisema akiwa nyumbani kwao watu wa Shirika la Agape walikwenda kijijini kwao kuonesha sinema juu ya madhara ya ndoa na mimba za utotoni ambapo alikutana na mkurugenzi wa shirika hilo na kumuomba ajiunge ili aweze kupata nafasi ya kujiendeleza kimasomo na hivi sasa anasoma kidato cha pili. 

Kwa upande wake katibu wa Baraza la watoto mkoani Shinyanga, Christina Bakari alisema ili kukabiliana na wimbi la ndoa na mimba za utotoni ni muhimu serikali na wadau mbalimbali wa asasi za kiraia wakashirikiana kwa pamoja kukomesha tabia hiyo inayochangiwa na tamaa ya mali kwa baadhi ya wazazi.

“Matukio ya ndoa za utotoni bado ni janga kubwa kwa sisi watoto wa kike hasa katika mkoa wetu wa Shinyanga, tunaiomba serikali iweke mkazo katika kupiga vita vitendo hivi, itunge sheria kali itakayowabana wazazi na wale wote wenye kupenda kuoa watoto wadogo badala ya kuwaacha wasome,”
  
“Kutokuwepo kwa sheria inayotoa adhabu kali kwa wazazi wanaowakatisha masomo ya watoto wa kike kwa lengo la kuwaozesha ni janga kubwa kwetu sisi watoto, maana hali ya umaskini ndani ya familia imesababisha tugeuzwe kuwa vitega uchumi kwa kuozeshwa tukiwa na umri mdogo badala ya kupewa haki yetu ya kupata elimu,” alieleza Christina.

Mmoja wa wawakilishi kutoka Shirika la ICS SP kanda ya Tanzania, akitoa ujumbe kwa wananchi walioshiriki maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Siku ya Mtoto wa Kike katika kijiji cha Nhelegani Mashariki kata ya Kizumbi, manispaa ya Shinyanga.

Akizungumza katika kongamano hilo mwakilishi kutoka Shirika la ICS SP Kanda ya Tanzania, Shadia Naka alisema serikali inapaswa kuongeza mkazo katika suala zima la ulinzi wa mtoto wa kike kwa kuhakikisha kila mtoto aliyekuwa shuleni hivi sasa anamaliza masomo yake bila ya kukatishwa kwa sababu zisizokuwa na msingi.

Hata hivyo alisema pana umuhimu pia wa serikali kujenga mazingira bora yatakayowezesha upatikanaji wa elimu bora badala ya bora elimu kwa kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia katika shule zote zilizopo hapa nchini ikiwemo kuweka mkazo kwenye ujenzi wa mabweni katika shule za sekondari.

“Ni muhimu kwa serikali hivi sasa ikahakikisha inatoa kipaumbele katika suala zima la uboreshaji wa elimu hapa nchini, elimu inayotolewa iwe ni elimu bora na siyo bora elimu, isaidie kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia, lakini pia mkazo uwekwe kwenye ujenzi wa mabweni ili kuwaokoa watoto wa kike wanaoishi mbali ya shule,” alieleza Naka.
 
Naye Kaimu mkurugenzi wa watoto kutoka wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na watoto, Margareth Mussai aliwaomba watoto wa kike walioko mashuleni kutokubali kurubuniwa na vishawishi vya wanaume na badala yake wajikite katika masomo ili wapate elimu itakayowasaidia katika maisha yao ya baadae.
 
Kaimu Mkurugenzi wa watoto kutoka wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na watoto, Margareth Mussai akiwahutubia wakazi wa kijiji cha Nhelegani, kata ya Kizumbi Manispaa ya Shinyanga.

Mkazi wa kijiji cha Nhelegani, Kata ya Kizumbi akichangia hoja kuhusiana na suala la jukumu la malezi ya watoto wa kike ambapo alisema ni jukumu la wazazi wawili, baba na mama.

Kaimu Mkurugenzi wa watoto, Margareth Mussai (aliyebeba mtoto) akiwa katika picha ya pamoja na watoto wa kijiji cha Nhelegani, kata ya Kizumbi, Manispaa ya Shinyanga.
 
Alisema kutokana na ongezeko la ndoa za utotoni katika mkoa wa Shinyanga ambao unaoongoza kwa asilimia 59, wizara yake imeamua maadhimisho ya siku ya Kimataifa ya mtoto wa kike yafanyikie mkoani humo ili kuweza kutoa elimu kwa wakazi wake waweze kuachana na tabia ya kuozesha watoto wenye umri mdogo ambayo ina athari kubwa kwa mtoto wa kike.
 
“Tunaamini elimu tutakayoitoa katika kipindi cha maadhimisho haya ambayo kilele chake ni Oktoba 11, mwaka huu tutaweza kufikisha ujumbe kwa wazazi, walezi, watoto na jamii nzima kwa ujumla ili waone tatizo, na wazazi waone umuhimu wa mtoto wa kike katika kuleta maendeleo ndani ya familia,” alieleza Mussai.
 
End.



Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top