Naibu waziri Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Luhaga Mpina akishiriki kufanya usafi mjini Shinyanga

Naibu waziri katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Luhaga Mpina ametishia kuanza kuwachukulia hatua za kinidhamu viongozi na watendaji wa serikali watakaoshindwa kusimamia kikamilifu kazi ya upandaji miti na utunzaji wa mazingira katika maeneo yao.

Mpina ametoa kauli hiyo aliposhiriki katika zoezi la kufanya usafi eneo la kata ya Ibinzamata Manispaa ya Shinyanga ikiwa ni  kutekeleza agizo la Rais Dkt. John Magufuli la kuwataka watanzania kufanya usafi kila siku ya jumamosi ya mwisho wa mwezi.
Zoezi hilo ambalo kitaifa kwa mwezi huu wa Oktoba limefanyika mkoani Shinyanga ambapo viongozi mbalimbali ngazi ya mitaa, manispaa, wilaya na mkoa walishirikiana na Naibu waziri Mpina walishiriki katika kufanya usafi kwenye maeneo mbalimbali ya mitaa ya manispaa ya Shinyanga.
Mbali ya kufanya usafi pia Naibu waziri Mpina alizindua kampeni ya upandaji miti katika manispaa ya Shinyanga kwa kupanda miti kwenye shule ya msingi Ibinzamata ambapo alitoa wito kwa wakazi wa manispaa hiyo kuhakikisha wanapanda miti mingi ili kukabiliana na kasi ya uharibifu wa mazingira.
Alisema ili kuhakikisha suala utunzaji wa mazingira linapewa kipaumbele ofisi yake itaanza kufuatilia kila wilaya kuangaliaa uwajibikaji wa viongozi na watendaji wa serikali katika suala la upandaji miti katika maeneo yao na kwa watakaobainika kushindwa kuwajibika kikamilifu ataagiza wachukuliwe hatua za kinidhamu.
“Suala la utunzaji wa mazingira siyo la hiari, ni amri na ni sheria, hivyo ye yote anayekiuka anastahili kuchukuliwa hatua, na mimi nawaagiza viongozi na watendaji wote wa serikali wasimamie kikamilifu zoezi la upandaji miti katika maeneo yao, ni jukumu lao,”
“Tumepanga kila kitaifa kila mwaka tupande miti ipatayo milioni 280 hii itapandwa katika hekta 185,000, na kwa ngazi ya wilaya wapande miti milioni mbili, na ofisi yangu itakwenda kila wilaya kukagua kuona miti iliyopandwa, maana kuna watendaji huwa wanatuletea takwimu hewa,” alieleza Mpina.
Naibu waziri Mpina akizindua kampeni ya upandaji miti katika manispaa ya Shinyanga, hapa ni eneo la shule ya msingi Ibinzamata.
Alisema wilaya yo yote itakayoshindwa kutimiza lengo la kupanda miti milioni mbili kwa mwaka watendaji wake wa serikali watachukuliwa hatua za kinidhamu na kwamba dhamira ya Rais Magufuli ya Hapa Kazi Tu, haikuwa nguvu ya soda hivyo lazima watu wahakikishe wanaitekeleza kwa vitendo.
Akiwahutubia wananchi mara baada ya kumaliza kazi ya upandaji miti na kufanya usafi eneo la kata ya Ibinzamata, Mpina aliwapongeza wakazi wa manispaa ya Shinyanga kwa jinsi wanavyotekeleza vizuri suala la kufanya usafi na kuelezea kushangazwa na jinsi walivyojitokeza kwa wingi katika kazi hiyo.



“Nichukue fursa hii kukupongezeni kwa kazi nzuri, kwa mara ya kwanza nimejikuta nakosa cha kufanya baada ya kila mtaa niliokwenda na ufagio wangu kukuta ukiwa msafi kutokana na kukuta wananchi tayari wamemaliza kazi hiyo, hii ni tofauti na mikoa mingine niliyowahi kutembelea,”
“Hapa mmeonesha wazi jinsi gani mnaunga mkono agizo la Rais wetu, Dkt. Magufuli la kufanya usafi kila jumamosi ya mwisho wa mwezi, hongereni sana na endeleeni na moyo huu, maana suala la usafi ni jukumu lenu ninyi wenyewe na inasaidia kuepukana na magonjwa ya mlipuko,” alieleza Mpina.
Akizungumzia suala upandaji miti na utunzaji wa mazingira alisema maeneo mengi ya Tanzania yanakabiliwa na kasi ya uharibifu wa mazingira kutokana na ongezeko kubwa la shughuli za kibinadamu hali inayosababisha ongezeko mabadiliko ya tabia nchi.
Alisema ili kukabiliana na hali hiyo ni jukumu la watanzania wenyewe kwa ushirikiano na viongozi na watendaji wao wa serikali kuhakikisha wanashiriki kikamilifu katika suala zima la utunzaji wa mazingira na upandaji miti kwa wingi kwenye maeneo yote ili kurejesha hali ya uoto wa asili uliopotea maeneo mengi nchini.
Katika hatua nyingine waziri Mpina amesema ofisi yake inajipanga kuupatia mkoa wa Shinyanga mtambo wa kisasa wa kutengeneza mkaa unaotokana na mabaki ya takataka na maganda ya miti ili kupunguza kasi ya matumizi ya nishati ya mkaa.
Alisema tayari maombi ya kupatiwa kwa mtambo huo yaliyowasilishwa ofisini kwake na viongozi wa wilaya ya Shinyanga yameanza kufanyiwa kazi na unatarajiwa kupatikana mapema mwaka ujao na ikiwezekana utazinduliwa kipindi cha mbio za mwenge utakapokuwa mkoani Shinyanga.
Awali katika hotuba yake fupi mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro alisema pamoja na wakazi wa wilaya yake kujitahidi katika suala la utunzaji wa mazingira bado wanakabiliwa na changamoto ya ukatwaji miti kutokana na shughuli ya uchomaji mkaa, na kwamba suluhisho lake ni kupata mtambo wa kutengeneza mkaa mbadala.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top