Mkurugenzi mtendaji wa Umoja wa Vilabu vya waandishi wa habari nchini (UTPC) akifunua warsha ya siku tatu kwa waandishi wa habari kutoka mikoa ya Kagera, Shinyanga, Mara, Simiyu na Mwanza iliyofanyika jijini Mwanza.


Mkurugenzi mtendaji wa TAMWA, Valerie Msoka akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa habari wakati wa kujadili changamoto wanazokutana nazo wanapofuatilia matukio ya ukatili wa kijinsia katika mikoa yao.

                                 Mmoja wa kikongwe aliyelazimika kukimbia makazi yake baada ya kutuhumiwa kuwa ni mchawi akihojiwa na mwandishi wa habari ambapo hata hivyo hakuwa na uwezo wa kujieleza kwa ufasaha juu ya maswahibu yaliyomsibu.
 
UMOJA wa vilabu vya waandishi wa habari nchini (UTPC) unakusudia kuanzisha ushirikiano wa karibu na Chama cha wanahabari wanawake Tanzania (TAMWA) kwa lengo la kuongeza nguvu katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia hapa nchini.


Hali hiyo imebainishwa jijini Mwanza na mkurugenzi mtendaji wa UTPC,  Abubakar Karsan alipokuwa akifungua warsha ya siku tatu kwa waandishi wa habari kutoka mikoa mitano ya kanda ya ziwa iliyoandaliwa na TAMWA kwa ufadhili ya Shirika la Idadi ya watu la Umoja wa mataifa (UNFPA).

Karsan alisema uongozi wa UTPC kwa kipindi kirefu ulikuwa ukitafuta utaratibu wa jinsi ya kuwa na ushirikiano na TAMWA kwa zaidi ya miaka mitano iliyopita na hatimaye ndoto yao hivi sasa imefanikiwa baada ya kuwepo kwa mipango ya kuanzishwa kwa mahusiano kati ya taasisi hizo mbili.

Alisema kitendo cha kuanzishwa kwa ushirikiano huo kitasaidia kwa kiasi kikubwa kwa waandishi wa habari kupitia kalamu zao kuweza kupiga vita vitendo vya ukatili wa kijinsia vinavyotendeka hapa nchini ambapo pia mipango imo mbioni kuundwa kwa mtandao wa waandishi wa habari watakaojikita zaidi katika kuandika habari za ukatili wa kijinsia.

“Ndugu mkurugenzi kuja kwako UTPC kumefungua ukurasa mpya wa ushirikiano baina ya asasi zetu mbili ambazo zina mchango muhimu sana kwa maendeleo ya taaluma ya uandishi wa habari hapa nchini kwa upande mmoja na maendeleo ya nchi kwa upande wa pili,”

“UTPC tunaahidi kutoa ushirikiano madhubuti kwa TAMWA ili malengo yetu yaweze kufanikiwa, hasa katika suala zima la kupiga vita vitendo vya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia vinavyoendelea kutokea katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu,” alieleza Karsan.

Akifafanua mkurugenzi huyo alisema vyombo vya habari vina dhima kubwa katika kupiga vita vitendo vya ukatili wa kijinsia ambavyo kama vitaachwa viendelee kutendeka vinaweza kuvunja mshikamano wa kijamii na hatima yake ni mparaganyiko wa taifa.

“Athari za ukatili wa kijinsia zinaweza kuwa za kimwili, kisaikolojia au za kiuchumi jamii, pamoja na ukweli kwamba athari hizi huwapata wanawake, wanaume na watoto lakini jinsi inayoathirika kwa kiasi kikubwa ni wanawake, na hii inatokana na fikra kengeufu inayojengwa kwamba mwanamke ni kiumbe dhaifu anayestahili kusaidiwa,” alieleza Karsan.

Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa TAMWA, Valerie Msoka aliwapongeza waandishi wa habari nchini kwa juhudi zao wanazozionesha katika kuandika habari zinazohusiana na vitendo vya ukatili wakielezea madhara wanayopata watu wanaotendewa vitendo hivyo kiasi cha jamii kuanza kuanza kubadilika.

“TAMWA mara kwa mara tumekuwa tukitoa mafunzo kwa waandishi wa habari hapa nchini kwa ajili ya kuwajengea uwezo wa jinsi ya kuandika kwa ufasaha habari zinazohusiana na vitendo vya ukatili wa kijinsia vinavyofanyika miongoni mwa jamii,”

“Tunaamini tutakapowajengea uwezo wana habari na wao kupitia kalamu zao wataweza kuifikisha elimu hii kwa sehemu kubwa ya jamii, watu wengi wataelewa ubaya wa kumfanyia mtu mwingine ukatili wa aina yoyote ile na hivyo kuachana na vitendo hivyo, mpaka sasa kuna mafanikio ambayo yameanza kuonekana kutokana na kazi za waandishi,” alieleza Msoka.

Alisema mafanikio ya TAMWA pia yamechangiwa na mchango mkubwa wanaoupata kutoka kwa makundi mbalimbali ya wanaharakati yanayojishughulisha kupiga vita ukatili wa kijinsia ikiwemo asasi za kiraia kama vile Mtandao wa Jinsia (TGNP), Kituo cha Sheria na haki za binadamu (LHRC), na Chama cha wanasheria wanawake (TAWLA).

Pia TAMWA hushirikiana na mashirika mbalimbali ya kimataifa yanayopigania haki za binadamu na kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia ambapo Shirika la Idadi ya watu la Umoja wa Mataifa (UNFPA) kwa hivi sasa ndilo linalofadhili mafunzo kwa waandishi wa habari juu ya harakati dhidi ya Ukatili wa kijinsia nchini.

Msoka anasema, “….Waandishi wa habari wana wajibu mkubwa wa kuleta mabadiliko ya kijamii kutokana na kazi kubwa waliyonayo katika kujenga na kubadilisha mwelekeo wa watu ambapo wakielimishwa kuhusu masuala ya ukatili wa kijinsia wataihamasisha jamii juu ya aina zote za ukatili huo na hivyo kuondoa mfumo wa ubaguzi wa kijinsia na kuwepo mahusiano mazuri yasiyo ya kikatili.”

Kwa upande wao waandishi hao wa habari waliweza kujadili changamoto mbalimbali zinazowakabili katika mikoa yao ambapo kwa sehemu kubwa changamoto hizo zilikuwa zikifanana ikiwemo tatizo la jamii kwa sehemu kubwa kuogopa kutoa taarifa juu ya vitendo vya ukatili vinavyofanyika katika familia zao kwa kuchelea aibu au kuchekwa na jamii.

Baadhi ya changamoto nyingine zilizobainishwa ni uwezo mdogo wa kifedha kwa ajili ya kusafiria kwenda maeneo ya vijijini ambako vitendo vingi vya ukatili wa kijinsia vimekuwa vikiendelea kutokea na jamii kwa sehemu kubwa ikiwa bado inaendelea kuheshimu mila na desturi zilizopitwa na wakati ambazo kwa sehemu kubwa zinawakandamiza wanawake na watoto.

Kundi la waandishi kutoka mkoani Shinyanga lilitaja pia tatizo la baadhi ya watendaji katika madawati ya jinsi yaliyopo katika vituo vya polisi kukataa kutoa ushirikiano kwa waandishi wa habari kwa visingizio kwamba bado wanafuatilia chanzo cha tukio husika.
 
Changamoto nyingine iliyobainishwa na waandishi kutoka mkoa wa Shinyanga na Kagera na tatizo la kushindwa kujieleza kwa ufasaha kwa waathirika wa vitendo vya ukatili wa kijinsia ikiwemo suala la mawasiliano ya lugha za asili ambazo waandishi hushindwa kuzielewa.  Hata hivyo walishauriwa kutafuta wakalimali pale linapojitokeza tatizo la lugha.

Kwa upande wao wawakilishi wa mkoa wa Kagera pamoja na changamoto nyingi walizoziainisha walisema tatizo la umbali wa maeneo ambako hutokea vitendo vya ukatili linachangia waandishi kushindwa kufika maeneo hayo kutokana na kutokuwa na usafiri ambapo walitoa mfano wa maeneo ya visiwa vilivyomo ndani ya ziwa Victoria.

Hata hivyo waandishi hao walijadili na kupendekeza njia mbalimbali za kukabiliana na changamoto zilizojitokeza ikiwemo suala la kutolewa elimu ya kutosha kwa jamii ili iweze kuachana na tabia ya kuficha au kuwaficha watu wanaotendewa vitendo vya kikatili na badala yake washirikiane na wadau wa kupiga vita vitendo hivyo kwa kuwafichua watuhumiwa wote ili sheria ichukue mkondo wake.

Waandishi hao walikubaliana pamoja na changamoto zinazowakabili kutumia fursa walizonazo kwa kuandika habari na makala mbalimbali zitakazoielimisha jamii iweze kushiriki kikamilifu katika kupiga vita vitendo vya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia katika maeneo yao na hivyo kuweza kupunguza kama siyo kukomesha kabisa vitendo hivyo.
 
Akichangia katika mbinu zilizobainishwa na waandishi ya jinsi ya kukabiliana na changamoto wanazokumbana nazo katika kufuatilia na kuandika habari juu ya ukatili wa kijinsia, mkurugenzi wa TAMWA aliwashauri wajenge utamaduni wa kushirikiana kati ya waandishi wa mkoa mmoja na mkoa mwingine kwa kupeana taarifa juu ya vitendo vilivyotokea ili waweze kushirikiana kufuatilia.
 
Lakini pia alisema pale waandishi wanapopata fursa ya kuhudhuria katika mikutano mbalimbali ya kijamii basi wajenge tabia ya kuomba nafasi ili waweze kutoa ujumbe mfupi juu ya ubaya wa vitendo vya ukatili wa kijinsia na jinsi ya kuvipiga vita ili jamii iliyohudhuria katika mikutano iweze kupata elimu na hivyo kuondoa woga na waweze kuwafichua watuhumiwa wanaojihusisha na vitendo hivyo.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top