BAADHI ya wazazi nchini wametajwa kuwa chanzo cha kuporomoka kwa maadili kwa watoto wao kutokana na kutowalea kimaadili tangu wakiwa watoto wadogo.
Hali hiyo imebainishwa na Sheikh wa mkoa wa Shinyanga, Ismail Habib Makusanya alipokuwa akitoa nasaha zake katika mashindano ya kusoma na kuhifadhi Qur – an yaliyoshirikisha wanafunzi zaidi ya 70 kutoka madrasa za mjini Shinyanga.

Sheikh Makusanya alisema kuporomoka kwa maadili miongoni mwa vijana wengi hapa nchini kunachangiwa kwa kiasi kikubwa na wazazi ama walezi ambao hawana tabia ya kuwalea watoto wao kimaadili tangu wakiwa na umri mdogo.

Alisema iwapo wazazi na walezi wote watajenga utamaduni wa kuwalea watoto wao kimaadili na kuwafundisha dini kwa ufasaha, hali ya kuporomoka kwa maadili kwa vijana wengi hapa nchini itapungua kwa kiasi kikubwa tofauti ilivyo hivi sasa katika maeneo mengi.

Aliendelea kueleza kuwa, kukosekana kwa maadili miongoni mwa vijana ndiyo chanzo cha matukio mengi ya kiuhalifu ikiwemo matumizi ya madawa ya kulevya, vitendo vya unyang’anyi, ukahaba na ushoga vinavyofanywa na vijana wengi wakiamini ndiyo ujana na maisha ya kisasa.

“Ndugu zangu lazima turejee kwenye mafundisho ya mwenyezi mungu na mtume wetu Muhammad (S.A.W) juu ya malezi ya watoto wetu, tuwajengee mazingira mazuri tangu wakiwa na umri mdogo, tuwalee kimaadili ya dini, tukifanya hivyo ni wazi hawataweza kufanya vitendo  vichafu watakapokuwa watu wazima,”

“Hivi sasa serikali inahangaika kupambana na watumiaji na wauzaji wa madawa ya kulevya, ukiangalia wanaofanya mambo haya ni hawahawa watoto wetu wenyewe, tujiulize walijifunzia wapi mambo haya? ni wazi hawakulelewa katika tabia na maadili mema, hivyo hawaoni ubaya wowote kujihusisha na vitendo hivyo,” alieleza.

Sheikh Makusanya alitoa wito kwa wazazi na walezi wote wa kiislamu hapa nchini kumrejea mwenyezi mungu kwa kufanya vitendo vizuri kama mafundisho ya mwenyezi mungu yanavyoelekeza, ambavyo vitawaepusha na mambo machafu pamoja na kuwafundishia watoto wao tabia na maadili mema.

Alifafanua kuwa  iwapo jamii nchini itajengwa katika misingi ya maadili mema hata serikali kwa upande wake haitokuwa na kazi kubwa ya kupambana na wavutaji au wauzaji wa madawa ya kulevya, wahalifu au  makahaba kwa vile hapatakuwa na watu wanaofanya vitendo hivyo.

Kwa upande wake mgeni rasmi katika mashindano hayo, Sheikh Hilal Soud ambaye ni mwenyekiti wa Kamati ya Istiqama mkoani Shinyanga alitoa wito kwa wazazi wa kiislamu kuwapeleka shule watoto wao ili waweze kupata elimu badala ya kuwaficha au kuwapa kazi ndogondogo ambazo hazitowasaidia hapo baadae.

Sheikh Hilal alisema suala la elimu ni muhimu katika ulimwengu wa hivi sasa na kwamba bila elimu hakuna jambo lolote la muhimu ambalo mtu anaweza kulifanya iwe upande wa dini au kidunia na hata mwenyezi mungu amesisitiza sana juu ya umuhimu wa watu kusoma.

“Elimu ndiyo urithi usiofilisika, na kwa sisi waumini wa kiislamu suala la kutafuta elimu ni moja ya mambo yaliyofalidhiwa juu yetu, hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha anawapatia watoto wake elimu zote mbili, ya dunia na ile ya akhera,”

“Tuache tabia ya kuwaficha majumbani au kuwapa vishughuli visivyo kuwa na faida ya baadae kwao, tuwapeleke shule wasome elimu ya dini na ya dunia kwa kadri ya uwezo wao, tuache kuridhika na elimu ya msingi tu, tuwakazanie, vinginevyo watakuwa na maisha magumu hapo baadae,” alieleza Sheikh Hilal.

Katika mashindano hayo mwanafunzi, Abdulaziz Mussa kutoka Madrasatul Farouq ya majengo Shinyanga aliibuka mshindi wa kwanza katika washindani waliohifadhi juzuu tatu ambapo alipewa zawadi ya shilingi 300,000 taslimu, tafsiri ya Qur-an moja na kitabu cha fiqhi.

Washindi waliohifadhi juzuu tatu, ni Said Muhibu kutoka Madrasat Ibaadh aliyepewa shilingi 200,000, Mussa Juma pia kutoka Ibaadh aliyekuwa mshindi wa tatu na kupewa shilingi 100,000 na msahafu mmoja wa tafsiri. Mohamed Mdone, Aisha Aboubakar na Mohamed Omari washindi kwa waliohifadhi juzuu mbili na kupewa shilingi 50,000 kila mmoja.

TUMEKUWEKEA HAPA PICHA ZAIDI ZA SHINDANO LA USOMAJI NA UHIFADHI WA QUR - AN KWA MADRASA ZA MJINI SHINYANGA.








Baadhi ya watoto walioshiriki shindano la Usomaji na Uhifadhi wa Qur - an.
Viongozi na waumini wakifuatilia kwa makini mashindano ya usomani na uhifadhi wa Qur - an









Majaji na waongozaji nao walikuwa katika kuhakikisha haki inatendeka.



Majaji kazini




Mau-staadhi wa Madrasa zilizofanya vizuri pia walitunukiwa zawadi.





Sehemu ya washindi wakipokea zawadi zao kutoka kwa mgeni rasmi, Sheikh Hilal Soud.




Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top