Wanachama wakiimba wimbo wa Solidarty kabla ya kuanza mkutano.

Katiba ya TUGHE
RAIS Dkt. John Magufuli amepongezwa kwa kazi kubwa anayoifanya hivi sasa hapa nchini ikiwemo kuwafukuza kazi wafanyakazi wanaotuhumiwa kughushi vyeti vya shule na waliotumia vyeti vya watu wengine ili kujipatia ajira.

 Pongezi hizo zimetolewa  na wanachama wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE) Tawi la Kituo cha Afya Kambarage manispaa ya Shinyanga katika uzinduzi rasmi wa Tawi la wafanyakazi katika kituo hicho cha afya.

Hata hivyo pamoja na pongezi hizo wafanyakazi hao wamemuomba Rais Dkt. Magufuli aangalie upya uamuzi wake wa kuwafukuza kwa kuruhusu waweze kulipwa mafao yao mbalimbali wanayostahili akizingatia mchango mkubwa walioutoa katika ujenzi wa taifa kipindi walichokuwa wakifanya kazi.




Katibu wa TUGHE mkoa, Tabu mambo akitoa maelekezo na maelezo muhimu kabla ya uchaguzi wa viongozi wa Tawi, kushoto ni Mwenyekiti wa kamati ya wanawake TUGHE Mkoa wa Shinyanga, Frola Magubo.
Wakifafanua wanachama hao walisema pamoja na kosa la wengi wao kutumia vyeti vya kidato cha nne visivyokuwa halali au vilivyoghushiwa, lakini bado waliweza kujiendeleza kitaaluma na kufanya vizuri na hivyo kuweza kufanya kazi zao kwa ufanisi na weledi mkubwa katika kipindi walichokuwa kazini.
 
Waliendelea kufafanua kuwa kati ya waliokumbwa na kashfa ya vyeti vya kidato cha nne ilichangiwa na serikali yenyewe kipindi cha awamu ya nne ilipowataka watumishi wote wa umma kuwa na kiwango cha elimu ya kidato cha nne na kushauriwa kujiendeleza hali iliyosababisha kwa waliokosa muda wa kusoma kununua vyeti mitaani.






Wanachama wa TUGHE, Tawi la Kituo cha Afya Kambarage na viongozi kutoka TUGHE mkoa wakimsikiliza kwa makini katibu wa mkoa, Tabu Mambo akitoa maelezo mbalimbali kuhusu katiba ya TUGHE na Sheria ya Ajira na Mahusiano kazini.

“Tunampongeza Rais wetu Dkt. Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya hivi sasa kuhakikisha utendaji kazi ndani ya serikali yake unakuwa wa ufanisi bila ya ujanja ujanja wa aina yoyote  au udanganyifu wa kitaaluma, hali itakayowezesha kila mfanyakazi kuwa na sifa stahiki anazopaswa kuwa nazo,”

“Hata hivyo tunafikiri ni vizuri Rais sasa atumie ubinadamu aangalie mchango uliotolewa na watumishi hawa wa umma ambao wengi wana zaidi ya miaka 30 kazini wakiwa wamebakiza kipindi kifupi cha kustaafu, hivyo kuwafukuza bila kuwalipa chochote ni kutothamini mchango wao pamoja na mapungufu waliyokuwa nayo,” walieleza.

Aidha walisema pamoja na udanganyifu wa vyeti vya kidato cha nne wengi wakiwemo walimu, wauguzi, madaktari na madereva lakini waliweza kufanya vizuri na kuhitimu mafunzo ya kozi zao walizosomea kwa kutumia vyeti vya kughushi na  hata walipoajiriwa walifanya kazi zao bila matatizo yoyote.

Waliendelea kueleza hata baadhi ya viongozi wa serikali waliopo madarakani hivi sasa wakiwemo waliofanya zoezi la uhakiki vyeti, walifundishwa na kuhitimu vizuri masomo yao vizuri na walimu wanaodaiwa ambao leo hii wamekutwa na kosa la kughushi vyeti.

“Ni kweli ndugu zetu hawa wana makosa, lakini pia kwa upande wa pili serikali iliyowaajiri ilikuwa na makosa yake, maana iliridhika na vyeti walivyowasilisha wakati wa usaili wao, hivyo ni vizuri busara ikatumika katika kuachana nao, iwaonee huruma iwalipe mafao yao wanayostahili kwa kuzingatia kazi walizofanya ndani ya serikali,”

“Pia tunamuomba Rais ahakikishe zoezi hili la uhakiki wa vyeti liwe endelevu ili kuweza kuwabaini wadanganyifu wote ambao bado wamo ndani ya ajira kwenye sekta ya umma bila kujali wapo kundi lipi la ajira, bila kufanya hivyo itakuwa sawa na baba anayebagua watoto ambao wote ni wake,” alieleza Anna Kasala.

Wakati huo huo Tawi hilo la TUGHE limefanya uchaguzi wa viongozi wake wa tawi watakaoongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo ambapo Dkt. Salome Mtani alichaguliwa kuwa mwenyekiti na katibu wa tawi ni Lazaro Joseph huku Marietha Buzwizu akichaguliwa kuwakilisha kundi la vijana.

Wajumbe wa tawi waliochaguliwa ni Yohana Kuzenza, Kanyala Maganga na Grace Gombanila ambapo Bernadetha Mushi alichaguliwa kuwa mwenyekiti kamati ya wanawake tawini na katibu wake ni Prisca Zabron huku Frida Mtungilei akichaguliwa kuwa mwekahazina, wajumbe wake ni Matlida Grey na Anna Kasalla.







Viongozi wapya wa Tawi wakikabidhiwa vitendea kazi, katiba na kanuni ya TUGHE.
Kwa upande wake aliyekuwa msimamizi wa uchaguzi huo, Katibu wa TUGHE mkoa, Tabu Mambo aliyeongozana na mwenyekiti wa mkoa wa kamati ya wanawake na mjumbe wa mkutano mkuu wa Taifa wa TUGHE, Frola Magubo aliwataka wajumbe waliochaguliwa kuhakikisha wanatimiza wajibu wao wa kuwatumikia wanachama kikamilifu.

Mambo alisema moja ya majukumu ya Tawi la wafanyakazi sehemu za kazi, ni kutetea na kulinda ajira, haki za wafanyakazi ikiwa ni pamoja na kujadili masharti ya utumishi kwa wanachama wake na kuhakikisha afya na usalama wa wafanyakazi vinadumishwa sehemu ya kazi.

Pia kuwasilisha mikataba ya hiari katika kamati ya utendaji ya mkoa na kuiarifu kuhusu suala lolote ambalo linaweza kusababisha mgogoro wa kikazi ikiwemo pia kutoa taarifa mara kwa mara kwa wanachama kuhusu shughuli za Tawi kwa ujumla.

“Endapo patatotekea mgogoro wa kikazi mahali pa kazi, Halmashauri ya Tawi itaitisha mkutano wa wanachama wote na kama ni mahali ambapo muafaka na mwajiri umeshindikana, kura ya maoni ya kuhusu uwezekano wa kuitisha mgogoro itapigwa,”

“Uamuzi wa kutangaza mgogoro utahitaji theluthi mbili ya wanachama na utawasilishwa mbele ya mkoa ili utoe kibali baada ya kushauriana na makao makuu ya chama,” alieleza katibu Mambo.

Aliwataka wajumbe waliochaguliwa kuhakikisha wanatetea maslahi ya wafanyakazi katika kudai haki zao ambapo hata hivyo alisisitiza suala la kutimiza wajibu kabla ya kudai haki na kwamba matawi ya chama sehemu ya kazi yanaundwa kwa mujibu wa sheria ya Ajira na Mahusiano kazini ya mwaka 2004.




Katibu wa Tawi, Lazaro Joseph akitoa neno la shukrani baada ya kuchaguliwa ambapo pia alifunga rasmi kikao.
“Kabla ya kudai haki zetu kwanza tuhakikishe wafanyakazi wanatimiza wajibu na malengo ya mwajiri, kisha ndipo tunadai haki, wafanyakazi wanayo haki ya kukutana na kujadili masuala muhimu juu ya mstakabali wa maslahi yenu kazini,” alieleza Mambo.


Wanachama wa Tawi la TUGHE Kituo cha Afya Kambarage wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wapya wa Tawi lao wakiwemo viongozi wa TUGHE mkoa waliosimamia uchaguzi.

Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top