Wakazi wa kata ya Mwakitolyo wakiwa na nyuso za furaha wakimpongeza mbunge wao kutokana na kutekeleza ahadi zake.
WAKAZI wa kata ya Mwakitolyo wilayani Shinyanga wamempongeza mbunge wa Jimbo la Solwa, Ahmed Salum (CCM) kwa jinsi anavyotekeleza ahadi mbalimbali alizoahidi kipindi cha kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 ikiwemo kuwaondolea kero ya miundombinu mibovu ya barabara.
 
Pongezi za wakazi hao zimetolewa mwishoni mwa wiki iliyopita katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kitongoji cha Mahiga ambako mbunge huyo alisikiliza malalamiko ya wachimbaji wadogo wa dhahabu waliopewa siku saba na mkuu wa mkoa, Zainab Telack wawe wameondoka ili kumpisha mwekezaji wa kichina.
 
Wakizungumza katika mkutano huo wakazi hao walielezea kuridhishwa na kazi zinazotekelezwa na mbunge wao hivi sasa na kwamba katika kipindi chake cha ubunge amefanya kazi kubwa katika kuwatatulia kero ya barabar a zilizokuwambovu na kuwezesha zipitike kwa urahisi tofauti na ilivyokuwa miaka ya nyuma.
 
Walisema miaka ya nyuma kata yao ilikuwa ikigeuka kisiwa nyakati za masika kutokana na kutokuwepo kwa barabara imara zinazopitika kwa kipindi cha mwaka mzima hali ambayo hivi sasa imebaki kuwa historia kutokana na kutengenezwa kwa barabara nyingi imara ndani ya kipindi cha miaka 10 iliyopita.
 
Mmoja wa viongozi wa chama katika kata ya Mwakitolyo akitoa salaam kwa niaba ya wananchi.

Mbunge Ahmed (katikati mwenye maiki) akiwahutubia wananchi wa Mwakitolyo.
“Kwa kweli tuna kila sababu ya kukupongeza mheshimiwa mbunge, umetufanyia mambo makubwa sisi watu wa Mwakitolyo, leo hii tunaweza kufanya mawasiliano na maeneo mengine kipindi chote cha mwaka tofauti na ilivyokuwa miaka ya nyuma, wasafiri wanaotaka kwenda jijini Mwanza au wilayani Kahama hawalazimiki tena kupitia Shinyanga mjini tena,”
 
“Pia jimbo letu linaongoza kwa kuwa na magari mengi ya wagonjwa (Ambulance) ikilinganishwa na maeneo mengine mkoani Shinyanga, karibu kila zahanati kuna gari la wagonjwa,  umeme tunaona juhudi zako, maeneo mengi tayari kazi ya upelekaji umeme wa REA inaendelea, lakini pia usambazaji wa maji kutoka Ziwa Victoria unaendelea katika vijiji vingi vya jimbo letu, tunakupongeza,” alieleza Shija Malisha.

Wasanii nao hawakuwa nyuma katika kutumbuiza mkutano wa mbunge.
Hata hivyo kwa upande mwingine wananchi hao walilalamikia tabia ya baadhi ya watendaji wa serikali ikiwemo ofisa mtendaji wa kata (WEO) ya Mwakitolyo kuwabughudhi kwa vitisho mbalimbali ikiwemo kuunga mkono agizo la wao kutakiwa kuondoka katika maeneo yao kwa lengo la kumpisha mwekezaji.
 
“Tunashukuru kwa uamuzi wa kututaka tusiondoke katika maeneo yetu mpaka pale Rais Dkt. John  Magufuli atakapotoa ufafanuzi juu ya kauli yake aliyoitoa hapo awali alipoagiza tusifukuzwe kwenye maeneo yetu, lakini tunaomba kama inawezekana leo hii uondoke na mtendaji wetu wa kata, huyu ni jipu maana ni moja ya kero hapa kwetu,”
 
“Tunasema ni jipu kwa sababu mara nyingi ana tabia ya kumkumbatia mwekezaji  wa kichina, na ukimuona tu amekwenda kwenye ofisi zake, basi akirudi ni kututaka tuondoke hapa, na kweli maana sasa hata mkuu wa mkoa naye ameungana naye na alitoa siku saba tuwe tumeondoka, tunakushukuru kwa kusema tusiondoke,” alieleza Mary Maganga.
 
 
Sehemu ya wachimbaji wadogo wakimpongeza kwa mbali mbunge Ahmed.
 
 
Mbunge Ahmed akiagana na wananchi baada ya mkutano.
Kwa upande wake mbunge Salum alisema ana uhakika mpaka ifikapo mwaka 2020 vijiji vyote katika Jimbo la Solwa vitakuwa vimepata umeme kupitia mradi wa umeme vijijini (REA) na kwamba ni wakati muafaka kwa wakazi wa wilaya hiyo kujiandaa kutumia fursa hiyo kwa kuanzisha miradi midogomidogo ya uzalishaji mali.
 
Alisema kwa mwaka 2017 tayari kazi ya upelekaji umeme katika vijiji  vitatu itakamilika na baada ya vijiji hivyo kazi hiyo itaendelea kufanyika katika vijiji 50 na inatarajiwa ifikapo mwishoni mwa mwaka 2020 vijiji vyote vya Jimbo la Solwa vitakuwa vimepatiwa huduma ya umeme.
 
“Ndugu zangu ninachowaomba kwa upande wenu ungeni mkono juhudi hizi kwa kuanzisha miradi midogo midogo ya uzalishaji mali ili umeme usiwe mapambo bali utumieni kuwaingizia kipato na pia jengeni nyumba bora.  Juu ya suala la maji, ninyi wenyewe ni mashahidi, kazi inaendelea katika maeneo mengi,”
 
“Naamini baada ya kipindi kifupi kijacho kero ya maji kwa watu wa Jimbo la Solwa itakuwa ni historia, lakini pia kuhusu barabara vimebaki vijiji vichache sana ambavyo havijapata barabara za uhakika, nawaahidi pia kero hiyo itamalizika kabla ya mwaka 2020.  Niwaombe wale mlioko kwenye uchimbaji mdogo jiungeni kwenye vikundi mpatiwe hatimiliki,” alieleza.
 
Kwa upande mwingine Salum alimwagiza mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, Mboje Ngassa kushughulikia malalamiko yaliyotolewa na wananchi dhidi ya mtendaji wa kata (WEO) wa Mwakitolyo anayedaiwa kuwabughudhi wananchi ambapo alikemea tabia ya watendaji kuwabughudhi wananchi ambao ndiyo waajiri wao wakuu.
 
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top