Naibu Katibu Mkuu wa CCM (bara), Rodrick Mpogolo  akizungumza na viongozi wa CCM ngazi ya matawi, kata, wilaya na mkoa wa Shinyanga, kushoto ni katibu wa CCM mkoani Shinyanga, Hawla Kachwamba na wa kwanza kulia ni mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro na mwenyekiti wa CCM wilaya ya Shinyanga mjini, Kanali Tajir Maulid.
BAADHI ya wanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoani Shinyanga wamelalamikia maamuzi yaliyotolewa hivi karibuni na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) ya kuwapa onyo kali wana CCM waliotuhumiwa kwa vitendo vya usaliti badala ya kuwafukuza kama ilivyopendekezwa na vikao vya wilaya na mkoa. 
Baadhi ya wanachama ambao ni viongozi wa ngazi za matawi, kata, wilaya na mkoa wa Shinyanga wakimsikiliza Naibu Katibu mkuu wa CCM Bara, Rodrick Mpogolo.



Malalamiko hayo yametolewa mbele ya Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Bara, Rodrick Mpogolo alipokuwa akizungumza na wajumbe wa sekretarieti za CCM ngazi ya matawi, kata, wilaya na mkoa wa Shinyanga akiwa katika ziara ya siku moja mkoani humo.

Akifafanua kuhusu kitendo cha kutofukuzwa kwa baadhi ya wasaliti wa chama, katibu mwenezi wa CCM wilayani Kahama, Masudi Melimeli aliyehoji kitendo cha kutofukuzwa uanachama kwa mwenyekiti wa Umoja wa wanawake wa CCM (UWT) Aoko Nyangusu aliyebainika kwa ushahidi wote kwamba alifanya usaliti kipindi cha uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

“Ndugu Naibu katibu mkuu, tunashukuru kwa maelezo yako mazuri kuhusiana na suala zima la mageuzi yaliyofanyika ndani ya chama chetu,  lakini hata hivyo sisi hapa Shinyanga tumesikitishwa na kitendo cha halmashauri kuu ya Taifa, kushindwa kuwachukulia hatua za kuwafukuza ndani ya chama wanachama waliobainika kutusaliti,

“Kweli chama kimefukuza baadhi ya wasaliti waliothibitika kutusaliti kipindi cha uchaguzi mkuu, lakini inavyoonekana bado mmeacha mizizi yao imebaki ndani ya chama, kule Kahama yupo mwenyekiti wa UWT wilaya, Aoko Nyangusu, huyu vikao vya wilaya na mkoa vilipendekeza afukuzwe uanachama, lakini tumeshangaa kusikia amepewa onyo kali,” alieleza.




Viongozi na makada wa CCM wakifuatilia hotuba ya Naibu Katibu mkuu wa CCM bara.

Alisema kuachwa kwa mwenyekiti huyo kutasababisha wana CCM wengine waendelee kuumia na kuteseka kutokana na vitendo vyake anavyovifanya ambapo pia alisema huko nyuma aliwahi kupewa onyo kali pamoja na aliyekuwa mwenyekiti wa CCM, Khamis Mgeja lakini wameshangaa kuona ameachwa tena.

“Ndugu naibu, ukweli ukitaka kufukuza mwehu basi lazima umfukuze na makopo kopo yake, hivi sasa amepewa karipio kali bado ameendelea kutamba kwamba hakuna mtu atakayemuweza, kwa madai anafanya kazi maalumu, hatujaridhishwa na hali hii japokuwa tunaheshimu maamuzi ya vikao vya juu na sisi tunamwachia mungu,” alieleza Melimeli.

Akijibu malalamiko hayo, Naibu katibu mkuu wa CCM, Mpogolo alisema vikao vya juu havijapuuza maazimio au ushauri uliotolewa na wilaya na mkoa kwani kila ngazi ilipewa mamlaka yake na kwamba maamuzi ya Halmashauri kuu ya Taifa katika kutathimini na kutafakari maamuzi ya mkoa iliona watu hawa wapewe adhabu anayostahili ni kupewa onyo kali.

Hata hivyo alisema maamuzi hayo hayazuii halmashauri kuu ya wilaya ama mkoa kuendelea kufuatilia nyenendo na maadili ya mwanachama huyo na iwapo itabainika anaendelea na vitendo vya usaliti dhidi ya chama basi hatua dhidi yake zichukuliwe.

“Naamini kamati ya siasa ya mkoa, katibu wa chama na kamati yake ya siasa ya wilaya wanao wajibu wa kufuatilia shughuli za kila siku za chama katika wilaya ya Kahama, kama mwanachama huyo aliyepewa adhabu ya onyo kali na anaendelea kukiuka maadili ya chama, lazima adhabu iendelee kuchukuliwa dhidi yake,” alieleza Mpogolo.

Katika hatua nyingine wanachama wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoani Shinyanga wamepongezwa kwa kazi kubwa waliyoifanya kipindi cha uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 iliyowezesha  wagombea wa chama hicho katika ngazi ya udiwani, ubunge na urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuibuka na ushindi mkubwa.

Mpogolo alisema mkoa wa Shinyanga ni miongoni mwa mikoa iliyomchagua kwa kura nyingi mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya CCM, Dkt. John Magufuli ambapo kitaifa ulishika nafasi ya tano kwa mikoa iliyotoa kura nyingi za urais na wa kwanza kwa mikoa ya kanda ya Ziwa.

“Katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 tulishinda kwa sababu wananchi walituamini, tulinadi ilani ya uchaguzi na kuonesha matendo mema ndiyo maana wananchi waliamua kuchagua Chama cha Mapinduzi, kazi hii lazima iendelezwe maana tunapomaliza uchaguzi mmoja hapohapo tunaanza maandalizi ya uchaguzi ujao,”

“Niwakumbushe kwenye mikoa bora, mkoa wa Shinyanga upo katika tano bota, mmefanya kazi kubwa kukiletea chama chetu ushindi, kwa hili niwapongeze wana Shinyanga, maana kwenye uchaguzi mkuu uliopita 2015 tulishinda kwa kiwango kikubwa kwa nafasi za udiwani, ubunge na urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alieleza Mpogolo.

Kwa upande mwingine Mpogolo aliwaomba wanachama wa CCM wakubali kuyapokea mabadiliko yaliyofanyika hivi karibuni ndani ya chama chao na kwamba mabadiliko hayo yamelenga kukiimarisha chama na kukiwezesha kuwa kipya kama lengo la serikali ya awamu ya tano ya kuifanya Tanzania kuwa mpya.

Alisema halmashauri kuu ya Taifa (NEC) iliyofanyika mwezi Desemba mwaka jana ilipitisha mabadiliko na mageuzi ndani ya Chama cha Mapinduzi kwa lengo la kukiimarisha katika ngazi ya mashina na matawi na kukifanya kiendelee kukubalika na watanzania wengi.

“Jambo kubwa lililonileta hapa kwenu na kuhimiza suala la uimarishaji chama chetu ngazi ya mashina na matawi, na hii lazima tuelewe ili uweze kuimarisha mashina na matawi lazima kwanza uanze kufanya mageuzi kwa mwanachama mmoja mmoja,”

“Chama chetu hakiwezi kuwa na nguvu kama hakitoi taswira nzuri kwa watu wanaoongozwa, kwa hiyo mageuzi yanayozungumzwa yanakwenda kuwagusa wana CCM wenyewe, msingi mkubwa ni wana CCM wenyewe kukubali kubadilika,” alieleza Mpogolo.

Akifafanua alisema wana CCM mmoja mmoja wakiweza kufanya mageuzi ni wazi CCM itaimarika na kuwa na nguvu kubwa na itaendelea kutawala nchi hii kwa kipindi kirefu kwa vile hakuna mtu atakayeweza kukiondoa madarakani.

Hata hivyo aliwakemea wana CCM ambao bado wana mawazo mawazo ya ki-UKAWA na kuwataka wasahau UKAWA kwa vile hivi sasa umeishasambaratishwa na hauna nguvu zozote na hivi sasa wafuasi wake wamejawa na hasira kutokana na kutopata ushindi.

“Raha ya CCM ni ushindi, na ninyi viongozi wa Shinyanga mnajua mlikuwa na wenzenu kule nyuma, wakaamua kwenda kule kwingine, je, leo hii wana furaha? hawana, na hawana la kufanya, hii ni kwa vile uamuzi wao haukuwa wa busara,”

“Nawapongezeni wana CCM wa Shinyanga, CCM itaendelea kuwa imara na hakuna mtu wa kuiondoa madarakani, CCM ina historia na mizizi yake na wapo wazee walioianzisha na hivi sasa wametukabidhi sisi, tunaendelea nayo, tunasonga mbele hakuna wa kurudi nyuma, kama bado kuna mwenye mawazo hayo, afanye mageuzi aambatane na CCM,” alieleza.

Hata hivyo naibu katibu mkuu huyo aliwaomba wana CCM kusimama imara na kufanya kazi ya kukijenga chama chao bila ya baadhi yao kutegeana na kwamba iwapo watafanya hivyo ipo hatari ya chama hicho kutetereka na kuwaomba kila mmoja atimize wajibu wake katika eneo lake.

Pia alitoa wito kwa watendaji wote wa ngazi ya wilaya na mkoa kuachana na utamaduni wa kukaa maofisini na badala yake watoke wawafuate wanachama matawini ambako watakuwa na fursa nzuri ya kukiimarisha chama sambamba na uimarishaji wa mashina ambako ndiko kwenye wanachama.

Wajumbe wa kamati ya siasa ya mkoa wakimsikiliza kwa makani Naibu katibu mkuu wa CCM bara.

Kwa upande wao baadhi ya wanachama hao walionesha hofu yao kutokana na mabadiliko yaliyofanyika ikiwemo kufuta baadhi ya nafasi muhimu ikiwemo ile ya makatibu wasaidizi na wale wa Uchumi, mipango na fedha na kwamba hatua hiyo inaweza kusababisha mdodoro wa kiuchumi ndani ya chama.

"Binafsi sipingani na mabadiliko yaliyofanyika, lakini hofu yangu ni iwapo hayataathiri hali ya uchumi ndani ya chama chetu, hasa pale ilipoamriwa kuondolewa kwa nafasi za makatibu wa uchumi na fedha ngazi ya mikoa na wilaya na makatibu wasaidizi, naamini hatua hii inaweza ikatuathiri kimapato," alieleza Hassan Mwendapole.




Wanachama wa CCM wakitoa maoni na ushauri wao mbele ya Naibu katibu mkuu wa CCM Bara, Rodrick Mpogolo

Akijibu hoja hiyo, Mpogolo alisema mabadiliko yanayolengwa ikiwemo kupunguza baadhi ya nafasi za kiuongozi yanakusudia kuimarisha zaidi ngazi ya matawi na mashina na kwamba hakuna sababu za wana CCM kuwa na hofu juu ya mabadiliko hayo kwa vile yamefanyika kwa umakini mkubwa.

End.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top