Baadhi ya watoto wa shule ya msingi Shingida wilayani Shinyanga wakijiandaa kurejea nyumbani baada ya kukamilisha masomo yao ya siku

WITO umetolewa kwa wakazi wa mkoa wa Shinyanga kujitolea kwa hali na mali kusaidia ujenzi wa vyumba maalumu kwenye shule za msingi na sekondari vitakavyotumika kwa ajili ya kujihifadhi watoto wa kike wanaoingia kwenye hedhi.


Ukosefu wa vyumba hivyo umetajwa kuwa moja ya changamoto inayowakabili watoto wengi wa kike katika shule za msingi na sekondari hali inayochangia wapoteze vipindi vingi vya masomo kila mwaka kutokana na kushindwa kuhudhuria masomo.

Wito huo umetolewa na mkurungenzi wa Shirika la Agape Aids Control Programme mkoani Shinyanga, John Myola kwenye kikao cha uzinduzi wa mradi wa utoaji elimu ya afya ya uzazi na haki ya mtoto utakaotekelezwa katika kata ya Usanda wilayani Shinyanga chini ya ufadhili wa Shirika la Save the Children.


Mkurugenzi wa Shirika la Agape, John Myola (aliyesimama) akitoa ufafanuzi juu ya utekelezaji wa mradi wa Elimu ya Afya ya uzazi na haki ya mtoto kwa viongozi na wazazi wa kata ya Usanda, kulia ni diwani wa kata ya Usanda.

Mkurugenzi wa Shirika la Agape, John Myola akitoa taarifa ya uzinduzi wa utekelezaji wa Mradi wa Elimu ya afya ya uzazi na haki ya mtoto kwa viongozi wa serikali na wawakilishi wa wazazi na walezi katika kata ya Usanda wilayani Shinyanga.
Akichangia hoja iliyowasilishwa na washiriki waliohudhuria uzinduzi wa mradi huo, Myola alisema imefika wakati jamii yenyewe ikabiliane na changamoto ya ukosefu wa vyumba hivyo na ijitolee kuvijenga kwa ushirikiano na serikali ili kuwanusuru watoto wa kike badala ya kusubiri misaada ya wafadhili au serikali kuu.

Akizungumzia changamoto hiyo, Myola alisema jamii inapaswa kubadilika kwa kuanza kuchukua hatua za kukabiliana na changamoto ambazo wana uwezo wa kukabiliana nazo mfano wa ujenzi wa vyumba hivyo ambavyo gharama zake siyo kubwa.

Kutokana na hali hiyo yeye binafsi aliahidi kuchangia bati 10 kwa shule yoyote katika kata ya Usanda itakayokuwa ya kwanza kuanzisha ujenzi wa chumba maalumu ambapo pia alisema atajitolea kutoa kilo 40 za unga na dagaa kwa watu watakaojitolea kujenga na yeye mwenyewe atashiriki kwenye ujenzi huo.

“Ukosefu wa vyumba hivi unawaathiri watoto wetu sisi wenyewe, hivyo tusibweteke kusubiri wengine kutuondolea tatizo hili, lazima tuamue, wenyewe tuanze sasa, kata ya Usanda ioneshe mfano kwamba jamii ikiamua inaweza, vyumba hivi havihitaji gharama kubwa, mbali ya watoto kujihifadhi pia vitatumika kutolea huduma ya kwanza kwa watakaopatwa tatizo lolote,”

“Mimi binafsi naahidi kuchangia bati 10 kwa watakaokuwa wa kwanza kuanzisha ujenzi, na nitatoa kilo 40 za unga na dagaa kwa ajili ya chakula cha watakaojitolea kujenga chumba hicho, ndugu zangu tutumie njia ya nguvu kazi, tusaidiane na serikali yetu ili kuwaondolea watoto wetu ukosefu wa eneo la kujihifadhi,” alieleza Myola.

Kwa upande wake mmoja wa washiriki wa kikao hicho, Kennedy Malesa alisema ukosefu wa vyumba maalumu kwa ajili ya kujihifadhi watoto wa kike ni changamoto iliyopo katika shule nyingi za msingi na sekondari maeneo mengi nchini hali inayosababisha washindwe kwenda shule wanapokuwa katika hedhi.

Awali wakichangia mada juu ya uendeshaji wa mradi wa elimu ya afya ya uzazi na haki ya mtoto, washiriki wa kikao hicho walisema iwapo elimu hiyo itawekewa mkazo itapunguza kwa kiasi kikubwa matukio ya mimba za utotoni ikiwemo maambukizi ya virusi vya UKIMWI.

“Tunawashukuru wenzetu wa Agape na Save the Children kwa kutuletea mradi huu, tunaani ukitekelezwa kikamilifu utapunguza tatizo la watoto wa kike kubeba mimba wakiwa na umri mdogo, wengi wanabebeshwa mimba kutokana na kutojitambua juu ya makuzi yao na wengine kuambukizwa virusi vya UKIMWI na magonjwa ya zinaa,”

Ofisa Mradi kutoka Shirika la Save the Children CIS, John Maliyapambe akitoa maelezo kuhusiana na mradi wa utoaji elimu ya afya ya uzazi na haki ya mtoto katika kata ya Usanda wilaya ya Shinyanga.
“Lakini ni vizuri elimu hii ikawafikia pia wazazi ili iwasaidie kubadilika, wapo baadhi yao hushindwa kusikiliza ushauri wa wazazi wenzao  wanaposhauriwa kuhusiana tabia mbaya za watoto wao wanaojiingiza katika nyendo zisizofaa ikiwemo kujihusisha na mambo ya mapenzi wakiwa na umri mdogo,” alieleza Chande Musa katibu wa msikiti wa Usanda.




Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top