Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Maji, Kilimo na Mifugo, Mary Nagu (wa tatu kutoka kushoto) akiwaongoza wajumbe wengine wa kamati yake kukagua tangi la maji linalojengwa wilayani Kishapu mkoani Shinyanga kwa ajili ya kusambaza maji katika mji wa Mhunze na vijiji jirani lenye uwezo wa kuhifadhi meta za ujazo 1,200 kwa wakati mmoja.

Kaimu mkurugenzi wa KASHWASA, Laurence Wasala akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi wa upelekaji maji wilayani Kishapu mkoani Shinyanga mbele ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji, Kilimo na Mifugo.


Mwenyekiti wa kamati, Mary Nagu akiongozana na wajumbe wake kukagua eneo la mradi wa ujenzi wa tangi la maji katika mji wa Mhunze, kushoto ni kaimu mkurugenzi wa KASHWASA, Lawrance Wasala.
MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa mazingira Kahama Shinyanga (KASHWASA) imepongezwa kwa kazi kubwa wanayoifanya kuhakikisha huduma ya maji kutoka mradi wa Ziwa Victoria inasambazwa na kuwafikia wananchi wengi mkoani Shinyanga na mkoa jirani wa Tabora. 


Pongezi hizo zimetolewa juzi na wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Maji, Kilimo na Mifugo iliyokuwa katika ziara ya siku mbili mkoani Shinyanga kutembelea na kukagua utekelezwaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo miradi ya maji inayotekelezwa na KASHWASA.

Wakizungumza katika kikao cha majumuisho baada ya kutembelea miradi ya maji inayotekelezwa na KASHWASA, wabunge hao walielezea kuridhishwa na kazi nzuri inayofanyika ya usambazaji wa maji katika wilaya za Shinyanga na Kishapu hali ambayo imewezesha wananchi wengi kupata maji kwa urahisi.

Wabunge hao walisema kazi inayofanywa na KASHWASA inaonesha jinsi gani serikali ya awamu ya tano inavyotekeleza kwa vitendo ahadi ilizozitoa kwa wananchi kuhusiana na suala zima la kuwaondolea kero ya maji iliyokuwa ikiwakabili katika maeneo yao.

Akitoa pongezi hizo kwa niaba ya wajumbe wake, mwenyekiti wa Kamati, Mary Nagu alisema kamati yake imeridhishwa na kazi zinazotekelezwa na KASHWASA ambazo zitawezesha wananchi wengi hivi sasa kupata huduma ya maji ya uhakika tofauti na ilivyokuwa siku za nyuma.

“Kwa kweli mimi na wenzangu tumeridhishwa na kazi nzuri inayofanywa na wenzetu wa KASHWASA, ni wazi wanatekeleza kikamilifu maelekezo ya serikali, na sisi wabunge hatuna budi pia kuipongeza serikali kwa jinsi inavyotekelezwa kwa vitendo suala la usambazaji wa maji kwa wananchi wetu hasa walioko maeneo ya vijijini,”

“Mradi huu wa maji kutoka Ziwa victoria ni mradi uliobuniwa miaka mingi iliyopita, awali ulikumbana na vikwazo vingi serikali ilipotaka kuutekeleza, nakumbuka tangu mimi nikiwa waziri wa HESAWA iliyokuwa ikishughulikia uchimbaji wa visima vifupi, tulipendekeza kujengwa kwa mradi huu, hatimaye umekamilika na unafanya kazi,” alieleza Nagu.

Awali akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi wa upanuzi wa mtandao wa usafirishaji maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika mji wa Kishapu kupitia mji mdogo wa Maganzo na mgodi wa Almasi wa Mwadui, Kaimu mkurugenzi wa KASHWASA, Mhandisi Laurence Wasala alisema mradi huo unakadiriwa kugharimu shilingi  bilioni 14.46.

“Kutokana na hali ya upatikanaji wa fedha kutoka serikalini na makubaliano kati ya KASHWASA na mgodi wa Almasi wa Mwadui, mradi ulipangwa kutekelezwa katika awamu mbili, awamu ya kwanza ilihusu ujenzi wa bomba kutoka Old Shinyanga hadi mgodi wa Almasi Mwadui,”

“Hii ilifanyika kutokana na makubaliano ya kisheria yaliyofikiwa kati ya KASHWASA na uongozi wa mgodi wa Almasi wa Mwadui, awamu hii ilipangwa kukamilika ndani ya muda wa miezi mitano tangu kuanza kwa utekelezaji, mradi mzima unakadiriwa kugharimu kiasi cha shilingi 14.46 bilioni, sawa na dola za kimarekani 6.62 milioni,” alieleza Wasala.

Mbali ya mradi wa usambazaji maji wilayani Kishapu pia KASHWASA itapeleka maji katika manispaa ya Tabora na miji midogo ya Igunga, Nzega, Kagongwa, Isaka na Tinde ambapo mradi huo umepangwa kuanza kutekelezwa mwezi Mei, 2017.

Baadhi ya miradi iliyotembelewa na kamati hiyo ya bunge ni pamoja na kuangalia ujenzi wa tangi kubwa linalojengwa katika mji wa Kishapu litakalokuwa na meta za ujazo 1,200 ambapo kazi hiyo imekamilika kwa asilimia 70 mpaka hivi sasa.

Mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya bunge, Mary Nagu akiteremka kutoka juu ya tangi linalojengwa wilayani Kishapu kwa ajili ya kusambaza maji katika mji wa Mhunze na vijiji vya jirani.


Wajumbe wa kamati ya bunge ya kudumu wakisikiliza maelezo kuhusiana na mradi wa usambazaji maji katika kijiji cha Bunambiyu wilayani Kishapu.

 
Mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack (mwenye ushungu) akibadilishana mawazo na viongozi wenzake baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa tangi la maji linalojengwa na KASHWASA wilayani Kishapu mkoani Shinyanga, wengine ni katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga, Anselim Tarimo (mwenye shati jeupe), Mwenyekiti wa Kamati, Mary Nagu na Laurence Wasala.


Mwenyekiti kamati ya kudumu ya bunge, Maji, Kilimo na Mifugo, Mary Nagu akipata maelezo ya mradi wa maji katika kijiji cha Bunambiyu wilayani Kishapu, katikati mwenye suti nyeusi ni Naibu waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Ole Nasha
Pia wajumbe walitembelea kuangalia en.eo ambalo mtandao wa bomba kutoka chanzo cha maji katika kijiji cha Ihelele wilayani Misungwi mkoani Mwanza kinapounganishwa kupeleka maji katika mji wa Shinyanga na wilaya ya Kishapu ambapo pia walitembelea mradi wa maji katika kijiji cha Bunambiyu wilayani Kishapu.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top