Meneja Mkuu wa mgodi wa Bulyanhulu wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga, Graham Crew (kushoto) akimkabidhi katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela (katikati) mfano wa hundi yenye thamani ya shilingi milioni 760.5 ikiwa ni malipo ya ada ya ushuru wa huduma kwa Halmashauri ya Msalala wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga kulia mwenye shati la kitenge ni mbunge wa Jimbo la Msalala, Ezekiel Maige. 

 
Meneja Mkuu wa Mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga, Graham Crew (kushoto) akimkabidhi mkuu wa mkoa wa Geita, Meja Jenerali mstaafu, Ezekiel Kyunga, mfano wa hundi yenye thamani ya shilingi 374,608,900 kwa ajili ya Halmashauri ya wilaya ya Nyang'hwale mkoani Geita ikiwa ni ada ya ushuru wa huduma kwa kipindi cha miezi sita (July - Dec. 2016) Kulia anayeshuhudia ni katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela.
MBUNGE wa Jimbo la Msalala wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga, Ezekiel Maige ameupongeza uongozi wa Mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu kwa kuilipa Halmashauri ya Msalala ada ya ushuru wa huduma kwa mujibu wa sheria.


Maige ametoa pongezi hizo katika hafla fupi ya makabidhiano ya hundi yenye thamani ya shilingi milioni 760 kwa halmashauri ya Msalala na shilingi milioni 374 kwa halmashauri ya wilaya ya Nyang’hwale mkoani Geita.

Akikabidhi hundi hizo, Meneja Mkuu wa mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu unaomilikiwa na kampuni ya Acacia, Graham Crew alisema malipo hayo ni moja ya utekelezaji wa sheria inayowataka wawekezaji kulipa ada ya ushuru wa huduma kwa halmashauri utakaosaidia kusukuma maendeleo ya jamii.

Akifafanua Crew alisema hadi kufikia mwishoni mwa mwaka 2016, mgodi huo umelipa kiasi cha shilingi bilioni 4.8 tangu mwaka 2014 kampuni ya Acacia ilipoanza kutoa malipo ya ushuru wa huduma wa asilimia 0.3 ya mapato ghafi kwa halmashauri ya husika.

“Fedha hii tunayoikabidhi leo hii ni malipo ya awamu ya pili ya ada ya ushuru wa huduma ambayo tumeanza kulipa tangu mwaka 2014, ni utekelezaji wa sheria inayotutaka kulipia ushuru wa huduma asilimia 0.3 ya mapato yetu ghafi tunayopata katika halmashauri husika,”

“Mpaka hivi sasa tumeisha lipa ushuru huu kiasi cha shilingi bilioni 4.8 kwa halmashauri ya Msalala mkoani Shinyanga na Nyang’hwale kwa mkoa wa Geita, kwa awamu hii ya pili kwa mwaka 2016, tumelipa shilingi milioni 760 kwa halmashauri ya Msalala na shilingi bilioni 374 kwa Nyang’hwale,” alieleza Crew.

Sehemu ya mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu.
Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Msalala, Ezekiel Maige pamoja na kupongeza kitendo cha mgodi huo kulipa ushuru stahiki kwa mujibu wa sheria, aliuomba uongozi wa mgodi kuwabana wakandarasi wadogo wanaopewa kazi na mgodi ili na wao waweze kulipa ada hiyo ya ushuru wa huduma.

Maige alisema pamoja na mgodi wa Bulyanhulu kutekeleza sheria, bado makampuni mengi ya ukandarasi yanayopewa kazi mbalimbali mgodini hayazilipi halmashauri husika ushuru huo na kwamba viongozi wa halmashauri hawana uwezo wa kuyabaini makampuni hayo bali kwa msaada wa uongozi wa mgodi.

“Pamoja na kuwapongezeni kwa utekelezaji wa sheria hii, lakini bado tuna safari ndefu, wananchi wetu bado wana kiu kubwa ya kuona jinsi gani wananufaika na raslimali zilizopo katika maeneo yao, hivyo tunaomba tusaidiane kuyabana makampuni mnayoyapa kazi ili na yenyewe yatulipe ushuru huu,” alieleza Maige.

Naye meneja mkuu wa mahusiano kati ya kampuni na serikali, Asa Mwaipopo alisema malipo yaliyolipwa na mgodi wa Bulyanhulu ni moja wa wajibu wake katika kutekeleza sheria zilizopo nchini kuhusiana na masuala ya uwekezaji.

Mwaipopo alisema pamekuwepo na mafanikio mazuri katika utekelezaji wa shughuli za uzalishaji wa mgodi hali iliyochangiwa na mahusiano mazuri yaliyopo kati ya uongozi wa mgodi, serikali na jamii yenyewe.

“Sisi tunaamini iwapo hali hii ya mahusiano mazuri itaendelea, ni wazi tutaongeza uzalishaji zaidi na hivyo kuwezesha kupatikana kwa fedha nyingi kwa upande huu wa ada ya ushuru wa huduma tunaolipa kila mwaka, tunaomba ushirikiano uliopo uendelezwe kwa pande zote husika,” alieleza Mwaipopo.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top