Mwenyekiti wa Shirika la Tanzania Mzalendo Foundation, Khamis Mgeja

Huyu ni mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Zainabu Telack akiwa katika moja ya mikutano na wananchi.

WAKUU wa mikoa na wilaya ambao maeneo yao yamekumbwa na upungufu mkubwa wa chakula wametakiwa kujitoa kafara kwa kuieleza serikali ukweli ili kuwanusuru wananchi wasife kwa njaa badala ya kuogopa kutumbuliwa katika madaraka waliyonayo.


Wito huo umetolewa na mwenyekiti wa asasi ya kiraia ya Tanzania Mzalendo Foundation, Khamis Mgeja alipokuwa akitoa salaam zake za mwaka mpya akiwa mkoani Tabora kwenye mapumziko mafupi.

Mgeja alisema maeneo mengi nchini hivi sasa yanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula kutokana na mvua kutokunyesha za kutosha na hivyo wananchi kuhitaji kupatiwa msaada wa chakula cha bei nafuu kutoka serikalini.

Hata hivyo alisema kutokana na kauli za mara kwa mara zinazotolewa na Rais Dkt. John Magufuli zikidai serikali haiwezi kutoa chakula kwa wananchi wake na kuwataka walime ambapo aliwaonya wakuu wa wilaya na mikoa wasimpelekee maombi ya chakula vinginevyo atawatumbua.

Alisema kauli hizo za rais zimesababisha baadhi ya wakuu wa mikoa na wilaya kukaa kimya wakiogopa kutoa taarifa ya mikoa au wilaya zao kukumbwa na baa la njaa kwa hofu ya kutumbuliwa hali inayochangia wananchi wengi kukosa chakula na kushindia uji au kula matunda.

“Naomba nitoe wito kwa viongozi wetu katika ngazi za mkoa na wilaya, wasiogope kutoa taarifa ya hali njaa katika maeneo yao, lazima watumie ujasiri wamweleze kiongozi wao hali halisi hata kama ataamua kuwatumbua,”

“Lazima waelewe suala la uongozi siyo jambo la kudumu, waelewe pia yapo maisha nje ya ukuu wa mkoa au wilaya, hivyo wakubali kuwa kafara na kujitoa sadaka kwa wananchi wanaowaongoza kwa kueleza ukweli, vinginevyo watu watakufa kwa njaa,” alieleza Mgeja.

Aliendelea kueleza kuwa hakuna aibu yoyote wala siyo kosa kwa kiongozi wa wananchi kueleza ukweli bali lipo tatizo miongoni mwa viongozi wa serikali kukumbwa na gonjwa la hofu na woga ambao unaweza kusababisha madhara kwa wananchi.

Alisema ni lazima wakuu wa mikoa na wa wilaya watambue vyeo walivyonavyo ni dhamana na hakuna mtu aliyezaliwa na cheo bali watambue kuwa uongozi ni matokeo tu yanayomkuta mwanadamu katika mchakato wa maisha yake.

“Mimi naamini iwapo viongozi wetu watakubali kueleza ukweli wa hali halisi ya chakula katika maeneo yao, itasaidia serikali kujipanga vizuri, na kwa upande mwingine tunaiomba serikali hii iwe sikivu katika suala zima la njaa, viongozi wetu wawape wananchi wake maneno yenye matumaini badala ya kuwakatisha tamaa,”

“Inashangaza kusikia kiongozi mkuu wa nchi anawaeleza wananchi wake eti,  ‘....serikali haina shamba wala chakula cha bure,’ au maneno ya ‘mwafaaa’ ukweli kauli za namna hii hazileti tija wala afya kwa watu anaowaongoza, lazima serikali iwajali wananchi walioiweka madarakani siyo kuwabeza,” alieleza Mgeja.


Baadhi ya maeneo ambayo yamekumbwa naukame wa kutisha.

Alisema anaiomba na kuishauri serikali kulipa kipaumbele suala uhaba wa chakula uliojitokeza katika maeneo mengi nchini kutokana na hali ya hewa ilivyobadilika na kusababisha uhaba mkubwa wa mvua na sasa mazao yameanza kunyauka kutokana na ukame.

Mgeja aliyewahi kuwa mwenyekiti wa CCM mkoani Shinyanga kabla ya kujiunga na CHADEMA ameishauri na kuiomba serikali ya awamu ya tano iweke wazi kiasi cha akiba ya chakula kilichopo hivi sasa katika hifadhi yake ili wananchi waweze kufahamu hali halisi ilivyo.

“Serikali inaposhindwa kusema ukweli eti kwa sababu ya
kiusalama wa kitaifa sasa tunajiuliza je chakula nacho kimekuwa zana
za ‘Kivita’?, mimi naamini iwapo serikali itakuwa wazi kuhusiana na akiba ya chakula wananchi watapata fursa ya kujipanga vizuri kwa kujifunga
mkanda,” alieleza.

Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top