Ofisa Maendeleo ya Jamii mkoani Shinyanga, Lydia Kwesigabo akiwasilisha mada kwa washiriki juu ya Sheria ya mtoto ya mwaka 2009

Washiriki wa warsha wakifuatilia kwa makini mada zinazowasilishwa, wa kwanza mwenye miwani ni katibu wa TAS mkoani Shinyanga, Lazaro Anaeli.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Ntuli Kapologwe (katikati) akifuatilia jambo katika warsha iliyofanyika kujadili changamoto mbalimbali zinazowakumba watu wenye Ualbino, wazazi na walezi wao.  Kushoto ni Ofisa habari kutoka TAS makao makuu, Dar es Salaam, Josephat Tonner na kulia ni mmoja wa washiriki kutoka nchini Uganda, Edith Nabalanga.

CHAMA cha Watu wenye Ualbino (TAS) mkoani Shinyanga kimeiomba serikali kutekeleza agizo lake lililotolewa mwaka 2012 likielekeza watu wenye ulemavu kupatiwa bure huduma za matibabu katika zahanati, vituo vya afya na hospitali za serikali.


Ombi hilo limetolewa na washiriki wa warsha ya siku moja iliyoandaliwa kwa ajili ya kubadilishana mawazo kati ya watu wenye ualbino, wazazi na walezi wao juu ya changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo sambamba na kuelimishana juu ya haki wanazostahili kupatiwa.

Mmoja wa washiriki wa warsha hiyo kutoka wilayani Kishapu, Joseph Masanja alihoji kitendo cha baadhi ya watoa huduma katika zahanati na hospitali za serikali kuwataka walemavu kuchangia huduma za matibabu wakati kuna waraka wa serikali unaoagiza watibiwe bure.

Masanja alisema walemavu wengi hawana uwezo hivyo wanashindwa kuchangia huduma na mara nyingi baadhi yao huondoka vituoni bila ya kupatiwa matibabu kutokana na kutokuwa na fedha.

Mbali ya matibabu pia walielezea masikitiko yao ya kukatiliwa kuajiriwa katika maeneo mengi kinyume na maelekezo yaliyotolewa na serikali ikielekeza eneo lolote la kazi asilimia tatu ya wafanyakazi wake wawe ni watu wenye walemavu hata hivyo waajiri hawatekelezi agizo hilo hata kama walemavu wanakidhi vigezo vya kazi iliyotangazwa.

Kwa upande wake Ofisa Mipango kutoka TAS makao makuu, Severin Edward alikiri kuwepo kwa agizo la walemavu kutibiwa bure lililotolewa kwa waraka wenye Kumb. Na. AB.24/280/01 wa Julai 13, 2012 na kusainiwa na aliyekuwa katibu mkuu wa TAMISEMI wakati huo, H. A. Kattanga.

Washiriki wakiwa makini katika kufuatilia mada zinazowasilishwa.

“Waraka huo ulisambazwa kwa makatibu tawala wote wa mikoa nchini ukiwa na kichwa cha habari; Kusimamia masuala mbalimbali yanayohusiana na watu wenye ulemavu ambapo waliagiza kuhakikisha walemavu wanapokwenda kutibiwa katika hospitali, vituo vya afya na zahanati zilizopo chini ya serikali hawatozwi huduma za matibabu,” alieleza Edward.

Aliendelea kufafanua kuwa mbali ya waraka huo wa serikali pia Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizosaini mkataba wa kimataifa wa Haki za watu wenye ulemavu (UNCRPD) na hata sheria namba tisa ya mwaka 2010 ya watu wenye ulemavu na Sera ya afya ya Taifa vinaelekeza walemavu kutibiwa bure.

Washiriki wa warsha hiyo iliyohudhuriwa pia na mshiriki mwenye ualbino kutoka nchini Uganda, Edith Nabalanga wameiomba serikali ihakikishe itoe msimamo wake ili kuwezesha sera na sheria mbalimbali zinazotungwa hapa nchini zinatekelezwa na kuondoa kupishana kwa matamko yanayotolewa.

Maofisa wa polisi kutoka kitengo cha dawati la jinsi walikuwa ni miongoni mwa washiriki wa warsha hiyo.



Ofisa Habari kutoka TAS Makao Makuu, Josephat Tonner akisisitiza jambo kwa washiriki.
Hata hivyo kwa upande wake Ofisa Habari kutoka TAS Makao Makuu, Josephat Tonner aliwahadharisha washiriki hao kuhusiana na suala la kutegemea kusaidiwa katika kila jambo hata kwa mambo  wanayoyaweza na kuwataka waache tabia ya kujinyanyapaa wao wenyewe na badala yake washirikiane na jamii katika masuala ya kimaendeleo.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top