Mmoja wa wahanga wa viboko vya walinzi wa Jadi (Sungusungu), John Kitumbo mkazi wa kijiji cha Welezo kata ya Nsalala wilayani Shinyanga akionesha majeraha aliyoyapata baada ya kucharazwa viboko.

Mkazi wa kijiji cha Welezo ambaye alijeruhiwa kwa kipingo cha sungusungu.
KATIKA hali isiyotarajiwa wakazi kadhaa wa kijiji cha Welezo kata ya Nsalala wilayani Shinyanga wamejeruhiwa sehemu mbalimbali za miili yao huku wengine wakipoteza fahamu baada kushambuliwa kwa vipigo vya fimbo na kundi la walinzi wa jadi sungusungu zaidi ya 800.
 
Tukio hilo lisilokuwa la kawaida limetokea Desemba 10, mwaka huu saa 4.00 asubuhi huko katika kijiji cha Welezo kata ya Nsalala wilayani Shinyanga baada ya kutokea vurugu zilizosababisha mapigano kati ya wanakijiji na walinzi wa jadi kutoka vijiji jirani vinavyozunguka kijiji hicho.
Kufuatia tukio hilo wanakijiji wa wamemkataa mwenyekiti wao wa serikali ya kijiji Salumu Shabani mbele ya mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro anayetuhumiwa kula njama za kuwaalika sungusungu hao waliowadhalilisha kwa kuwacharaza viboko huku wakipewa adhabu za kupiga pushapu bila kujali wanawake wenye ujauzito.

Kamanda wa sungusungu wilaya ya Shinyanga vijijini, Kulwa Masanja akijieleza mbele ya mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro baada ya kutuhumiwa kuondoka na fedha za wanakijiji shilingi 200,000 zilizotolewa na mkazi wa Welezo aliyetuhumiwa kujihusisha na vitendo vya uhalifu.
Wakizungumza katika mkutano wa hadhara ulioitishwa na mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro, wanakiji hao walidai chanzo cha wao kuadhibiwa na kujeruhiwa baada ya kucharazwa viboko huku wengine wakipoteza fahamu kuwashinikiza viongozi wao kuwasomea taarifa ya mapato na matumizi ya kijiji.
Pia walisema viongozi wao wa sungusungu kijijini hapo walishindwa kutekeleza agizo la mkutano mkuu wa kijiji ulioagiza wanakijiji wagawane mpunga ambao hukusanywa kutoka kwa watu wanaolipishwa adhabu ya “mchenya” baada ya kufanya makosa madogo madogo kijijini.
Wakifafanua walisema hivi karibuni walifanya mkutano mkuu wa kijiji ambapo moja ya maazimio yaliyotolewa ni viongozi wa serikali ya kijiji na walinzi wa jadi kuandaa taarifa ya mapato na matumizi ikiwemo kupanga utaratibu wa jinsi wanakijiji watakavyogawiwa mpunga uliokwisha kusanywa zaidi ya magunia 150.

Wananchi wakitoa malalamiko yao mbele ya mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro baada ya kucharazwa viboko na sungusungu.

 

Kaimu mwenyekiti wa Serikali ya kijiji, Janeth Kulobone aliyechaguliwa baada ya kuenguliwa kwa mwenyekiti wa zamani Salumu Shabani.



Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Welezo, Salumu Shabani ambaye amekataliwa na wananchi wake.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro.
Hata hivyo siku iliyopangwa viongozi hao hawakuweza kujitokeza katika mkutano uliokuwa umeitishwa na badala yake waliendesha vikao vya ndani wakishirikiana na viongozi wa walinzi wa jadi (sungusungu) kitu ambacho wanakijiji hawakukiafiki na hivyo kuchukua hatua ya kuukataa uongozi mzima wa sungsungu.
“Baada ya kubaini viongozi wetu wanatuzungusha na hawataki kutekeleza maazimio ya mkutano mkuu, wanakijiji waliamua kuwavua madaraka viongozi wa sungusungu, hali ambayo wenzetu hawakuiafiki, na hivyo walikula njama na viongozi wa sungusungu ngazi ya kata na tarafa ili kutukomoa,”
“Tulipowavua madaraka viongozi wa sungusungu, Sungusungu ngazi ya kata na tarafa walipitisha azimio la kijiji chetu kutengwa, tulitengwa na baada ya muda tukaombwa tuchangie shilingi 5,000 kila kaya ili  tuondolewe adhabu tuliyopewa, kiasi cha shilingi milioni moja na laki tatu kilikusanywa, tulinunua ng’ombe sita na mbuzi kadhaa kwa ajili ya kazi hiyo,” alieleza John Kitumbo.
Kitumbo aliendelea kufafanua kuwa baada ya kukamilisha mahitaji yote kwa ajili ya shughuli za kutawadhwa upya kuwa sungusungu, mkutano uliitishwa na viongozi wa jadi kutoka ngazi ya kata, tarafa na wilaya ndiyo waliohusika kusimamia kazi hiyo kwa lengo la kijiji chao kuondolewa adhabu ya kutengwa.
Hata hivyo siku ya kufanyika kwa shughuli iliyokuwa imekusudiwa, walishangaa kuona viongozi wao wakiibuka na agenda tofauti na iliyokuwa imepangwa kufanyika ambapo kikao hicho kiligeuka cha kuwataja watu wahalifu, wizi na wakata mapanga vikongwe.
“Ajabu siku ya mkutano rasmi tulishangaa kugeuziwa kibao, tukiwa tunajiandaa kutawadhwa upya, ghafla kamanda wa sungusungu wa wilaya, Kulwa Masanja alianza kuita majina ya watu na kuwataka wajitokeze mbele ya mkutano ambapo walielezwa wao ni wahalifu na wanatakiwa kujikomboa kwa shilingi 200,000 kila mmoja,”
“Suala la kutaja majina ya wahalifu haikuwa agenda yetu siku hiyo, baadhi ya watu waliotuhumiwa na kutajwa waliitwa mbele kisha walichapwa viboko na kutakiwa kuondoka mkutanoni  vinginevyo walipe shilingi 200,000 ili wajikomboke, mmoja alilipa lakini mtu wa nne aligoma, akapigwa fimbo, aligoma na kumkwida shati mpigaji, hapo ndipo vurugu zilipoanzia,” alieleza Janeth Kulubone.
Kutokana na hali hiyo mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Josephine Matiro alitoa agizo la kusimamishwa uongozi mwenyekiti wa Serikali ya  kijiji cha Welezo, Salumu Shabani na kuagiza kufanyika uchunguzi dhidi ya tuhuma zote anazotuhumiwa na kuivunja kamati nzima ya sungusungu ya kijiji ambapo wanakijiji walichagua kamati mpya.
“Nimesikiliza maelezo yenu kwa kina, nimebaini chanzo cha vurugu hizi ni viongozi wenu kukiuka maadili ya uongozi, sasa na mimi naunga mkono azimio lenu la kumkataa mwenyekiti wa serikali ya kijiji, asimame na uchunguzi wa tuhuma zake ufanyike, na hapahapa chagueni mwenyekiti wa muda, na kamati mpya ya sungusungu,” alieleza Matiro.
Mkuu huyo aliongeza kueleza, “.....Wananchi wamenyanyaswa, wameumizwa kwa sababu ya viongozi wa sungusungu na serikali ya kijiji,  sasa tunawaondoa wote,  hii nchi ni ya amani,  haiwezekani watu wachache waharibu amani yetu, sungusungu kazi yenu siyo kunyanyasa wananchi hii iwe mara ya mwisho, eleweni sehemu yoyote yenye vurugu hapawezi kuwa na maendeleo.”
Aidha Matiro amekemea vikali tabia ya baadhi ya viongozi wa serikali za vijiji kufuja mali za wananchi na pale wanapotakiwa kusoma taarifa ya mapato na matumizi hushindwa kufanya hivyo wakiogopa kuumbuliwa na kueleza kuanzia sasa ofisi yake itafuatilia viongozi wote wasiopenda kutekeleza taratibu za kazi na kuwachukulia hatua.

 





Askari wa Jeshi la Polisi akigawa karatasi kwa ajili ya kupiga kura za siri kufichua watu wanaojihusisha na vitendo vya uhalifu.
Katika hatua nyingine wanakijiji hao waliamua kupiga kura za siri ili kuwataja watu wanaotuhumiwa kwa vitendo vya uhalifu mbalimbali ikiwemo mauaji ya vikongwe na kumuomba mkuu wa wilaya kutoyatambua majina ya awali yaliyokuwa yameandaliwa na viongozi wa sungusungu wakishirikiana na mwenyekiti wa serikali ya kijiji.


Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Welezo, Salumu Shabani akiondoka eneo la mkutano baada ya kukataliwa na wanakijiji.

Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top