Mjumbe wa Timu ya kampeni za kuwanadi wagombea wa CCM, Zuhura Waziri (wa pili kutoka kulia) akiwa pamoja na mgombea udiwani katika kata ya Ndala Manispaa ya Shinyanga, Abel Kaholwe (mwenye T-Shirt Nyeusi) na mwenyekiti wa CCM kata ya Ndala, Boniface Tungu wakiwa katika mkutano wa kampeni kata ya Ndala.
Mwenyekiti wa CCM kata ya Ndala akimnadi mgombea udiwani wa CCM kata ya Ndala, Abel Kaholwe katika mkutano wa kampeni kwa wakazi wa kata ya Ndama Manispaa ya Shinyanga.

Hata mimi Push - Up nazimudu eti, tazama hapa!!! ndivyo anavyoelekea kueleza mgombea udiwani kwa tiketi ya CCM katika kata ya Ndala Shinyanga.
WAKAZI wa kata ya Ndala Manispaa ya Shinyanga wameombwa Oktoba 25, mwaka huu wahakikishe wanatumia vizuri kura zao kwa kumchagua diwani mwenye uwezo atakayeshughulikia kero zao badala ya kumchagua mtu anayetaka sifa na maslahi binafsi.

Ushauri huo umetolewa na mmoja wa wajumbe wa timu ya kampeni za kuwanadi wagombea wa CCM katika jimbo la Shinyanga mjini, Zuhura Waziri katika mkutano wa kampeni za kuwanadi wagombea wa chama hicho uliofanyika kwenye viwanja vya kanisa la Angilakana kata ya Ndala mjini humo.

Waziri alisema suala la maendeleo katika eneo lolote lile linahitaji mtu muadilifu na mchapa kazi kama alivyo mgombea wa CCM, Abel Kaholwe ambaye mbali ya kuwa kijana lakini pia anao uzoefu wa kutosha wa kushughulikia matatizo ya wananchi.

“Ndugu zangu wakazi wa kata ya Ndala, tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu Oktoba 25, mwaka huu, ni vizuri tukazitumia vizuri kura zetu kwa kumchagua mgombea wetu wa CCM, ni kijana na mchapa kazi, msirudie makosa ya mwaka 2010 kwa kuchagua diwani kutoka upinzani,”

“Ninyi wenyewe ni mashahidi kutokana na kudorora kwa maendeleo katika kata yenu, yapo mambo mengi yameshindikana kutekelezwa kutokana na udhaifu wa diwani mliyekuwa mmemchagua, kwa hali hiyo tunawaomba msirudie tena kosa la kulamba sumu, litawacheleweshea maendeleo,” alieleza Waziri.

Kwa upande wake mgombea udiwani kwa tiketi ya CCM katika kata hiyo ya Ndala, Abel Kaholwe aliwaomba wakazi wa kata hiyo wampe kura za kishindi ili aweze kuwa diwani wao na apate fursa ya kushughulikia kero nyingi zilizopo katika kata hiyo.

“Tunaingia katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu wakazi wa kata ya Ndala tukiwa na agenda tatu muhimu, ipo kero ya kupandishwa ovyo kwa kodi za majengo, ukosefu wa huduma za afya na ubovu wa miundombinu ya barabara na kutokupimwa kwa viwanja vya makazi,

“Yote haya katika kipindi cha nyuma yalishindwa kutekelezwa kutokana na udhaifu wa diwani tuliyekuwa naye, huyu kipindi kirefu alishughulikia matatizo yake badala ya wananchi, nakuombeni tusirudie kosa, nipeni kura zenu niweze kuwatumikia,” alieleza Kaholwe.

Kwa upande wake mmoja wa wagombea wa udiwani viti maalumu, Mariamu Nyangaka aliwataka wakazi wa kata hiyo kuhakikisha wanatunza shahada zao za kupigia kura na wasikubali kurubuniwa na watu wanaopita pita mitaani wakitaka kuzinunua na kwamba kura zao zina thamani zaidi ya fedha watakazopewa.



Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top