Hizi ndizo fomu rasmi za kuomba kugombea ubunge wa Jimbo la Solwa kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM).
 
Mshandete hapa anajaza kitabu cha wageni
 
 
Mgombea ubunge Jimbo la Solwa wilayani Shinyanga, Amos Mshandete akipokea rasmi fomu zake kutoka kwa katibu wa CCM wilaya ya Shinyanga vijijini, Margareth Cosmas.
WANACHAMA wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wenye nia ya kugombea nafasi za udiwani na ubunge katika uchaguzi mkuu ujao wameshauriwa kutowekeana vinyongo wala uadui kwa vile kila mmoja ana haki ya kuchagua au kuchaguliwa kuwa kiongozi ili mradi ametimiza sifa zinazotakiwa.
Ushauri huo umetolewa juzi na aliyekuwa mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga na diwani wa kata ya Ilola kwa tiketi ya CCM, Amos Malugu Mshandete alipokuwa akichukua rasmi fomu kwa ajili ya kugombea ubunge katika jimbo la Solwa wilayani humo.
 
Mshandete alisema mara kwa mara kinapofika kipindi cha uchaguzi mkuu baadhi ya wanachama wa CCM huwekeana uadui usio na sababu baada ya baadhi yao kujitokeza kuomba kugombea nafasi za udiwani ama ubunge katika maeneo yao hali inayochangia makundi na kuanza kuchafuana.
 
Pokea rasmi fomu hizi, ukazijaze kwa usahihi na kuzirejesha ifikapo Julai 19, mwaka huu saa 10 kamili jioni.
Katibu wa CCM wilaya ya Shinyanga vijijini, Margareth Cosmas akitoa maelezo muhimu kwa mgombea Mshandete yatakayomuwezesha kujaza fomu zake kwa usahihi.
 
Akifafanua Mshandete alisema kwa kawaida ndani ya CCM wanachama huwa hawapingani bali ni kujipanga kuangalia ni mwana CCM yupi anayeweza kuipeperusha vyema bendera ya CCM katika nafasi ya udiwani, ubunge na urais na hiyo ni haki ya kila mwanachama.
 
“Ni vizuri wana CCM katika kipindi hiki cha mchakato wa kura za maoni tukadumisha umoja na mshikamano wetu kwa kila mmoja kujiona ana haki sawa na mwenzake katika kugombea nafasi yoyote ya uongozi anayoihitaji na kazi ya kuamua nani awe mgombea rasmi waachiwe wanachama wenyewe,”
 
“Binafsi baada ya kukaa na kutafakari kazi zangu nilizozitekeleza kwa upande huu wa udiwani kwenye kata yangu na halmashauri nzima ya Shinyanga nikiwa mwenyekiti wa halmashauri, nimeona wazi sasa ni wakati muafaka wa kujikita katika nafasi ya ubunge ili niweze kuwatumika zaidi wananchi wangu,” alieleza Mshandete.
 
Alisema hatua yake ya kuamua kugombea ubunge katika jimbo la Solwa imetokana na kuombwa na wapiga kura wa jimbo hilo kwa kipindi kirefu na wao ndiyo wanaoelewa sababu za kumuomba agombee hivyo ameona akubali ombi hilo na  iwapo atachaguliwa ni wazi hatawaangusha.
 
Aliendelea kueleza katika kipindi chake cha miaka 10 akiwa diwani wa kata ya Ilola na miaka mitano ya uenyekiti wa halmashauri ya wilaya kwa kiasi kikubwa amejitahidi kutekeleza kikamilifu ahadi zote alizozitoa kwa wapiga kura wake kama ilivyoainishwa ndani ya ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.
 
Mpambe wa mgombea Mshandete akikabidhi ada ya kuchukulia fomu kiasi cha shilingi 100,000.
“Katika miaka 10 ya udiwani wangu naamini nimefanya mambo mengi katika sekta za elimu, afya, maji, miundombinu ya barabara ambapo kwa upande wa maji hivi karibuni kata yangu itaanza kupata huduma ya maji kutoka Ziwa Victoria, na shule zote tatu za msingi tumekamilisha ujenzi wa  nyumba za walimu siyo chini ya nne,”
 
“Kwa upande wa afya nimekamilisha ujenzi wa zahanati mbili na hivi sasa tupo katika kukamilisha ujenzi wa Kituo cha afya, naamini nikipata fursa ya kuwa mbunge nitafanya mengi, muhimu wana CCM tuhakikishe uchaguzi hautugawi, kazi ya nani atachaguliwa tuwaachie waajiri wetu ambao ni wananchi,” alieleza.

Wanachama wengine wa CCM waliokuwa wamejitokeza kuchukua fomu za kugombea ubunge katika jimbo hilo la Solwa mbali ya Mshandete ni pamoja na mbunge anayemaliza muda wake, Ahmed Salumu, Kafile Paulo, Renatus Chokala na Mhandisi Luhumbi Kaswende.
 
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top