Moja ya eneo la uchekejaji wa dhahabu katika mgodi mdogo wa Mwabomba - Kahama.
Maofisa kutoka Rafiki SDO wakiwa katika maandalizi ya kuwasafirisha watoto 50 kutoka mgodi wa Mwabomba.
Mmoja wa watoto wanaotumikishwa katika migodi midogo ya dhahabu wilayani Kahama.
Mkurugenzi mtendaji wa Shirika la Rafiki SDO, Gerald Ng'ong'a akitoa hotuba kwa wageni waalikwa kwenye hafla fupi ya kuwaaga watoto 50 wanaopelekwa katika vyuo vya ufundi wilayani Nzega mkoani Tabora.

Sehemu ya watoto walioibuliwa kutoka kwenye ajira za migodini - Mwabomba Kahama.
Mratibu wa mradi kutoka Shirika la Terre des Hommes Samson Kube akitoa nasaha zake kwa watoto.

SHERIA ya mtoto ya mwaka 2009 inaeleza wazi kati ya mambo yanayokatazwa kutendewa watoto chini ya umri wa miaka 18 ni kuajiriwa katika kazi ngumu au zile zinazotajwa kama ajira hatarishi kwa mtoto.


Hata hivyo katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 toleo la 2005 Sehemu ya pili katika Ibara ya 11 vifungu vidogo vya (2) na (3) vinaeleza, nanukuu, (2) Kila mtu anayo haki ya kujielimisha, na kila raia atakuwa huru kutafuta elimu katika fani anayopenda hadi kufikia upeo wowote kulingana na stahili na uwezo wake,”

(3) Serikali itafanya jitihada kuhakikisha kwamba watu wote wanapata fursa sawa na za kutosha kuwawezesha kupata elimu na mafunzo ya ufundi katika ngazi zote za shule na vyuo vinginevyo vya mafunzo,” mwisho wa kunukuu.

Kwa mujibu wa vifungu hivyo vya katiba ni wazi kwamba mtu ye yote anayemzuia mtoto kupata elimu kwa kadri ya uwezo wake anakuwa amevunja katiba ya nchi na ukipatikana ushahidi wa kutosha juu ya kitendo hicho anastahili kuchukuliwa hatua za kisheria.

Pamoja na katiba kueleza na kufafanua wazi kuhusu haki ya kupata elimu kwa kila mtu ikiwemo watoto lakini hapa nchini watoto wengi wamebainika kunyimwa haki hiyo kutokana na hali ya kimaisha ndani ya baadhi ya familia inayosababisha watoto kugeuzwa vitega uchumi na watafutaji wa kipato ndani ya familia.

Maeneo ambayo yamekithiri kwa ukiukwaji wa haki za watoto ni pamoja na yaliyoko kandokando ya migodi midogo midogo na mikubwa hususani ile ya dhahabu na Tanzanite, maeneo ya wavuvi, uchimbaji wa kokoto na mchanga, mashamba ya tumbaku na kwenye shughuli za uchomaji wa mkaa.

Pamoja na kwamba ndani ya sheria ya mtoto ya mwaka 2009 vifungu vya 77 na 86 kuruhusu watoto wenye umri wa kuanzia miaka 14 kufanya kazi nyepesi na kupata malipo stahiki lakini hata hivyo ieleweke kazi zinazoruhusiwa ni zile zisizoathiri afya mtoto husika.

Hata hivyo kifungu cha 78 cha sheria hiyo ya mtoto kinazuia mtu ye yote kumwajiri mtoto katika kazi ye yote ile ya kinyonyaji au ya hatari kwa maisha yake ambapo katika sehemu ya pili kifungu cha 12 kinazuia watoto kuajiriwa katika kazi zitakazosababisha waathirike kiakili, kielimu, kiafya au kuathiri maendeleo yao ya kiroho.

Katika kuangalia uhalisia utabaini bado katika maeneo mengi hapa nchini haki za watoto wengi zimekuwa zikikiukwa bila ya kuwepo mtu au mamlaka yo yote inayokemea hali hiyo na hivyo mtu akitembelea katika miji mingi mikuu hatokosa kukutana na makundi ya watoto wanaoishi katika mazingira magumu.

Kutokana na hali hiyo baadhi ya mashirika na asasi mbalimbali za kiraia zinazojishughulisha na utetezi wa haki za mtoto hapa nchini hivi sasa yanaendesha harakati mbalimbali za kuwasaidia watoto walioko katika makundi hatarishi kwa lengo la kuwasaidia ili waweze kupata elimu itakayowasaidia katika maisha yao ya baadae.

Mashirika na asasi hizo yanaendesha miradi mbalimbali yenye lengo la kuwanusuru watoto walioko katika hatari ya kujiingiza katika makundi hatarishi kwa wale wa kiume na kwa upande wa watoto wa kike kuwaepusha na mimba na ndoa za utotoni vitendo ambavyo katika siku za hivi karibuni vimekithiri katika mkoa wa Shinyanga.

Shirika la kimataifa la nchini Uholanzi liitwalo, Terre des Hommes (TdH) jina lenye maana ya Dunia ya wenye huruma hivi sasa linafadhili miradi miwili mikubwa mkoani Shinyanga inayolenga kuwasaidia watoto mmoja ukiwa ni ule wa kutokomeza ajira za watoto migodini.

Mradi huu wa mwaka mmoja hivi sasa unatekelezwa wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga katika halmashauri mbili za Msalala na Ushetu kwenye kata nne ambazo ni kata ya Isaka, Chela, Lunguya na Idahina katika vijiji vitano vilivyopo katika kata hizo kupitia mashirika manne ya kiraia yaliyopo katika wilaya hiyo.

Moja ya mashirika hayo ni Shirika la Rafiki Social Organization Development (Rafiki SDO) ambalo tayari limeanza kutekeleza mradi huo wa Tokomeza ajira za watoto migodini katika maeneo ya Kata ya Mwabomba kuanzia Julai, 2014.

Akizungumzia utekelezaji wa mradi huo mkurugenzi mtendaji wa shirika la Rafiki SDO, Gerald Ng’ong’a anasema moja ya kazi kubwa inayotekelezwa na shirika lake ni kufanya utafiti na kuwatambua watoto wanaofanya kazi katika migodi hiyo na kuwarudisha shule kulingana na umri wao.

Ng’ong’a anasema, “….Mradi wa tokomeza ajira za watoto migodini ni mradi unaotekelezwa na shirika letu kwa ushirikiano wa mashirika mengine yaliyopo wilayani Kahama ambayo ni SHIREMA, SHIHABI na HUHESO wote tukifadhiliwa na Shirika la kutoka nchini uholanzi la Terre des Hommes,”

“Mbali ya lengo la kuwatambua watoto walioko katika maeneo ya migodi midogo, lakini kubwa zaidi ni kuhakikisha tunatokomeza utumikishwaji wa watoto walio chini ya umri wa miaka 18 kwenye migodi hiyo iliyopo wilayani Kahama.”

Mkurugenzi huyo anasema shirika hilo linatekeleza mradi huo kwa kuzingatia malengo mahususi ya uanzishwaji wake ambapo mbali ya kupiga vita ajira mbaya kwa watoto lakini pia linajishughulisha na utetezi wa haki za watoto na vijana mkoani Shinyanga.

Anasema hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Desemba, 2014 tayari shirika lake lilikuwa limewatambua watoto 4,200 walioko katika maeneo ya migodi wilayani Kahama ambao miongoni mwao watoto 800 ilibainika wanafanya kazi katika migodi hiyo huku wakiwa ni wanafunzi katika shule za msingi.

“Lengo la mradi huu ilikuwa tuutekeleza ndani ya kipindi cha mwaka mmoja tu, lakini baada ya kufanyika kwa utafiti wa kina tumebaini ukubwa wa tatizo, kuna watoto wengi wameacha shule na kukimbilia migodini, na hii inatokana na hali ngumu ya maisha miongoni mwa familia zinazoishi kandokando ya migodi hiyo,”

“Kwa hali hiyo tayari tumeanza mazungumzo na mfadhili wetu Shirika la Terre des Hommes ili kuangalia uwezekano wa kuongeza muda wa utekelezaji wa mradi huu ili angalao sasa ufanyike kwa kipindi cha miaka mitano tuweze kuwaibua na kuwaondoa katika ajira hatarishi watoto wote walioko migodini,” anaeleza Ng’ong’a.

Anasema lengo la hivi sasa ni kuwasaidia watoto 800 waliokwisha ibuliwa katika migodi midogo ya Nhumbi, Nyangalata, Mwabomba na Nyamtengela ambao baadhi wanaobainika kutoroka shule wanarudishwa ili waendelee na masomo yao na wengine wanapelekwa katika vyuo vya ufundi kufundishwa ufundi wa fani mbalimbali.

“Mpaka hivi sasa tumeishafanikisha kupeleka watoto 150 katika vyuo vya ufundi vya Malampaka FDC wilayani Maswa mkoa wa Simiyu, Mwananla FDC na Nzega FDC wilayani Nzega mkoa wa Tabora, na hivi karibuni tutapeleka watoto wengine 100 katika vyuo hivyo,”

“Lakini pia mradi unashughulika na kazi ya kuwajengea uwezo wazazi wa watoto wote wanaotolewa katika ajira mbaya ambao kwa sehemu kubwa walikuwa wakitegemea kipato kutoka kwa watoto hao, tunawafundisha elimu ya ujasiriamali na kuwaanzishia vikundi vidogo vya uzalishaji mali,” anaeleza Ng’ong’a.

Anasema lengo la kuwasaidia wazazi hao ni kuwawezesha waweze kujitegemea badala ya kuwa tegemezi kwa watoto wao na kwamba wasipojengewa uwezo kuna hatari hata pale watoto waliondolewa katika ajira mbaya watakapomaliza mafunzo yao wakajikuta wanajerea walikotoka na hivyo kazi yote iliyofanyika kupoteza maana.

“Lakini pia mradi huu umejikita katika kutoa elimu kwa kamati za ulinzi wa watoto na viongozi wa serikali za vijiji juu ya jinsi ya kuwashawishi watoto kuachana na kazi za migodini pamoja na kuandaa mpango wa utekelezaji wa mradi mzima,” anaeleza.

Hata hivyo mkurugenzi huyo anasema pamoja na juhudi zinazotekelezwa na asasi mbalimbali za kiraia katika kuwasaidia watoto hao bado halmashauri za wilaya kwa upande wake zinawajibika kuanza kujipanga kuangalia jinsi gani zitaweza kuwasaidia mara baada ya kumaliza mafunzo yao vyuoni.

“Ni muhimu hivi sasa halmashauri zote ambako watoto hawa wameokolewa zianze mpango mahsusi wa kutenga bajeti itakayowezesha kuwasaidia pale watakapohitimu mafunzo yao kwa kuwapatia mitaji midogo itakayowawezesha waweze kujiajiri wenyewe badala ya kuendelea kuwa tegemezi,”

“Lakini pia kuna umuhimu wa halmashauri hizi kujitungia sheria ndogo katika maeneo yake ya vijijini zitakazowabana wamiliki wa migodi watakaokutwa wakiendelea kuajiri watoto wadogo kinyume cha sheria ya mtoto na kutoa elimu kwa serikali za vijiji juu ya umuhimu wa kumlinda mtoto bila kutegemea watu wa nje,” anaeleza Ng’ong’a.
 
Kwa upande wake mratibu wa mradi huo kutoka Shirika la Terre des Hommes (TdH), Samson Kube anasema kwa sasa shirika lake linatekeleza mradi huo kwa ushirikiano wa asasi nne za kiraia zilizopo wilayani Kahama katika mkoa wa Shinyanga na kwamba lengo kuu ni kupunguza tatizo la ajira mbaya kwa watoto chini ya umri wa miaka 18.


“Mradi huu umepangwa kutekelezwa ndani ya kipindi cha mwaka mmoja, lakini hata hivyo kwa hali ilivyo tumebaini tatizo ni kubwa, tunafanya mawasiliano ili kuangalia uwezekano wa kuongeza muda badala ya mwaka mmoja iwe ni miaka mitano, maana tumebaini kuna kundi kubwa la watoto chini ya umri wa miaka 18 waliozagaa katika migodi iliyopo Kahama," anaeleza Kube.


Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top