Mbunge wa viti maalumu (CHADEMA) mkoani Shinyanga, Rachel Mashishanga (mwenye Truck suit) akikabidhi kombe kwa kapteni wa timu ya Kolandoto Kombaini manispaa ya Shinyanga Juma Tunze baada ya kuibuka na ushindi katika fainali ya Ligi ya Mashishanga Cup iliyofanyika juzi mjini Shinyanga kwa kuifunga timu ya Veterani ya mjini humo kwa magoli 4 - 1, kushoto mwenye T-shirt nyeupe ni mwenyekiti wa SHIDIFA, Salum Kitumbo.
 
TIMU ya kombaini ya mpira wa miguu kutoka kata ya Kolandoto manispaa ya Shinyanga imeibuka kidedea katika mashindano ya kugombea kombe la Mashishanga baada ya kuwachapa wapinzani wao timu ya Veterani ya mjini Shinyanga kwa mabao 4 – 1.


Kufuatia ushindi huo timu hiyo ilikabidhiwa rasmi kombe la ubingwa huo lenye thamani ya shilingi laki nne, fedha taslimu shilingi 500,000 na mipira mitatu ambapo mshindi wa pili, Veterani walikabidhiwa fedha taslimu shilingi 300,000, seti ya jezi na mipira miwili huku mshindi wa tatu timu ya kata ya Ngokolo walipata shilingi laki mbili na mipira miwili.

Kwa upande wa mchezo wa mpira wa pete wanawake, timu ya Polisi Shinyanga iliyojinyakulia kombe na fedha taslimu shilingi laki tatu ambapo mshindi wa pili timu ya walimu manispaa alipata shilingi laki mbili na mipira miwili huku timu ya ShyCom ikiibuka na ushindi wa tatu iliyojinyakulia shilingi laki moja na mipira miwili.

Akikabidhi zawadi kwa washindi wa mashindano hayo yaliyozishirikisha timu 17 za mpira wa miguu kutoka kata zote za manispaa ya Shinyanga na sita za mpira wa pete  mgeni rasmi, Askofu Edson Mwombeki alimpongeza mwandaaji wake mbunge wa viti maalum kwa tiketi ya CHADEMA, Rachel Mashishanga kwa uamuzi wa kukuza michezo jimboni.

Mwombeki alisema kupitia michezo hiyo mbali ya kuibua vipaji vya vijana lakini pia imeweza kuongeza mshikamano miongoni mwao bila kujali itikadi ya vyama vyao vya siasa na kwamba michezo hiyo itawasaidia vijana hao kujitangaza na kuweza kujiunga na timu kubwa ambapo hivi sasa michezo ni sehemu ya ajira.

Naye mbunge Mashishanga alisema lengo la kuandaa mashindano hayo maarufu kwa jina la Mashishanga Cup ni kutaka kuwaweka pamoja vijana wa jimbo la Shinyanga na kujijenga kiafya na pia kukuza vipaji vyao katika michezo hiyo pamoja na kuwapa sehemu ya kupata burudani wakazi wa Shinyanga.

“Ndugu zangu mbali ya kutoa shukrani zangu za dhati kwa ushiriki wenu katika mashindano haya lakini niwaeleze lengo lake kubwa ni kujenga mahusiano mazuri miongoni mwetu bila kujali itikadi za vyama vyetu vya siasa, na huu ni mwanzo tu, lakini hivi karibuni natarajia kuendesha mashindano mengi kwa upande wa mbio za baiskeli,” alieleza Mashishanga.

Hata hivyo mbunge huyo aliishauri serikali iangalie uwezekano wa kuwatengea fungu maalumu wabunge wa viti maalumu ili liweze kuwasaidia katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimaendeleo katika majimbo wanayoyaongoza ikiwemo michezo kama inavyofanyika kwa wabunge wa majimbo.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top