Baadhi ya wanafunzi wakikamatwa na askari polisi
Mji wa Katoro jana ulizizima kwa mabomu ya machozi wakati polisi walipokuwa wakiwatawanya wanafunzi na wananchi waliofunga barabara kuu ya Geita Bukoba  waliokuwa wakiishinikiza Serikali kuwawekea matuta ili kuepukana na ajali.


Tafrani hiyo ilikuja baada ya mwanafunzi Mussa Joseph (9), wa darasa la nne, Shule ya Msingi Ludete, kugongwa na kufa wakati akivuka barabara katika eneo la stendi mpya Katoro.

Sinema nzima ilianza saa mbili asubuhi baada ya ajali hiyo ambapo wakazi wa eneo hilo wakishirikiana na wanafunzi wa Shule za Msingi Ludete na Mkapa kufunga barabara  kwa mawe huku wakiwa wameshika silaha mbalimbali.

Kwa mujibu wa Diwani wa Kata ya Katoro, Gervas Daudi, akizungumza eneo la tukio alidai kuwa mwanafunzi huyo aligongwa na pikipiki hiyo majira ya saa tano asubuhi wakati akivuka barabara akitoka shuleni hapo.

Alisema mwanafunzi huyo ambaye amezikwa jana nyumbani kwao Katoro alifariki dunia papohapo kutokana na pikipiki hiyo kuwa kwenye mwendo kasi na dereva wake hakuweza kusimama kuhofia  kupigwa na wananchi.

Mkuu wa Wilaya ya Geita, Manzie Mangochie, alifika eneo la tukio na kuamuru uongozi wa halmashauri ya wilaya, walimu waliohamasisha vurugu hizo wachukuliwe hatua za kinidhamu na kwamba walimu wakuu wa shule hizo washushwe vyeo.

 Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Joseph  Konyo alithibitisha tukio hilo ingawa hakutaka kuzungumzia kwa undani kwa kuwa mkuu wa wilaya alikwishalizungumzia.

Mwenyekiti wa Kitongoji cha Kalifonia, Elias Muembeni alisema  wanafunzi hao wamechukua hatua ya kufunga barabara  baada ya kuwapo kwa ajali za mara kwa mara katika eneo hilo.

“Hadi sasa zaidi ya watu watano wamekwishapoteza maisha kwa kugongwa na magari pamoja na pikipiki katika eneo hili,” alisema Muembeni.

Aliongeza:  “Badala  ya kutumia  busara, waliamua kulala barabarani wakiwa tayari kwa lolote na kudai wasingetoka hadi matuta  yawekwe ndiyo maana foleni ya magari imekuwa kubwa kama unavyoiona.’

Chanzo cha Habari: Gazeti la Mwananchi.

Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top