Mwenyekiti TCCIA mkoani Shinyanga, Dickson Musula akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake (hawapo pichani).
 
Hizi ni baadhi ya stakabadhi zinazotolewa na wakala wa vipimo baada ya kufanya ukaguzi wa mizani ya mfanyabiashara.  Juu ni fedha zilizolipwa fundi mizani kwa ajili ya matengenezo, na chini ni stakabadhi ya serikali kwa ajili ya ukaguzi,     
Moja ya viwanda vilivyoathiriwa na ubabe wa maofisa vipimo mkoani Shinyanga, inadaiwa walibeba mikono mitatu ya kwenye mizani na hivyo kusababisha kiwanda kushindwa kufanya kazi.
 
Mmoja wa watumishi wa kiwanda cha Gladi Oil & Food Co. Ltd. akitumia mzani mdogo kwa shida baada ya mizani ya kawaida kubebwa na maofisa vipimo.
CHAMA Cha Wafanyabiashara, Viwanda na Kilimo (TCCIA) mkoani Shinyanga kimetoa ufafanuzi kuhusiana na taarifa iliyotolewa hivi karibuni na Wakala wa vipimo mkoani humo ikidaiwa kuwepo kwa wafanyabiashara wanaoharibu kwa makusudi mizani zao kwa lengo la kuwapunja wateja.
 
Akitoa tamko rasmi mbele ya waandishi wa habari, mwenyekiti wa TCCIA mkoani Shinyanga, Dickson Musula alisema mgogoro uliopo kati ya wafanyabiashara na maofisa vipimo mkoani humo unachangiwa kwa kiasi kikubwa na tabia ya maofisa hao kutoza gharama kubwa za ukaguzi wa mizani kinyume na maelekezo ya sheria.
 
Alisema TCCIA mkoani humo mara kwa mara imekuwa ikiwaelimisha wafanyabiashara ambao ni wanachama wake juu ya umuhimu wa kuheshimu sheria za nchi ikiwemo kuzingatia masharti ya biashara wanazoziendesha ili kuondoa migogoro isiyokuwa ya lazima kati yao na mamlaka nyingine za nchi.
 
Hata hivyo alisema tatizo lililopo mkoani Shinyanga linatokana na wakala wa vipimo kuwatoza gharama kubwa wafanyabiashara pale wanapofanya ukaguzi wa mizani pia hupenda kutumia ubabe wanapotekeleza majukumu yao hali inayosababisha wafanyabiashara wengi waanze kuwakwepa.
 
“TCCIA mkoani Shinyanga tumeshangazwa na taarifa zilizotolewa mwishoni mwa wiki iliyopita na meneja wakala wa vipimo mkoani Shinyanga akidai kuna wafanyabiashara wengi wanye tabia ya kuchezea vipimo vyao kwa lengo la kuwapunja wateja wao, lakini ukweli halisi sivyo ulivyo,”
 
“Hatusemi wafanyabiashara wote ni wasafi, bali tunachokipigia kelele ni suala la kutozwa fedha nyingi kinyume na utaratibu, kila mwaka wakati wa ukaguzi tunatozwa kuanzia shilingi 70,000 na kuendelea kulingana na ukubwa wa mizani badala ya shilingi 40,000 za kisheria, hilo ndilo tunalolipinga kwa nguvu zote kila mwaka,” alieleza Musula.
 
Akifafanua alisema kisheria ada ya ukaguzi kwa mujibu wa sheria ya vipimo sura namba 340 iliyofanyiwa mapitio mwaka 2002 mizani ya kawaida isiyozidi uzito wa kilogramu 300 hupaswa kulipiwa ada ya shilingi 40,000 pekee lakini hata hivyo hutozwa shilingi 30,000 nyingine ikiwa ni gharama za matengenezo iwapo mzani una matatizo.
 
“Sasa ajabu ni kwamba maofisa vipimo wetu baada ya kufanya ukaguzi baadae hujigeuza ndiyo wasemaji wa mafundi wanaorekebisha mizani  unapokuwa na matatizo, wanatutoza shilingi 30,000 kwa kila mzani bila kujali ni mzima au mbovu  wanalazimisha lazima zilipwe hapa ndiyo penye tatizo, maana ulazimishaji huu ni sawa  na wizi,”
 
“Kibaya zaidi angalia hizi stakabadhi zao (angalia picha juu) kuna hii ya shilingi 40,000 ni ya serikali, lakini hii ya pili ni ya kampuni inayofanya marekebisho ya mizani zenye matatizo, ajabu mtu anayeandika stakabadhi hizi ni mmoja wa maofisa vipimo badala ya mafundi wenyewe, utaratibu huu TCCIA tunaupinga na kuupiga vita,” alieleza Musula.
 
Musula alisema wafanyabiashara mkoani Shinyanga hawapingani na sheria zilizopo bali wanachokipinga ni vitendo vya uonevu wanavyotendewa na maofisa vipimo mkoani humo ambao mara nyingi hutumia vitisho wanapotekeleza majukumu yao na hata wanapotoa taarifa zao kwa ajili ya kazi ya ukaguzi huwa hazioneshi tarehe na eneo husika la kufanyia kazi hiyo.
 
Hivi karibuni wakala wa vipimo mkoani Shinyanga ulitoa taarifa ya kuwatahadharisha wafanyabiashara wenye tabia ya kuchezea mizani zao kwa lengo la kuwapunja wateja baada ya kufanya ukaguzi sehemu mbalimbali na kuwakamata baadhi ya wafanyabiashara waliokutwa wameharibu mizani zao kwa makusudi.

Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top