Umoja wa mataifa umewataka wanasiasa na viongozi wa kidini Nchini Myanmar kulaani matamshi ya uchochezi na chuki yaliyotolewa na kiongozi mmoja wa kibudha dhidi ya mjumbe maalum wa umoja wa mataifa.


Kiongozi huyo wa kibudha Ashin Wirathu alimtusi mjumbe wa Umoja wa Mataifa kwa kumuita ''Kahaba'' na ''Mbwa''
Mkuu wa kitengo cha haki za Binadamu katika Umoja huo, Zeid Ra'ad Al Hussein alisema matamshi ya kiongozi huyo ni ya chuki na ya uchochezi.

Aliyetusiwa ni mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa kutoka nchini Korea Kusini, Yanghee Lee, aliyekuwa nchini Myanmar wiki jana kuzungumzia hali inayowakumba waisilamu ambao ni wachache nchini humo. 

Wirathu alifungwa jela karibu miaka kumi kwa kuchochea ghasia dhidi ya waislamu. 

Mtawa huyo ni kiongozi wa vuguvugu la 969, ambalo linataka Myanmar kuwa nchi ya Kibudha pekee yake na pia amekuwa akitoa wito wa waaisilamu kuwekewa vikwazo pamoja na kudharauliwa.

Bwana Zeid aliyataja matamshi ya kiongozi huyo wa kibudha kama matusi makubwa na ya kibaguzi. 

"Ningependa kutoa wito kwa viongozi wa kidini na kisiasa nchini Myanmar kulaani uchochezi wa aina yoyote na chuki,'' alisema bwana Zeid. 

Tangu utawala wa kijeshi kumalizika nchini Myanmar iliyokuwa inajulikana kama Burma mnamo mwaka 2011 , watawa wamekuwa wakitaka dini ya kibudha kuwa dini ya kitaifa na harakati hizo zimekuwa zikishika kasi kote nchini.

Mwaka 2012, mamia ya watu waliuawa na maelfu ya wengine kuachwa bila makao baada ya ghasia kuzuka dhidi ya waumini wa kibudha na waisilamu katika jimbo la Rakhine hasa kutoka kwa waisilamu wa Rohingya.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top