Kaburi la marehemu Bernadetha Stephen likiwa limefukuliwa na watu wasiojulikana kama jinsi linavyoonekana kwa kutoka juu.
Mkuu wa Upelelezi Polisi Mkoani Shinyanga, Kamanda Mussa Taibu (aliyeinama kushoto) akiangalia jinsi kaburi lilivyofukuliwa.
Hali hali ya kaburi lilivyokuwa likionekana baada ya kufukuliwa na watu wasiojulikana.
Wananchi wakiangalia jinsi kaburi lilivyofukuliwa.
Mkuu wa Upelelezi Polisi Mkoa wa Shinyanga, Mussa Taibu (kushoto mwenye suti nyeusi na karatasi mkononi) akitoa maelezo kwa wananchi muda mfupi baada ya kuagiza kufukiwa upya kwa kaburi lililokuwa limefukuliwa.
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida kaburi la marehemu Bernadetha Stephen (35) ambaye mwili wake ulizikwa na kifaranga cha kuku tumboni hivi karibuni katika kile kilichodaiwa kutekeleza mila za kikurya limefukuliwa  usiku na watu wasiojulikana.
Hali hiyo imezua sintofahamu miongoni mwa wakazi wa kata ya Masekelo Manispaa ya Shinyanga akiwemo mume wa marehemu huyo Maulidi Njunju ambaye hata hivyo hakutaka kuzungumza lolote mbele ya waandishi wa habari.
 
Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo kaburi hilo lilifukuliwa usiku wa kuamkia Januari 13, mwaka huu ambapo baadhi ya wananchi walitoa taarifa juu ya kitendo hicho na kusababisha umati wa wananchi kufurika katika makaburi hayo kwa lengo la kujionea kilichotokea.
 
Mbali ya kufukuliwa kwa kaburi hilo baadhi ya watu walivumisha uvumi mjini humo kwamba mwili wa marehemu Bernadetha ulionekana ukiwa umesimama juu ya kaburi hilo hali iliyowashitua baadhi ya watu hata hivyo hakuna hata mmoja aliyethibitisha kuonekana kwa mwili huo kama ilivyokuwa ikivumishwa.
 
Kwa upande wake mjumbe mwingine wa serikali ya mtaa wa Mapinduzi Deogratius Masanja alisema mume wa marehemu Bernadetha awali alimpa taarifa kwamba siku tatu zilizopita ndugu wawili wa marehemu huyo walionekana katika mtaa huo katika mazingira ya kutatanisha.
 
Hata hivyo alisema alihisi huenda walikuja kumalizia mambo yao ya kimila baada ya mazishi yaliyofanyika mnamo Januari 3, mwaka huu lakini pia baadhi ya wakazi wa maeneo jirani na makaburi hayo walidai juzi usiku waliliona gari moja likiranda randa katika maeneo hayo japokuwa hawakuweza kubaini iwapo ni ndugu wa marehemu au watu wengine.
 
Akizungumzia tukio hilo katika eneo la makaburi hayo ya kata ya Masekelo, Mkuu wa upelelezi wa Polisi Mkoa wa Shinyanga (RCO), Mussa Taibu mbali ya kulaani kitendo hicho aliwataka wakazi wa mkoa wa Shinyanga kujiepusha na vitendo vya kishirikina ambavyo havina faida yoyote mbali ya kuwapotezea muda wao bure na badala yake wamrejee mungu.
 
Marehemu Bernadetha Stephen alifariki dunia Januari mosi mwaka huu katika hospitali ya serikali mkoani Shinyanga alikokuwa amelazwa kutokana na kusumbuliwa na uvimbe tumboni,  alizikwa Januari 3, hata hivyo wakati wa mazishi yake ndugu walizua tafrani kubwa baada ya kulazimisha kufanyika kwa mitambiko ya kimila na hivyo kumzika akiwa na kifaranga cha kuku tumboni.
 
 
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top