KAMANDA WA POLISI WA MKOA WA SHINYANGA, JUSTUS KAMUGISHA
MAMA mdogo wa mwanafunzi anayesoma kidato cha kwanza (13) (jina limehifadhiwa) aliyebakwa na askari wa kikosi cha kuzuia ghasia (FFU) mkoani Shinyanga amelilalamikia jeshi la polisi kwa kitendo cha kumpora mtoto wake hali ambayo imesababisha ashindwe kurudi shuleni kuendelea na masomo yake.
 
Mbali ya kulalamikia kuporwa kwa mtoto wake pia mama huyo Neema Elisha ameelezea wasiwasi wake kutokana na mwenendo mzima wa kesi ya polisi huyo mbakaji inavyoendeshwa ikionesha dalili zisizoacha shaka kwamba inachezewa kwa lengo la kutaka kuharibu ushahidi ili kumnusuru mtuhumiwa huyo.
 
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Shinyanga, Neema alisema mara baada ya mwanae kubakwa na mmoja wa askari wa kikosi cha FFU aliyemtaja kwa jina moja la Alex mnamo Januari 4, mwaka huu na wao kufungua mashitaka kituoni wamekuwa wakisumbuliwa kila mara pasipo sababu za msingi.
 
Akifafanua alisema katika hali isiyokuwa ya kawaida baada ya mtoto wake kutoa maelezo ya jinsi alivyobakwa polisi walikula njama na kumpora kutoka nyumbani kwake Ngokolo manispaa ya Shinyanga katika mazingira ya kutatanisha ambapo walimlazimisha atoe upya maelezo yake huku akishinikizwa aeleze hakubakwa bali polisi aliyemtendea kitendo hicho ni mpenzi wake.
 
“Kinachotia wasiwasi mpaka sasa sifahamu mwanangu anaishi wapi, nilipokwenda kituoni kuulizia waliniambia eti anatunzwa na ustawi wa jamii baada ya mtoto kulalamika kwamba ninampiga sana kushinikiza aseme alibakwa wakati siyo kweli, lakini nashangaa polisi wao ndiyo watuhumiwa wanakaaje na mlalamikaji? hapa kweli kuna haki itatendeka?” alihoji Neema.
 
Alisema pamoja na kwamba wao ndiyo walalamikaji mpaka sasa hawana taarifa zozote iwapo kesi hiyo imefikishwa mahakamani au bado na hata juzi walipofuatilia ofisini kwa mkuu wa kituo (OCS) kutaka kufahamu mtoto alipo na kama kesi imefikishwa mahakamani walifukuzwa na kutakiwa waondoke mara moja kituoni hapo kwa vile wao ni kichomi.
 
Kamanda wa Polisi mkoani Shinyanga Justus Kamugisha alikanusha madai ya polisi kumpora mtoto huyo na kufafanua kuwa baada ya kufuatilia alibaini mtoto alikwenda mwenyewe kituoni akilalamika kupigwa sana na mama yake na kwamba kutokana na majadiliano yaliyofanyika walikubaliana akatunzwe na watu wa ustawi wa jamii mpaka pale kesi yake itakapoanza kusikilizwa.
 
“Polisi hatuwezi kufanya upuuzi huo, nashangaa ninyi waandishi  na watu wa Agape sijui kwa nini mnalifuatilia sana hili, nilipopewa taarifa za kupotea kwake nilishituka, nilifuatilia mwenyewe na nilipewa taarifa yupo kituoni amekimbia kwao baada ya kupigwa sana, tukaone vyema atunzwe na watu wa ustawi, sasa vipi idaiwe tumempora?” alieleza Kamugisha.
 
Akizungumzia suala la mtoto huyo kulazimishwa kutoa maelezo zaidi ya mara tatu Kamugisha alisema huo ni utaratibu wa polisi na kwamba wanaweza kuchukua maelezo kutoka kwa mlalamikaji hata zaidi ya mara kumi iwapo wataona yale ya awali bado hayajajitoshelezi na kufafanua kuwa utaratibu huo ni wa kawaida katika masuala ya kiupelelezi.
 
“Tutahakikisha haki inatendeka, huyu polisi iwapo atabainika amefanya kosa, kwanza tutamvua upolisi wake na kumpeleka mahakamani kujibu shitaka lake, binafsi nitatoa taarifa kamili mara baada ya kukamilika kwa upelelezi, hakuna mtu anayetaka kumlinda mtuhumiwa iwapo atabainika ametenda kosa,” alieleza Kamugisha.
 
Kwa upande wake mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Festo Kang’ombe alikiri kupata taarifa za ofisa wake wa Ustawi wa Jamii, Emmanuel Nhabi kukabidhiwa mtoto huyo japokuwa hakuwa na taarifa kamili ya tukio zima lililosababisha akabidhiwe mikononi mwa ustawi wa jamii.
 
Akizungumza mbele ya mkurugenzi wake Nhabi alikiri kukabidhiwa mtoto huyo na mkuu wa kituo cha polisi (OCS) cha mjini Shinyanga baada ya kuelezwa alikuwa akifanyiwa vitendo vya ukatili na kutakiwa akamkabidhi katika kituo cha Buhangija Jumuishi wakati akisubiri kesi yake, hata hivyo alisema  juzi alilazimika kumrejesha tena mikononi mwa polisi wenyewe.
 
Akizungumzia suala hilo Mwanasheria mkuu wa serikali mkoani Shinyanga, Seth Mkemwa alikiri kupokea jalada la kesi ya polisi wa FFU anayetuhumiwa kubaka na tayari kesi hiyo imefikishwa mahakamani kwa kutajwa mara ya kwanza ambapo alisema kiutaratibu kwa mara ya kwanza siyo lazima mama wa mtoto kupewa taarifa au kulazimika kuwepo mahakamani.
 
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top