Haya ni majeraha yanayotokana na shambulizi alilopokea mwananchi huyu kutoka kwa askari Magereza wa Gereza la Shinyanga.
KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida mkazi wa kijiji cha Nhelegani manispaa ya Shinyanga ameshambuliwa kwa kipigo na askari wa Jeshi la Magereza na kujeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za mwili wake baada ya kugoma kuwapa askari hao soda na biskuti.


Tukio hilo la aina yake limetokea katika Gereza la wilaya ya Shinyanga wakati mwananchi huyo aliyejitambulisha kwa jina la Lugenzi Maguta (45) alipokwenda kumsalimia ndugu yake aliyeko mahabusu aliyemtaja kwa jina la Mahushi Nangale.

Mbali ya kushambuliwa kwa kipigo hadi kupasuka katika miguu yake yote miwili kutokana na kupigwa virungu bado askari magereza hao wanadaiwa kumgeuzia kibao kwa kumfungulia shitaka la kufanya fujo gerezani tuhuma ambazo alidai ni za uongo kwa vile hakuna fujo yoyote iliyotokea.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati akipatiwa matibabu katika hospitali ya serikali, Maguta alisema askari waliomshambulia waliokuwa wamevaa kiraia hawakuwa zamu bali walikuwa nje ya gereza waliamua kumshambulia kwa madai walichukizwa na kitendo chake cha kukataa kuacha soda na biskuti alizokuwa nazo.

“Baadaye wale askari waliomba tusameheane lakini walielekezwa twende nao pamoja kituo cha polisi na kama ni kusameheana tukaelewane huko huko, maana yule kiongozi wao alisema tukielewana kienyeji mimi baadae naweza kuwageuka, tulikwenda hadi kituoni na sote tukatoa maelezo yetu, na kisha nilipewa PF 3 kwenda kutibiwa,” alieleza Magucha.

Alisema baada ya kupewa fomu namba tatu aliongozana kwenda hospitali na askari wote wanne wawili waliokuwa zamu na waliomshambulia kwa kipigo ambako baada ya kupimwa fomu ilijazwa na kurudishwa polisi hata hivyo wakiwa wanarejea kituoni askari wale walimlazimisha akaeleze kuwa hakuumia sana.

Kwa upande wake msemaji wa Jeshi la Magereza mkoani Shinyanga, ACP Grace Massawe alikanusha kuwepo kwa tukio lolote la kutokea fujo gerezani wala kushambuliwa kwa mwananchi ye yote aliyekuwa amekwenda kumsalimia ndugu yake.

“Ndugu zangu hapa ofisini hatuna taarifa zozote za kushambuliwa kwa raia gerezani au kutokea fujo, taarifa hizi ndiyo kwanza nazisikia kutoka kwenu waandishi, nakushukuruni sana tutalifanyia kazi suala hili mara moja, maana haturuhusu watu kupigwa ovyo, achilia mbali raia wa kawaida awe mahabusu au mfungwa hawaruhusiwi kupigwa,” alieleza Massawe.

Naye Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Justus Kamugisha hakuwa na taarifa zozote kuhusiana na tukio hilo ambapo alisema atawasiliana na mkuu wa kituo cha polisi wilaya (OCD) ili apate taarifa kamili na kama kweli limetokea ofisi yake itafanya uchunguzi wa kina ili kubaini ukweli wake na sheria ichukue mkondo wake kwa watakaobainika.


Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top