Shinyanga

WAKAZI  wa Mkoa wa Shinyanga wameshauriwa kutopatwa na hofu yoyote juu ya ugonjwa hatari wa Ebola na kwamba mpaka hivi sasa hakuna taarifa zozote za kuwepo kwa ugonjwa huo hapa nchini.


Mbali ya kuondolewa hofu hiyo pia wameshauriwa kupuuza taarifa  zinazosambazwa na baadhi ya watu wakidai ugonjwa huo unaweza kuingia nchini wakati wowote baada ya kupatikana kwa mtu mmoja nchini Rwanda anayehisiwa kuwa na Ebola.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, mganga mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Dkt. Ntuli Kapologwe alisema mpaka hivi sasa hakuna taarifa zozote za kuwepo kwa ugonjwa huo nchini na kwamba hata kama utabainika kuingia nchini anayepaswa kutoa taarifa kitaifa ni Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.

Dkt. Kapologwe alisema wapo baadhi ya watu wamekuwa wakisambaza taarifa zinazowatia hofu wananchi na kwamba katika ngazi ya mkoa mtu anayestahili kutoa taarifa ya kuwepo ugonjwa huo ni mganga mkuu wa mkoa ambaye ndiye mtaalamu katika masuala yote ya kiafya mkoani.

“Mpaka sasa hakuna taarifa za kuwepo kwa ugonjwa huu, hivyo hakuna  sababu  ya kuwa na wasiwasi, badala yake waendelee kufanya kazi zao bila ya hofu yoyote, na iwapo itabainika kuna mtu mwenye ugonjwa huo, basi wizara ya afya au waganga wa mikoa ndiyo wenye wajibu wa kutoa taarifa mara moja,” alisema.

Alisema tayari yeye na timu ya wataalamu wenzake mkoani humo wamekaa na kujipanga ili pale patakapotokea mtu ye yote atakayehisiwa kuwa na ugonjwa huo, timu hiyo iweze kwenda mara moja sehemu alipo mgonjwa huyo kwa lengo la kumchunguza kwa kina ili kujiridhisha kabla ya kutangaza kuwa ana ugonjwa wa Ebola.

“Tumejiandaa kikamilifu katika kukabiliana na ugonjwa huu iwapo itatokea umeingia mkoani kwetu, tayari tumeisha nunua vifaa tiba na vizuizi vya ugonjwa huo na pia vifaa vilivyoagizwa na serikali viko njiani tunatarajia kuvipokea wakati wowote kuanzia sasa,”

“Tunachowaomba  wananchi popote pale walipo watakapomuona mtu ye yote anayeonesha dalili za kuwa na ugonjwa usio wa kawaida wamuwahishe hospitali mara moja badala ya kutafuta tiba mbadala za mitaani au kumpeleka kwa waganga wa kienyeji,”

“Ni muhimu kwanza wakazielewa dalili za ugonjwa huu ambazo ni mgonjwa kuwa na homa kali huku akitokwa na damu sehemu zote za wazi katika mwili wake, hivyo mtu akiwa na dalili hizo ni muhimu awahishwe hospitali bila ya kucheleweshwa,” alieleza Dkt. Kapologwe.


Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top