Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Shinyanga mjini, Kanali Maulid akikabidhi funguo za basi dogo kwa mwenyekiti wa timu ya Stand United, Aman Vicent baada ya kukabidhi rasmi hilo ikiwa ni ahadi ya mbunge wa jimbo la Shinyanga mjini, Stephen Masele.
 
Mwenyekiti Aman akitoa neno la shukrani kwa mgeni rasmi.
Huu ndiyo mchuma waliokabidhiwa rasmi wachezaji wa timu ya Stand United Shinyanga baada ya kufanikiwa kupanda daraja na hivi sasa watacheza Ligi Kuu ya Vodacom.
 
Baadhi ya viongozi waliohudhuria sherehe za makabidhiano wakiwa ndani ya basi hilo baada ya kukabidhiwa rasmi kwa viongozi wa timu ya Stand United. Wa kwanza kulia ni Naibu Meya wa Manispaa ya Shinyanga, David Nkulila.
HATIMAYE mbunge wa Jimbo la Shinyanga mjini (CCM) Steven Masele ametimiza rasmi ahadi yake ya kuipatia timu ya Stand United  basi dogo aina ya Coaster litakalowasaidia kwa ajili ya usafiri wakati wakishiriki Ligi Kuu ya Vodacom.


Mbunge Masele aliwaahidi wachezaji wa timu hiyo kwamba iwapo watafanikiwa kupanda daraja na kucheza ligi kuu ya Vodacom basi mchango wake kwao itakuwa ni kuwapatia usafiri ili waweze kushiriki vyema katika kinyang’anyiro hicho.

Basi hilo dogo lilikabidhiwa katika sherehe fupi za makabidhiano zilizofanyika katika viwanja vya kituo cha mabasi yaendayo wilayani cha mjini humo ambapo mgeni rasmi alikuwa mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Shinyanga mjini, Kanali Maulid.

Akikabidhi rasmi basi hilo kwa viongozi wa timu ya Stand United kwa niaba ya mbunge Masele ambaye hivi sasa yuko nje ya nchi kikazi, Kanali Maulidi aliwapongeza wachezaji na viongozi wote wa timu hiyo kwa jinsi walivyoweza kujituma na kufanikiwa kupanda daraja na hivyo mwaka huu watacheza ligi kuu ya Vodacom.

“Nimekuja hapa kwa niaba ya mbunge wenu Steven Masele, amenituma niwakabidhi msaada huu aliokuwa amewaahidi, leo hii ametimiza ahadi yake, lakini name pia nitumie fursa hii kukupongezeni kwa juhudi zenu zilizowesha mkafikia hatua hii, niwaombe msibweteke ili kuepuka kushuka daraja,”

“Sisi wakazi wa Shinyanga ahadi yetu ni kuendelea kuwaunga mkono ili mshiriki vyema ligi hii ya Vodacom, CCM kwa upande wake tumewashauri wenzetu wa manispaa waangalie jinsi gani watakusaidieni, maana sasa hii timu ipo katika himaya yake, pale itakapokuwa ikicheza yapo mapato fulani yataingia manispaa,” alieleza Kanali Maulid.

Awali viongozi wa timu hiyo, Amani Vincet ambaye ni mwenyekiti na ofisa habari wa timu, Isaack Kisesa walimpongeza mbunge Masele kwa kutimiza ahadi yake ambapo waliahidi kulitumia vizuri basi hilo ambalo kwa kiasi kikubwa litawapunguzia tatizo la usafiri watakapokuwa wakicheza michezo yao ya ligi ya Vodacom.

“Tuna kila sababu leo hii kumpongeza mbunge wetu kwa kutimiza ahadi yake kwetu, lakini tuwaombe wadau wengine wa mchezo wa mpira wa miguu hapa mkoani waendelea kujitokeza kutuchangia michango mbalimbali ili tuweze kushiriki vizuri ligi hii, tuache kuweka siasa katika michezo, sisi tunachoahidi ni kuhakikisha hatushuki daraja,” alieleza Vicent.

Mwisho.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top