Ofisaelimu ya mpiga kura kutoka Tume ya Uchaguzi ya Taifa, Salvatory Alute (aliyesimama) akitoa maelezo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) katikati ni Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kushoto ni Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga, Festo Kang'ombe.
Baadhi ya waandishi wa habari mkoani Shinyanga wakifuatilia hotuba ya mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji mstaafu Damian Lubuva alipokuwa akifungua mkutano kati ya tume yake na waandishi wa habari.

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imewatoa hofu watanzania na kuwaomba waendelee kuiamini pamoja na kwamba mwenyekiti na makamishina wake wanateuliwa na Rais Jakaya Kikwete.

Hali hiyo ilibainishwa  na Mwenyekiti wa tume hiyo, Jaji mstaafu Damian Lubuva alipofungua mkutano kati ya tume na waandishi wa habari mkoani Shinyanga kwa ajili ya kupatiwa taarifa juu ya maandalizi ya uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura kwa mfumo wa teknolojia ya Biometrick Voter Registration (BVR).

Jaji Lubuva amesema pamoja na kwamba Rais ndiye aliyemteua yeye pamoja na makamishina wengine wa tume lakini haiwi sababu ya kuwafanya watanzania waamini kuwa tume hiyo siyo huru na kwamba tangu alipoteuliwa kuwa mwenyekiti wa tume haijatokea hata siku moja kuelekezwa na Rais au chama chochote cha siasa kitu cha kufanya.

“Ndugu zangu si kweli kwamba kitendo cha Rais kumteua mwenyekiti wa tume ya uchaguzi pamoja na makamishina wake kinaondoa uhuru wa tume hiyo katika kutimiza wajibu wake, binafsi tangu niteuliwe, Rais wala kiongozi ye yote wa siasa hawajawahi kunielekeza nini cha kufanya, muda wote tume ipo huru,”

“Tatizo hapa ni hisia zilizomo ndani ya vichwa vya wananchi, kwamba kwa vile tunateuliwa na Rais basi hatuwezi kuwa huru, lakini tupende tusipende mamlaka ya mwisho ya uteuzi bado yataendelea kubaki mkononi mwa Rais wa nchi labda tusubiri iwapo mchakato wa katiba mpya utapita kule Dodoma ndani ya bunge la katiba,” anaeleza.

Akizungumzia uboreshwaji wa daftari la kudumu la wapiga kura kwa kutumia teknolojia ya Biometric Voter Registration (BVR) alisema lengo ni kuondoa changamoto zilizojitokeza katika matumizi ya teknolojia ya Optical Mark Recognition (OMR) uliosababisha daftari la kudumu la wapiga kura kuwa na kasoro nyingi.

“Matumizi ya BVR yatapunguza au kuondoa kabisa matatizo yaliyomo kwenye daftari lililopo ikiwemo kuzuia mtu kujiandikisha zaidi ya mara moja. Lakini pia tunaomba ieleweke na kusisitiza kuwa kitambulisho hiki cha BVR – Kit ni kwa ajili ya uandikishaji wapiga kura tu na hatutopiga kura kwa njia ya kielektroniki au vinginevyo,” anaeleza Jaji Lubuva.

Akifafanua kuhusu uboreshaji huo wa daftari,  alisema baada ya kuanza kwa uandikishaji wapiga kura wote waliojiandikisha awali na ambao hawajaandikishwa walazimika kwenda vituoni kwa ajili ya kuandikishwa upya kwa maana ya kuchukuliwa taarifa za kibaiolojia kwa wale waliomo ndani ya daftari na kubadili taarifa kwa waliohama maeneo au kubadili majina.

Jaji Lubuva aliwaomba waandishi wa habari kusaidia kuihamasisha jamii ili ione umuhimu wa kwenda kujiandikisha pale kazi hiyo itakapoanza na waache kuwasikiliza wapotoshaji wanaodai kwamba uboreshwaji wa daftari la kudumu la wapiga kura umelenga kukisaidia au kukipendelea chama chochote cha siasa.

“Waandishi ni sehemu muhimu katika jamii, ninyi mkielewa itakuwa rahisi kuielimisha jamii, tuwaomba mtusaidie kuwaondoa wasiwasi wananchi kwamba wasiwe na tabia ya kuogopa mabadiliko, wapo wanaohofu yasije kutokea kama ilivyotokea katika nchi jirani ya Kenya, kwetu hapa mfumo huu wa BVR utaishia katika uandikishaji pekee, upigaji kura utakuwa kwa mfumo uleule tuliouzoea,”

“Kwa utaratibu huu wa sasa, vituo vya kujiandikisha vimeongezeka kutoka 24,919 hadi 40,015 vilivyowekwa kuanzia ngazi ya vitongoji, vijiji, mitaa ili kuwezesha kuwa karibu zaidi na wananchi ili kupunguza malalamiko ya umbali wa vituo vya kujiandikisha na kuongeza mwamko wa kujiandikisha na kupiga kura,” anasema Jaji Lubuva.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top