Kahama

VIJANA nchini na watanzania wengine wameshauriwa kutumia fursa mbalimbali zilizopo ili waweze kujipatia ajira halali badala ya kukimbilia kufanya shughuli ambazo mara nyingi huwangiza wengi wao matatani ikiwemo uuzaji wa madawa ya kulevya.

Ushauri huo umetolewa juzi na mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Khamis Mgeja alipokuwa akikabidhi msaada wa TV yenye thamani ya shilingi 260,000 kwa kijiwe cha uuzaji wa kahawa maarufu kwa jina la BBC katika mji mdogo wa Isaka wilayani Kahama.

Mgeja alisema baadhi ya vijana wamekuwa wakishawishika kupata utajiri wa haraka haraka na hivyo kujiingiza katika shughuli zisizo halali ikiwemo uuzaji wa madawa ya kulevya tatizo ambalo linaelekea kuwa sugu katika nchi hii na kuchafua sifa iliyokuwa nayo miaka ya nyuma.


Alisema iwapo vijana katika nchi hii watazitumia vizuri fursa mbalimbali zilizopo hapa nchini wanaweza kujipatia ajira zitakazowaingizia kipato kikubwa badala ya kufanya shughuli ambazo mara nyingi husababisha waishie kufungwa gerezani.

Akifafanua alisema Tanzania ni moja ya nchi duniani iliyobarikiwa kuwa na fursa kupitia sekta za kilimo, ufugaji na uvuvi, ujasiriamali mdogo na uanzishaji wa viwanda vidogo ambazo watanzania wanaweza kuzitumia na kujipatia ajira bila ya kutegemea kuajiriwa ofisini na kujikwamua kiuchumi badala ya kufanya kazi haramu.

“Ndugu zangu hasa ninyi vijana Tanzania  tuna fursa nyingi iwapo zitatumika vizuri mnaweza kujiajiri wenyewe badala ya kusubiri kuajiriwa ofisini, msiwe na tamaa ya kupata utajiri wa haraka haraka bila ya kufanya kazi halali na badala yake kukimbilia kazi haramu kama vile uuzaji wa madawa ya kulevya,”


“Maisha bora yaliyoahidiwa na serikali ya CCM siyo kwamba yatadondoka kutoka mbinguni, hapana, bali ni kwa kufanya kazi, tumieni fursa zilizopo, na sasa hivi mkoa wetu tuna viwanda vingi vipya vimejengwa ni fursa pia ya kujipatia ajira, kazi ya serikali ni kuibua fursa, ninyi mnazitumia,” alieleza Mgeja.

Awali akipokea msaada huo wa TV mwenyekiti wa kikundi cha wajasiliamali hao wauza kahawa, Ali Msangi alimshukuru mwenyekiti huyo wa CCM mkoani Shinyanga ambapo alisema msaada huo umefika wakati muafaka kwa vile wataweza kufuatilia kwa kina mjadala wa rasimu ya pili ya katiba unaoendelea hivi sasa bungeni.

Mwishoni mwa mwaka uliopita wajasiriamali hao walimuomba mwenyekiti wa CCM mkoani humo aliyekuwa katika ziara ya kukagua utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010 awasaidie kupata TV moja itakayowasaidia kupata habari mbalimbali za dunia nyakati za asubuhi na jioni ili waweze kuelewa yanayojiri ndani na nje ya nchi.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top