Kamishna wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini, Pius Nyambacha.
 
Kamishna Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji akizungumza na wana habari wa mkoani Shinyanga.



JESHI la Zimamoto na Uokoaji nchini limewaomba wananchi kuacha kutoa lawama dhidi yake kila pale panapotokea janga la moto na badala yake walisaidie kwa kuishinikiza serikali itatue changamoto kadhaa zinazolikabili ili liweze kufanya kazi zake kwa ufanisi mzuri.
 
Ombi hilo limetolewa na Kamishna Mkuu wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini, Pius Nyambacha alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini Shinyanga muda mfupi baada ya kuwasili mkoani humo kukagua shughuli za jeshi hilo.
 
Nyambacha alisema kwa kipindi kirefu Jeshi la Zimamoto limekuwa likilaumiwa kwa uzembe kutokana na kushindwa kukabiliana na majanga ya moto katika maeneo mengi nchini ambapo hata hivyo jamii haichunguzi kwa kina chanzo chake na badala yake hubaki wakilalamika kulaumu.
 
Alisema zipo changamoto nyingi zinazolikabili Jeshi lake na hivyo kushindwa kufanya kazi zake kwa ufanisi ikiwemo suala la uhaba wa maeneo ya kuongezea maji mijini pale linapotokea tatizo la nyumba kuungua moto kutokana na kuhitajika kwa maji mengi ili kuweza kukabiliana na moto.
 
“Yapo mambo mengi ambayo tunaamini wenzetu wananchi hawayaelewi na hivyo kila mara kutushushia lawama kwamba sisi ni wazembe, ukweli tunajitahidi sana, sasa tuwaombe wenzetu wana habari mtusaidie kuielimisha jamii ili iweze kuwa na uelewa wa kutosha jinsi tunavyofanya hii kazi hasa upande wa uzimaji wa moto,”
 
“Zipo changamoto nyingi zinazotukabili hasa tatizo la uhaba wa maeneo ya kuongezea maji katika sehemu nyingi za miji yetu, wananchi wanapaswa waelewe kuwa magari yetu hutumia lita 2000 za maji ndani ya dakika mbili yanapozima moto, hivyo yanapomalizika lazima tuongeze mengine,” alieleza Nyambacha.
 
Akifafanua magari mengi yaliyopo nchini hayana uwezo wa kuchukua maji mengi zaidi hivyo yanapomalizika hulazimika kurudi katika eneo la kujazia maji na mara nyingi maeneo hayo yanakuwa mbali na eneo la tukio la moto na kwamba ndiyo sababu ya wananchi kulalamika kwamba zimamoto walikwenda bila maji.
 
“Hili ni tatizo kubwa sana, sisi wenyewe hatupendi iwe hivyo, laiti miji yetu ingekuwa na utaratibu wa kujenga (viosk) vingi mitaani kwa ajili ya magari yetu kujazia maji tungeweza kukabiliana vizuri na majanga ya moto yanayotokea katika maeneo yetu, lakini pia lipo tatizo la uchakavu wa magari, hili linafanyiwa kazi na serikali,” alieleza.
 
Kwa upande wake Kamanda wa Jeshi la Zimamoto mkoani Shinyanga, Elias Mugisha aliiomba serikali iuongezee mkoa wake askari wa kutosha ili kuweza kufanya kazi zao kwa ufanisi ambapo alisema mpaka sasa mkoa huo una askari 41 katika wilaya zote ikiwemo na viwanja vya ndege vya Ibadakuli na Kahama.
 
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top