Moja ya majengo ya Hospitali ya wilaya ya Kishapu, hili ni jengo la wajawazito.
 
Sehemu ya Jengo la Matibabu ya nje (OPD)
 
Madiwani wakiongozwa na mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu, Justine Sheka wakiwa nje ya moja ya majengo ya hospitali mipya ya wilaya.
 
Hapa ni kwenye lango kuu la kuingilia Hospitali.
WANANCHI wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga wamewapongeza madiwani wa halmashauri hiyo kutokana na kusimamia vyema miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika wilaya yao ikiwemo ujenzi wa hospitali ya wilaya.
 
Wakizungumza na waandishi wa habari wilayani humo juzi muda mfupi mara baada ya madiwani kukamilisha ziara ya ukaguzi wa majengo ya hospitali ya wilaya hiyo ambayo yamekamilika kwa takribani asilimia 85, baadhi ya wananchi walisema kukamilika kwa hospitali hiyo kutawaondolea kero ya kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma za matibabu.
 
Wananchi hao walisema kwa kipindi kirefu tangu wilaya ya Kishapu ilipoanzishwa hawakuwa na huduma ya hospitali ya wilaya hali iliyowalazimu kusafiri zaidi ya kilometa 40 kwenda Shinyanga mjini ili kuweza kupata huduma za matibabu ya uhakika.
 
Mmoja wa wananchi hao Boniface Maganga alisema kukamilika kwa ujenzi wa hospitali ya wilaya kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na juhudi na usimamizi wa kutosha wa madiwani wa halmashauri hiyo ya wilaya na kwamba wameonesha jinsi gani walivyowawakilisha vizuri wapiga kura wao.
 
“Binafsi nimefurahishwa sana kuona hatimae baada ya muda mfupi watu wa Kishapu tutakuwa na hospitali yetu ya wilaya, tena ya kisasa kutokana na majengo yake yote kujengwa kisasa, hatutalazimika tena kwenda Shinyanga au hospitali ya Kolandoto kutafuta matibabu, kwa hili tunawapongeza madiwani wetu kwa kazi nzuri,” alisema Maganga.
 
Mkazi wa Mhunze madukani Salum Bakari alisema kutokana na kazi nzuri iliyofanywa na madiwani wao bila kujali itikadi ya vyama vyao vya siasa ni vizuri wananchi wakawapatia kipindi kingine cha miaka mitano ili wakamilishe shughuli zote za kimaendeleo walizozianzisha.
 
“Kwa kweli madiwani wetu wameweza kufuta kabisa aibu ambayo wilaya yetu miaka ya nyuma tuliipata baada ya kufichuliwa ufisadi wa wizi wa zaidi ya shilingi bilioni sita, walikaa chini na kuamua kufanya kazi, kweli kazi imefanyika, na sasa Kishapu ni shapu kwa maendeleo na siyo kwa ufisadi,” alieleza Bakari.
Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu, Jane Mutagurwa (wa kwanza kulia) akiwa pamoja na madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Kishapu wakipokea maelekezo kutoka kwa mmoja wa wataalamu juu ya ujenzi wa hospitali ya wilaya ya Kishapu
 
Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Kishapu, Jane Mutagurwa alisema kazi kubwa ya ujenzi wa hospitali hiyo imekamilika kwa sehemu kubwa inatarajiwa iwapo mipango ya upatikanaji wa vifaa inaweza kuanza kutoa huduma kwa wananchi mwanzoni mwa mwezi Julai mwaka huu.
 
“Mheshimiwa mwenyekiti sehemu kubwa ya ujenzi wa hospitali yetu ya wilaya imekamilika, majengo yaliyo tayari ni pamoja na jengo la wagonjwa wa nje (OPD) jengo la kisasa la kujifungulia akinamama wajawazito, jengo la upasuaji, la kuhifadhia maiti na wodi mbili za kulaza wagonjwa kwa wanawake na wanaume ambapo ujenzi wote unatarajia kugharimu kiasi cha shilingi bilioni 1.547,”
 
Hapa ni kwenye jengo la kisasa la kuhifadhia maiti
“Kwa ujumla ujenzi kwa asilimia kubwa umekamilika, tunachosubiri hivi sasa ni kupokea vifaa mbalimbali ikiwemo samani na vitendea kazi katika jengo la upasuaji na tunatarajia mambo yakienda vizuri hospitali yetu inaweza kuanza kazi mwishoni mwa mwezi huu au mwanzoni mwa Julai, mwaka huu,” alieleza Mutagurwa.
 
Mwisho.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top