KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida wakazi wa kata ya Masekelo manispaa ya Shinyanga juzi walilazimika kususia mazishi ya mmoja wa wakazi wa kata hiyo baada ya wana ndugu kushinikiza kufanya vitendo vya kimila makaburini ikiwemo kuupasua mwili wa marehemu kabla ya kuzikwa.


Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo, kitendo cha wanandugu wa marehemu aliyetajwa kwa jina la Bernadetha Stephen (35) aliyekuwa akiishi mtaa wa Mapinduzi katika kata hiyo ya Masekelo kushinikiza kumpasua marehemu kabla ya mazishi kilisababisha kutokea kwa vurugu kubwa eneo la makaburini.

Hata hivyo awali siku moja kabla ya kuzikwa kwa marehemu huyo baadhi ya wanandugu walitishia kususia kumzika ndugu yao kutokana na kitendo cha mumewe kushindwa kumlipia mahari hali na hivyo kushinikiza walipwe kwanza kiasi cha shilingi milioni moja ndipo washiriki mazishi.

Mashuhuda hao walisema kutokana na msimamo wa wanandugu kulazimisha kutekeleza mambo yao ya kimila sehemu kubwa ya wananchi iliamua kususia mazishi hayo na kuondoka katika eneo la makaburi na kuwaacha wakiendelea kutekeleza mila zao za kikurya.

Wakifafanua walisema marehemu Bernadetha alifariki dunia Januari mosi mwaka huu akiwa katika hospitali ya mkoa wa Shinyanga akipatiwa matibabu kutokana na kusumbuliwa kwa ugonjwa wa tumbo unaohisiwa kuwa chanzo cha kifo chake ambapo mazishi yake yalifanyika juzi mchana huko katika makaburi ya kata ya Masekelo.

Walisema marehemu huyo alikuwa akisumbuliwa na uvimbe tumboni ambapo ambapo mmoja wa ndugu aliyetokea mkoani Mara inadaiwa ndiye aliyeshinikiza kufanyika kwa mambo hayo ya kimila kwa lengo la kuondoa mikosi ndani ya familia yao kutokana na wanandugu wengi kufariki dunia kwa ugonjwa huo.

Hata hivyo wanajamii waliokuwa wamehudhuria katika mazishi hayo walipinga vikali kitendo hicho na kushauri kuwa kama pangekuwa na ulazima wa kutekeleza mila hiyo basi kazi hiyo ingefanyikia hospitali eneo ambalo ni la faragha badala ya kulitekeleza mbele ya kadamnasi ya watu.

Mmoja wa mashuhuda hao (jina limehifadhiwa) alisema mgogoro huo ulianzia nyumbani kwa marehemu kabla ya kuelekea makaburini ambapo baadhi ya ndugu pamoja na kuielewa hali hiyo walionesha utulivu lakini baada ya kufika makaburini na kuanza shughuli za mazishi ndipo mmoja wa wanandugu alipoingia kaburini akiwa na wembe mkononi.

“Tulipokuwa nyumbani dalili za kutokea vurugu zilianza kujionesha, lakini sehemu kubwa ya wanandugu walitulia mpaka pale tulipofika eneo la makaburi na kuanza shughuli za mazishi, ghafla mmoja wana ndugu aliingia kaburini akiwa ameshika wembe mkononi huku amevaa glovu,”

“Wakati akiingia kaburini alikuwa pia ameshika boksi dogo ndani yake kukiwa na kifaranga cha kuku ambapo aliwazuia wananchi kuacha mara moja shughuli ya kutupia udongo kaburini ambapo ghafla alifungua sanduku lililokuwa limehifadhi mwili wa marehemu na kuanza kumchana tumbo lake kwa wembe,” alieleza shuhuda huyo.

Alisema hali hiyo iliwashitua watu wengi ambao sehemu kubwa waliamua kususia mazishi hayo na kuondoka katika eneo la makaburi ambapo ndugu huyo alimchinja kuku aliyekuwa naye na damu yake aliimwaga kwenye mwili wa marehemu na kisha kumwingiza kuku yule kwenye tumbo la marehemu kwa imani kwamba ni kumaliza mkosi ndani ya ukoo wao.

“Alipomaliza kumwingiza kuku yule katika tumbo la marehemu ndipo alipofunika tena sanduku lile na yeye kutoka nje ya kaburi ambapo aliwaomba wananchi waendelee na kazi ya ufukiaji wa kaburi lile hata hivyo sehemu kubwa ya wananchi walikuwa wameisha ondoka katika maeneo hayo ya makaburi,” aliendelea kueleza shuhuda wa tukio hilo.

Akielezea tukio hilo Ofisa mtendaji kata ya Ndala, Dickson Venance alisema kabla ya siku moja ya mazishi palitokea mgogoro kati ya aliyekuwa mume wa marehemu ukihusiana na suala la mahari ambapo walishinikiza kupasua mwili wa marehemu na kasha waondoke naokwenda kuzika kwao mkoani Mara.

“Nilijitahidi kusuluhisha mgogoro huo ambapo ndugu walikubali kulipwa kiasi cha shilingi laki moja ambapo ndugu wa upande wa mume walichangishana na kufanikiwa kupata kiasi hicho cha fedha na kuzikabidhi kwa ndugu wa marehemu walioridhia mazishi hayo kufanyika mjini Shinyanga,” alieleza Venance.

Hata hivyo ilielezwa baadhi ya wananchi waliamua kutoa taarifa za tukio hilo katika kituo cha polisi ambao walifikia katika eneo la makaburi wakati shughuli za mazishi zikiendelea na kuwakamata wanandugu wote waliohusika na uendeshaji wa shughuli kimila kinyume cha utaratibu.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Justus Kamugisha alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba wanandugu waliohusika walikamatwa na kuhojiwa kwa muda na ilipobaika ni mambo ya kimila waliachiwa huru na kuruhusiwa kuendelea na shughuli za mazishi.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top