Naibu waziri akitoa pongezi kwa watendaji wa KASHWASA eneo la mradi wa kupeleka maji kutoka Ziwa Victoria kwenda wilayani Kishapu mkoani Shinyanga.
 
Mheshimiwa Naibu waziri kazi ya kupeleka maji wilaya ya Kishapu ndivyo inavyoendelea hivi. Anaeleza Mhandisi Laurence Wasala (kushoto) anayesikiliza ni Naibu waziri wa Maji, Amos Makala.


 
Naibu waziri wa Maji, Amos Makala (mwenye suti nyeusi) na mkuu wa wilaya ya Kishapu, Wilson Nkhambaku (mwenye shati la draft) wakijionea jinsi kazi inavyoendelea.
HATIMAYE serikali imeanza kutekeleza ahadi iliyotolewa na waziri wa Maji nchini, Profesa Jumanne Maghembe ya kuwapatia wakazi wa wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga maji kutoka mradi mkubwa wa maji ya Ziwa Victoria baada ya kazi ya utandazaji wa bomba za maji kwenda wilayani humo kuanza hivi karibuni.


Mradi huo ambao ni miongoni mwa miradi mikubwa nchini unaotekelezwa kwa fedha za ndani unatarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi bilioni 13.5 utakapokamilika na unatekelezwa kwa kuwatumia watumishi wa Mamlaka ya Kusambaza Maji katika miji ya Kahama na Shinyanga (KASHWASA).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa  kwa Naibu waziri wa Maji, Amos Makala aliyekuwa katika ziara ya siku moja mkoani Shinyanga, utekelezwaji wa mradi huo unatokana na ahadi iliyotolewa na waziri maji nchini, Profesa Jumanne kwa wananchi wa wilaya ya Kishapu alipotembelea wilaya hiyo mnamo mwezi Machi, 2014.

Waziri Maghembe akiwa mkoani Shinyanga alipokea taarifa za kiufundi zilizoonesha kuwepo kwa uwezekano mkubwa wa kupanua mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Victoria kuanzia eneo la Old Shinyanga kwenye wilayani Kishapu ambapo pia kwa kuanzia vijiji 12 kando ya mtandao wa bomba hilo vitanufaika.

Akisoma taarifa yake kwa Naibu waziri, Kaimu mkurugenzi wa KASHWASA, Mhandisi Laurence Wasala ilisema mapitio ya usanifu wa mradi huo ulifanywa na Mhandisi mshauri GIBB East Africa mnamo mwaka 2008 ili kuona uwezekano wa kuunganishwa wilaya hiyo kwa gharama ndogo na kutumia watumishi wa ndani.


Kaimu Mkurugenzi wa KASHWASA, Mhandisi Laurence Wasala (wa kwanza kulia) akitoa maelezo kwa Naibu waziri wa Maji, Amos Makala juu ya kazi ya utekelezaji wa mradi wa kupeleka maji kutoka Ziwa Victoria kwenda wilayani Kishapu mkoani Shinyanga.
“Mheshimiwa Naibu waziri, kazi za upimaji na usanifu ilianza mwezi Mei 2014 na kukamilika mwezi Agosti 2014, ujenzi wa mradi ulianza rasmi mwanzoni mwa mwezi Februari, 2015 baada ya kukamilika kwa mchakato wa ununuzi wa mabomba, viungio na baadhi ya vitendea kazi,”

“Kwa ujumla ujenzi wa mradi huu umefikia kiasi cha asilimia 30 na inatarajiwa ifikapo mwishoni mwa mwezi Septemba, 2015 utakuwa umekamilika kwa upande wa eneo la Old Shinyanga na Mgodi wa Almasi wa Mwadui, kazi zote zinatekelezwa na watumishi wa ndani wa KASHWASA na kutoka kwa mzabuni wa bomba,” alieleza Mhandisi Wasala.

Akifafanua Wasala alitaja hatua iliyokwisha fikiwa katika ujenzi wa mradi huo mpaka hivi sasa ikiwemo usafishaji wa njia ya bomba yenye urefu wa mita 20,000 kati ya mita 22,800 ambayo imekamilika.

Pia uchimbaji wa mtaro wa kulaza bomba wenye urefu wa mita 21,000 kati ya mita 22,800 hadi Williamson Diamonds Ltd Mwadui, na mita 63,000 hadi mji wa Kishapu pia umekamilika.









Ulazaji na ufungaji wa bomba umekamilika urefu wa mita 12,966 kati ya mita 21,000 zilizochimbwa, ulipuaji wa miamba katika eneo la Ikonongo umekamilika na kwa sasa unaendelea katika maeneo mengine.

Aidha jumla ya valvu tano za kuondolea hewa kwenye bomba (air valves) zimefungwa kati ya 12, valvu moja ya kuondolea uchafu kwenye bomba (washout valves) kati ya sita imefungwa na bends tatu kati ya 19 zimekamilika kufungwa.

Naibu waziri wa maji nchini, Amos Makala akisisitiza jambo kwa mkuu wa wilaya ya Kishapu, mkoani Shinyanga, Wilson Nkhambaku (kushoto) muda mfupi baada ya kumaliza ziara ya kukagua mradi wa kupeleka katika wilaya ya Kishapu maji kutoka Ziwa Victoria, kulia ni mkurugenzi wa Mamlaka ya maji na Usafi wa Mazingira Manispaa ya Shinyanga (SHUWASA), mhandisi Mahola

Kwa upande wake Naibu waziri Makala aliwapongeza watumishi wa KASHWASA kwa juhudi na kazi kubwa wanazozifanya kuhakikisha mradi huo unakamilika katika muda na wakati uliopangwa ambapo aliahidi kufanyia kazi changamoto za hapa na pale zinazojitokeza ikiwemo upatikanaji wa kibali cha kupitisha bomba eneo la jeshi na reli.

“Binafsi nipongeze juhudi kubwa zinazofanywa na wizara pamoja na wenzetu wa KASHWASA, niseme tu kwa kazi  kubwa hii inayofanywa na serikali wananchi waendelee kuwa na imani na serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kama jinsi alivyoahidi waziri Maghembe, ni wazi maji haya yatafika Kishapu kwa wakati,” alieleza Makala.

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Kishapu, Wilson Nkhambaku alisema mara baada ya maji kufika katika makao makuu ya wilaya, serikali ya wilaya itashirikiana na halmashauri yake ya Kishapu kusambaza huduma ya maji katika vijiji vyote jirani ya maeneo ya mtandao wa bomba kutokea Old Shinyanga.
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top