WAFUNGWA BASIL MRAMBA (Kushoto) na DANIEL YONA (Kulia)
Siku nne baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwahukumu kifungo cha miaka mitatu jela mawaziri wa zamani katika Serikali ya Awamu ya Tatu, Daniel Yona na Basil Mramba, upande wa mashitaka umewasilisha  kusudio la kukata rufaa.


Kwa mujibu wa kusudio hilo lililowasilishwa jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wanapinga adhabu na hukumu iliyotolewa na jopo la mahakimu watatu, John Utamwa, Sam Rumanyika na Saul Kinemela, pamoja na kuachiwa huru kwa aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Gray Mgonja.

Hakimu mfawidhi wa mahakama hiyo, Cyprian Mkeha alisema kusudio hilo limeshawasilishwa na upande wa mashitaka mahakamani hapo.

Wakati upande wa mashitaka ukichukua hatua hiyo, mawakili wa kina Mramba na Yona nao wameanza mchakato wa kutaka ‘kuwachomoa’ gerezani na kuwarudisha uraiani kwa kuomba wapatiwe dhamana wakati watakapokuwa wakisubiri rufaa yao kusikilizwa.

Mramba na Yona walihukumiwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kifungo cha miaka mitatu jela baada ya kupatikana na hatia ya makosa ya matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia hasara serikali ya Sh11.5 bilioni.

Hata hivyo, wakili wa Yona, Elisa Msuya, juzi alisema kwasasa wanaandaa maombi ya dhamana na wakati wowote watafungua maombi hayo Mahakama Kuu ya Dar es Salaam, wakati wakisubiri kukata rufaa kupinga hukumu iliyotolewa.

Akizungumzia azma hiyo, Wakili wa Serikali, Charles Anindo alisema  kwa mujibu wa  kifungu cha 368 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai sura ya 20 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2009, kinaruhusu  mfungwa kuombewa dhamana wakati rufaa yake inasubiri kusikilizwa.

Hata hivyo, Wakili Anindo alibainisha kuwa kifungu hicho kinahusika tu kama kuna uwezekano mkubwa wa rufaa hiyo kushinda.

Hata hivyo, wakati Yona na Mramba wakitiwa hatiani na kuhukumiwa kifungo hicho, Mgonja aliachiwa huru baada ya mahakama kuridhika kuwa hana hatia kwa mashitaka kumi na moja yaliyokuwa yakimkabili.

Akisoma hukumu hiyo kwa niaba ya jopo la mahakimu watatu waliokuwa wakiisikiliza kesi hiyo,  Hakimu Mkazi, Sam Rumanyika alisema baada ya kupitia ushahidi uliotolewa na mashahidi 13 wa upande wa mashitaka na mashahidi sita wa upande wa utetezi wakiwamo washitakiwa wenyewe, walimuachia huru Katibu Mkuu wa zamani wa Wizara ya Fedha, Gray Mgonja kwa kuwa upande wa mashitaka ulishindwa kuthibitisha mashitaka yake pasi kuacha shaka.

Mramba alitiwa hatiani katika mashtaka yote kumi na moja yaliyokuwa yakimkabili na katika shitaka la kwanza hadi la 10 ambayo ni ya matumizi mabaya ya madaraka na kuhukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela kwa kila shitaka.

Hata hivyo, watatumia miaka mitatu tu kwani adhabu zote zinakwenda sambamba.

Katika shitaka la kumi na moja ambalo ni la kuisababishia Serikali hasara ya Sh11.7 bilioni alitiwa hatiani na kuhukumiwa kifungo cha miaka mitatu jela ama kulipa fidia ya Sh5 milioni.

Yona alitiwa hatiani kwa mashitaka manne, shtaka la kwanza, la pili, la tatu na la tano ambayo ni ya matumizi mabaya ya madaraka pamoja na la kumi na moja la kuisababishia hasara Serikali ya Sh11.7 bilioni.

Chanzo:  Mwananchi News
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top