Mamia ya wapiga kura wa Jimbo la Kisesa wakisalimiana na mbunge wao, Luhaga Mpina muda mfupi baada ya kukabidhiwa vifaa mbalimbali kwa ajili ya shughuli za uzalishaji mali. Hapa ni Kata ya Lubiga
MBUNGE anayemaliza muda wake katika Jimbo la Kisesa wilaya ya Meatu mkoani Simiyu, Luhaga Mpina (CCM) amepongezwa na wapiga kura wake kwa kitendo chake cha kutekeleza ahadi zake alizozitoa mwaka 2010 baada ya kugawa vifaa mbalimbali vyenye thamani ya shilingi milioni 200.
  
Pongezi za wananchi hao wa Kisesa zimetolewa kwa nyakati tofauti katika kata za Lubiga, Mwakisandu, Mwabusalu, Mwasengela, Sakasaka, Sanga Itenje, Isengwa na Lingeka ambapo Mpina alikabidhi vifaa kwa vikundi vya wajasiliamali wadogo na vile vya kilimo cha umwagiliaji.

Vifaa vilivyokabidhiwa ni pamoja na pampu 20 kwa ajili ya visima vifupi vya maji, pampu 31 za kilimo cha umwagiliaji, mashine moja ya kuoshea magari kwa kikundi cha vijana wanaoosha magari katika kata ya Mwandoya na pikipiki 30 kwa vijana waendesha bodaboda.

Diwani wa Kata ya Lubiga, Juma Mpina (Kulia)  akipokea vifaa kutoka kwa mbunge wa Jimbo la Kisesa, Luhaga Mpina (mwenye miwani)  kwa ajili ya wajasiliamali wa kata yake.
Vifaa vingine vilivyotolewa ni mashine mbili za kusindika mafuta ya alizeti, mashine tano za kuchakata katani, baiskeli mbili za walemavu wa viungo, vyerehani 50 kwa vikundi vya ushonaji, pikipiki tano kwa shule tano za sekondari, vitanda sita vya kujifungulia wajawazito na kompyuta 10 na printa nne kwa shule za sekondari.

Pia alikabidhi madawati 250 kwa ajili ya shule za sekondari zilizopo katika jimbo la Kisesa ambapo alisema vifaa vyote alivyovitoa ni katika kukamilisha ahadi zake alizowaahidi wapiga kura mwaka 2010 na kufafanua kuwa vifaa hivyo havitokani na mfuko wa jimbo bali amevikusanya kutoka kwa marafiki zake na sehemu ya mshahara wake.

“Nitahadharishe kitu kimoja, vifaa hivi sivitoi kama rushwa, bali ni ahadi nilizozitoa kwenu, huko nyuma tumekabidhi vitu mbalimbali na hivi vya leo ni katika kukakamilisha ahadi zangu kwenu, sehemu kubwa nimechangiwa na rafiki zangu ikiwemo watu SIDO waliotoa mashine za katani na hizi za kusindika mafuta ya alizeti,” alieleza Mpina.

Mwenekiti wa Kikundi cha Ukunaji katani Azimio katika kata ya Sakasaka, Esther Mboje (katikati) akipokea mashine mbili za kukuna katani kutoka kwa mbunge wa Jimbo la Kisesa, Luhaga Mpina, nyuma yao ni wanakikundi cha Azimio wakishuhudia makabidhiano hayo.
Wakati huo huo mbunge huyo amewashukuru wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Jimbo la Kisesa kwa kitendo chao cha kumpitisha bila kupingwa katika mchakato wa kura za maoni ambapo hakuna mwana CCM ye yote aliyejitokeza kumpinga.
  
Mpina alitoa shukrani hizo juzi katika mikutano ya hadhara iliyofanyika kwa nyakati tofauti kwenye kata mbalimbali jimboni Kisesa iliyoambatana na shughuli ya kukabidhi vifaa hivyo kwa vikundi vya wajasiliamali na vile ya kilimo cha umwagiliaji na vya watumiaji maji.

Mpina alisema hatua ya wana CCM kutokuchukua fomu kuwania kiti cha ubunge katika jimbo hilo imeonesha wazi bado wana imani naye hali iliyoonesha wazi wanathamini kazi kubwa alizowafanyia katika kipindi cha miaka 10 ya ubunge wake ambapo jimbo la Kisesa limepiga hatua kubwa katika suala zima la maendeleo.

“Nichukue fursa hii kuwashukuru sana wanachama wenzangu wa CCM kwa imani yenu kubwa mliyonionesha, kwa kweli nimeona jinsi gani mnavyothamini mchango wangu katika kuwatumikieni, na mimi naomba nitoe ahadi kwenu kwamba tarajieni mambo makubwa zaidi katika kipindi kijacho iwapo nitashinda hapo Oktoba 25, mwaka huu,”

“Jambo kubwa ninalowaomba jitokezeni kwa wingi siku ya upigaji kura Oktoba 25, mwaka huu ili muudhihirishie umma kwamba jimbo la Kisesa daima litaendelea kuongozwa na wabunge wa CCM, binafsi sioni mpinzani kutoka kwa wenzetu wa vyama upinzani, aliyeteuliwa na CHADEMA nimekuwa nikimwangusha tangu 2005, sina hofu naye,” alieleza Mpina.

PICHA ZAIDI ZA MAKABIDHIANO YA VIFAA MBALIMBALI KWA VIKUNDI VYA WAJASILIAMALI JIMBO LA KISESA. 


Mama huyu anaonesha jinsi gani alivyofurahishwa na kitendo cha mbunge wake kumkomboa kwa kumpatia vitendea kazi, kikundi chake kilikabidhiwa cherehani ya kushonea.


Wakazi wa kata ya Lingeka pia hawakusahaulika.

Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top