Mheshimiwa Mpina akisaini kitabu cha wageni katika ofisi za CCM wilayani Meatu muda mfupi kabla ya kuzungumza na mamia ya wana CCM waliojitokeza kumdhamini.
Jamani nilikuwa sitanii, bali nimedhamiria kweli kukabidhiwa kijiti na Rais Jakaya Kikwete, fomu hizi hapa!!!
Mheshimiwa Luhaga Mpina akiingia katika ukumbi wa mikutano wa CCM wilayani Meatu, Simiyu, mkono wake wa kulia akionesha mkoba wenye fomu za kuomba kugombea urais.

KADA WA CCM KUTOKA WILAYA YA MEATU MKOANI SIMIYU, LUHAGA MPINA AFUNGA ZOEZI LA KUSAKA WADHAMINI KWA KISHINDO.

·       Apata Baraka za wazazi wawili,
Baba na Mama Luhaga Mpina wakitambulishwa mbele ya wadhamini wa Mpina.

·       Mwenyekiti wa CCM wilaya ampongeza, uamuzi wake umeitangaza wilaya ya Meatu kitaifa na hadi mataifa ya nje.
Katibu wa CCM wilayani Meatu, Jonathan Mabiya akimkabidhi rasmi mheshimiwa Mpina fomu za wadhamini aliowapata katika wilaya hiyo.  Katikati anayeshuhudia ni mwenyekiti wa CCM wilayani Meatu, Juma Mwiburi (mzee wa Jumlajumla)
·       Adhaminiwa na wana CCM 945.


Meatu Simiyu.

MMOJA wa makada wa Chama cha Mapinduzi (CCM) anayeomba kuteuliwa na chama chake kupeperusha bendera ya CCM katika kinyang’anyiro cha urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Luhaga Mpina amekamilisha rasmi zoezi la kutafuta wadhamini 450 katika mikoa 15 ikiwemo mitatu ya Tanzania Zanzibar.

Mpina ambaye pia ni mbunge wa Jimbo la Kisesa amehitimisha zoezi hilo Juni 27, mwaka huu mjini Mwanhuzi wilayani Meatu mkoa wa Simiyu ambako alipata wadhamini 945 waliojitokeza kumuunga mkono katika adhima yake ya kuomba kuteuliwa kugombea nafasi ya urais kwa tiketi ya CCM katika uchaguzi mkuu utakaofanyika nchini, Oktoba 25, mwaka huu.

Katika hafla fupi ya kukamilisha idadi ya wadhamini wanaotakiwa kwa mujibu wa kanuni zilizotolewa na uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) zilizofanyika katika viwanja vya Ofisi ya CCM mjini Mwanhuzi iliyohudhuriwa na mamia ya wana CCM wilayani Meatu, Luhaga alieleza furaha yake isiyo na kifani kwa jinsi wana CCM wenzake walivyojitokeza kumuunga mkono.

Alisema mbali ya wana CCM wa Meatu ambako ndiko alikozaliwa lakini pia alipata mapokezi makubwa na yenye kutia moyo katika safari yake aliyoikusudia katika mikoa mingine 16 aliyotembelea kutafuta wadhamini wa kumdhamini na kwamba kila alikokwenda wana CCM walionesha dhahiri kumuunga mkono huku wengi wao wakisema awamu ya rais wa tano ni lazima iongozwe na rais kijana, mfano wake Mpina.

Miongoni mwa walioshiriki katika hafla hiyo ni wazazi wawili, Baba na Mama wa Mheshimiwa Mpina, ambao kutokana na furaha waliyosema walisema hawakuwa na la kueleza na kwamba wanaamini mtoto waliyemzaa si wakwao peke yao bali ni wa watu wa Meatu nzima, na kwamba kupata kwake nafasi hiyo ya urais itakuwa si sifa yao wazazi peke yao bali kwa wana Meatu na mkoa wa Simiyu kwa ujumla.

Mama mzazi wa Mheshimiwa Mpina (mwenye kitambaa kichwani) akifuatilia kwa makini hotuba ya mwanae katika ukumbi wa CCM wilaya Meatu, Simiyu.
Ahsanteni sana jamani, tuombeane dua njema, nipasue kule Dodoma, Juni 12, 2015.
Awali akimkaribisha kuzungumza na wana CCM waliojiotokeza kumdhamini, mwenyekiti wa CCM wilayani Meatu, Juma Mwiburi alimshukuru Mpina kwa uamuzi wake sahihi wa kuamua kuwania kuteuliwa ili aweze kugombea nafasi hiyo kubwa ndani ya nchi na chama chake na kwamba kutokana na ujasiri wake anaamini ataimudu vyema.

“Kwa uwezo wako ninavyokuelewa na umahiri 
wako, mwenyezi mungu atakubaliki, kwa sababu tutakubaliki kuanzia sisi kuanzia leo tunakuombea kwa mwenyezi mungu mradi jina lifike tu mbele ya mkutano mkuu, tayari umeisha kuwa rais,”

“Naelewa huna ubaguzi, na moyo wako nauelewa, na uchapa kazi wako, naamini mzee Mpina hakukosea, ni baraka zako, na mama amesema si yeye peke yake aliyekuzaa bali wote tumekuzaa, sasa tunakuombea kwa mwenyezi mungu safari hii ni ndefu, lakini kwa maombi tunayoomba wilaya nzima ya Meatu na mkoa mzima wa Simiyu, tunakuombea na kukutakia kila la kheri,” alieleza Mwiburi.

Kwa upande wake katibu wa CCM wilayani Meatu, Jonathan Mabiya alisema jumla ya wana CCM 945, kati yao 900 waliotoka ngazi ya kata, na 45 kutoka ofisi ya wilaya walijitokeza kumdhamini mheshimiwa Mpina, na kwamba fomu zote zilizowekwa saini na wadhamini hao na kugongwa mhuri wa CCM na mkurugenzi wa uchaguzi wilayani humo ambaye ni yeye zimekamilika kikamilifu.

“Mheshimiwa Mpina tunakuombea kwa mwenyezi mungu akutangulie katika safari yako ya urejeshaji wa fomu hizo makao makuu ya Chama mkoani Dodoma, nikuhakikishie wanachama wote waliojitokeza kukudhamini ni wanachama safi na hai wa Chama cha Mapinduzi, wanazo kadi na wamelipia ada zao, ni hai kabisa, tunaamini kazi hii tumeifanya kwa umakini, ni wazi mkoa wa Simiyu tumeuwakilisha vizuri,” alieleza Mabiya.

NAKUSHUKURUNI SANA!! SANA!! KWA KUNIUNGA MKONO.
Mheshimiwa Mpina akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na wadhamini wake.

Akizungumza na wana CCM waliojitokeza kumdhamini na wanachama wengine kwa ujumla, Mpina alisema uamuzi wake wa kuomba kuteuliwa kugombea nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano aliuchukua baada ya kujipima na kuona anaweza kuiongoza nchi ya Tanzania, na chama chake cha CCM akiwa mwenyekiti wa CCM wa Taifa.

Mpina alisema mbali ya kuamini anaweza kuongoza nafasi hiyo kubwa katika taifa la Tanzania, lakini pia ni haki yake ya kikatiba na ni katika kutekeleza kwa vitendo demokrasia na hatua hiyo ni kutimiza ahadi yake ya awali kwa wakazi wa wilaya ya Meatu aliyoitoa Mei 31, mwaka huu kwamba atagombea nafasi hiyo ya urais, na kweli ametimiza ahadi hiyo.

“Ndugu zangu nataka niwathibitishie kwamba ile ahadi yangu niliyoitoa Mei 31, mwaka huu nimeenda kutekeleza na ndiyo mkoba huu mnaouona ninao hapa ambao nilikabidhiwa pale CCM makao makuu, Dodoma, ukiwa na fomu ya kuomba uteuzi na zile za wadhamini wanaohitajika kunidhamini,”

“Lakini niwaeleza ukweli katika mikoa yote 17 niliyotembelea kutafuta wadhamini, kabla ya kukaribishwa kuzungumza na wadhamini wangu, watu waliokuwa wakiulizana, mbona mgombea urais hatumuoni hapa, hii ni kutoka na umbile la mwili wangu kuwa dogo,”

“Na hata pale nilipokuwa nikisimama watu walionesha wasiwasi, hata baada ya kumaliza kuwahutubia wengi walinikubali, na wengine kusema wazi huyu ndiye Rais tunayemtaka, ni kutokana na jinsi nilivyokuwa nikijieleza, walithibitisha ninafaa kwa nafasi hii ninayoiomba, na kila sehemu tulikuwa tukiombewa dua,” alieleza Mpina.

Mpina aliiitaja mikoa 17 aliyoitembelea kusaka wadhamini 450 ukiwemo mkoa wa Simiyu, na kwamba maeneo mengi walipata wadhamini wengi na hata hivyo walizingatia hitaji na maelekezo ya CCM makao makuu ya wadhamini 450, na kwamba katika mikoa yote walipata wadhamini safi wenye sifa zote zilizoainishwa.

Aliitaja mikoa mingine mbali ya Simiyu kuwa ni pamoja na Dodoma, Shinyanga, Singida, Tabora, Mwanza, Kilimanjaro, Manyara, Arusha, Tanga, Morogoro, Pwani, Iringa, Manyara, Mjini Unguja, Mjini Magharibi na Kusini Unguja.

Hata hivyo Mpina alisema kwa mujibu wa maelekezo ya sheria na kanuni yaliyotolewa na CCM makao makuu asingeweza kuzungumzia mengi kuhusiana na adhima yake ya kutaka kuteuliwa kugombea nafasi hiyo ya urais kwa vile kufanya hivyo itakuwa ni sawa na kuanza kampeni na atakuwa amekwenda kinyume na maelekezo hayo.

“Baada ya kuchukua fomu pale Dodoma, tulipewa nafasi ya kutangaza nia na nafasi ya kuongea kidogo nini tunachofikiria kukifanyia Chama chetu cha Mapinduzi lakini pia utaifanyia nini nchi yako, hayo yote yaliisha fanyika, sasa hivi haturuhusiwi tena  kuanza kuzungumza kana kwamba unafanya kampeni, ukifanya hivyo unakuwa tayari umepoteza,” alieleza.

Hata hivyo alisema wengi walikuwa wakimpigia simu na kumuuliza kwa nini ameamua kugombea nafasi hiyo ya urais, ambapo aliwajibu kuwa yeye ni mwana CCM na anayo haki ya kugombea nafasi hiyo ambayo muda si mrefu itabaki wazi baada ya Rais aliyepo madarakani kukamilisha kipindi chake cha miaka 10.

“Ndugu zangu kwa kifupi tu niwathibitishie tena kwamba nafasi hii ninaimudu, na niwaeleze wazi kati ya watia nia wengine wapatao 39, sioni atakayenishinda iwapo haki itatendeka, maana muda mrefu nilikuwa nikiomba kwa mungu taifa letu liweze kupata kiongozi mzuri atakayeliongoza taifa hili, lakini kila nilipoomba, mwenyezi mungu alinijibu, ni wewe mwenyewe Mpina ndiyo unayefaa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alieleza na kushangiliwa.

Mpina alitarajia kwenda mkoani Dodoma siku ya Jumanne, Juni 30, mwaka huu kwa lengo la kukabidhi rasmi fomu zake za kuomba kugombea nafasi hiyo ya urais ambazo zimeambatanishwa pamoja na fomu zote za wadhamini wake 450.


Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top