Moja ya Nyumba zilizoezuliwa na upepo katika kijiji cha Mwakata wilayani Kahama.




Mbuzi hawa ni miongoni mwa mifugo iliyokufa kutokana na mvua hiyo iliyoambatana na upepo na mawe makubwa ya saruji.
WATU 42 wakazi wa kijiji cha Mwakata kata ya Mwakata wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga wamekufa huku wengine 89 wakijeruhiwa vibaya baada ya nyumba zao kubomolewa na mvua kubwa iliyonyesha usiku wa kuamkia Machi 4, mwaka huu ikiambatana na upepo mkali na mawe makubwa ya saruji.



Mbali ya kupoteza maisha ya watu pia mifugo kadhaa ikiwemo ng’ombe, mbuzi na punda imekufa kufuatia mvua hiyo iliyonyesha kijijini hapo kwa zaidi ya saa moja huku ikiharibu mazao mbalimbali ya chakula mashambani na kuacha familia kadhaa zikiwa hazina makazi.

Baadhi ya wakazi wa kijiji hicho walionusurika katika tukio hilo wamelieleza Majira kwamba mvua hiyo ilianza kunyesha mnamo saa 4.00 usiku hadi saa 5.02 usiku wa kuamkia Machi 4, 2014 ikiambatana na upepo mkali na mawe makubwa ya saruji yenye ukubwa wa ndoo ndogo za plastiki zenye ujazo wa lita 10.

Wanakijiji hao walisema maeneo yaliyoathiriwa vibaya na mvua hiyo ni pamoja na kijiji cha Mwakata, Nhumbi na Mangung’humwa katika kata hiyo ya Mwakata na kwamba mpaka sasa familia kadhaa hazina makazi baada ya nyumba zao kubomoka.

“Mimi binafsi nyumba zangu mbili zimebomolewa na baadhi ya wateja wangu waliokuwa katika matibabu (tiba za jadi) wawili wamejeruhiwa na wamepelekwa hospitali ya serikali mjini Kahama kupatiwa matibabu, mvua hii imetushangaza sana, maana ilikuwa inateremsha mawe makubwa mfano wa ndoo ndogo,”

“Watu wengi wamepoteza maisha, hali hii haijawahi kutokea hapa kwetu hata wakati wa mvua zile za El-nino haikuwa hivi, ni hatari sana maana watu wengi wameangukiwa nyumba wakiwa ndani na wengine kujeruhiwa na mawe ya mvua, maana yalikuwa makubwa sana,” alieleza Machimu Ndalo ambaye ni mganga wa jadi kijijini hapo.

Akizungumzia tukio hilo mkuu wa wilaya ya Kahama, Benson Mpesya alisema watu 35 walifia katika eneo la tukio huku wengine watatu wakifia katika hospitali ya wilaya mjini Kahama walikopelekwa kwa ajili ya kupatiwa matibabu.

“Ni kweli kumetokea maafa makubwa yaliyosababishwa na mvua kubwa iliyonyesha usiku wa kuamkia leo (jana), na hapa ninapozungumza na wewe tayari tumeopoa miili ya watu 35 iliyokuwa imefunikwa na nyumba zilizoanguka, hali ni mbaya sana, wengine watatu wamefia hospitali mjini Kahama mida hii,” alieleza Mpesya.

Hata hivyo mkuu huyo alisema mpaka hiyo jana mchana walikuwa bado wanaendelea na ukaguzi zaidi katika kila kaya ili kuweza kubaini idadi halisi ya watu waliopoteza maisha kutokana na mvua hiyo na ukubwa wa hasara iliyopatikana ikiwemo mifugo na mazao yaliyoharibika.

Naye Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani Shinyanga, Elisa Mugisha alisema baada ya kupata taarifa za kuwepo kwa tukio hilo kikosi cha Zimamoto kilikwenda katika kijiji hicho kwa ajili ya shughuli za uokoaji sambamba na kuwawahisha katika hospitali ya wilaya majeruhi waliojeruhiwa na mvua hiyo.

Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Ally Rufunga alithibitisha kutokea kwa vifo vya watu 42 na majeruhi 89 waliopatikana na kukimbizwa katika hospitali ya serikali mjini Kahama kupatiwa matibabu na kwamba idadi kubwa ya waliokufa ni watoto wadogo.



Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top