Mbunge wa Jimbo la Shinyanga mjini, Stephen Masele akizungumza na wananchi wa mji wa Shinyanga wakiwemo wanachama wa timu ya Stand United (Chama la Wana).
TIMU ya Stand United maarufu kwa jina la “Chama la wana” ya mkoani Shinyanga imepata mfadhili mwingine mpya atakayeidhamini timu hiyo katika msimu huu wa ligi ya Vodacom kwa shilingi milioni 100.
 
Mdhamini huyo ni Kampuni ya Biko inayoendesha michezo ya kubahatisha kupitia mitandao ya simu hapa nchini ambayo imefikia makubaliano na timu hiyo inayocheza ligi ya Vodacom (VPL) kwa kuidhamini kwa kipindi cha msimu mmoja wa 2017/2018.
 
Akitoa taarifa hiyo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika mjini Shinyanga, mbunge wa Jimbo la Shinyanga mjini, Stephen Masele alisema kampuni ya Biko imekubali kutoa udhamini wa shilingi milioni 100 kwa timu hiyo ikiwa ni pamoja na vifaa vya michezo.
 
Masele alisema iwapo Stand United wataonesha mwenendo mzuri kwenye ligi ya mwaka huu, Biko itaongeza udhamini wake katika msimu ujao wa 2018/2019 kwa kuipatia timu hiyo kiasi cha shilingi milioni 200.
 
Hatua hiyo ya kampuni ya Biko imetajwa itaisaidia zaidi timu ya Stand United ambayo katika msimu uliopita ilikumbwa na mgogoro mkubwa na kusababisha kumpoteza mdhamini wake aliyekuwa akiidhamini, kampuni ya Acacia aliyeamua kujitoa.
 
Kwa upande wake Masele alisema baada ya timu hiyo kupata viongozi wake waliochaguliwa na wanachama wenyewe hivi na yeye mwenyewe sasa ameamua kuisimamia kwa ukaribu zaidi ili iweze kufanya vizuri kwenye ligi ya mwaka huu sambamba na kudhibiti matumizi ya fedha za Klabu.
 
“Ndugu wanachama na wapenzi wa timu yetu ya Stand, leo kwetu ni siku ya furaha baada ya kupata mdhamini mwingine aliyekubali kuidhamini timu yetu kwa kipindi cha mwaka mmoja huu wa 2017, hii ni baada ya kumpoteza mfadhili wa awali kampuni ya Acacia,”
 
“Nimezungumza na wamiliki wa kampuni ya Biko, wamekubali kutushika mkono, na wameahidi tukifanya vizuri, msimu ujao wa 2018/2019 wataongeza ufadhili wao ambapo utafikia shilingi milioni 200, na mimi leo nimeamua kujitolea rasmi kuisimamia timu kwa ukaribu zaidi ili iweze kufanya vizuri,” alieleza Masele.
 
Masele alifafanua kuwa katika msimu uliopita aliweza kutafuta wafadhili kampuni ya Acacia  waliokubali kuidhamini timu kwa kiasi cha shilingi bilioni 2.4, lakini baada ya kujitokeza mvutano kati ya pande mbili za Stand wanachama na Stand Kampuni, Acacia waliamua kujitoa.
 
Kwa upande wake mwenyekiti wa Klabu ya Stand United, Dkt. Ellyson Maeja alishukuru mchango wa mbunge kuwezesha timu hiyo kupata mfadhili mwingine na kwamba kwa upande wao wanachama na viongozi hivi sasa wana mshikamano mzuri.
 
“Tunakushukuru sana mbunge Masele, kwa kweli udhamini huu umekuja kwa wakati muafaka, maana ndiyo kwanza timu imeanza michezo yake ya ligi, tunaamini zile changamoto tulizonazo kwa sasa zitapungua kwa kiasi kikubwa, na sisi tunaahidi kuutumia vyema ufadhili huu wa Biko,” alieleza Dkt. Maeja.
 
Mbunge Masele na mwenyekiti wa Klabu ya Stand United Shinyanga, Dkt. Maeja.
Mmoja wa wanachama wa Stand United, Omari Malula akitoa mchango wake wa mawazo wa jinsi ya kuiwezesha timu yao kufanya vizuri katika ligi kuu ya 2017/2018

Baadhi ya viongozi na wapenzi wa Timu ya Stand United wakifuatilia hotuba ya mbunge Masele
 
Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Asante kwa kutembelea mtandao huu

Post a Comment

 
Top